Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 2 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 29 2023-08-30

Name

Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JUDITH S. KAPINGA K.n.y. MHE. ZAINAB A. KATIMBA aliuliza: -

Je, lini Serikali itaboresha Mitaala ya Elimu ili mafunzo ya biashara yatolewe kuanzia shule za Msingi?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Athman Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara iko katika hatua za ukamilishaji wa mapitio ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya 2014 na Mitaala katika ngazi ya Elimu ya Awali, Msingi, Sekondari na Mafunzo ya Ualimu. Aidha, Wizara imevielekeza Vyuo Vikuu kuhuisha na kufanya maboresho ya mitaala yote ili iendane na Dira na Mipango ya Maendeleo ya Taifa katika kutoa elimu itakayompa kijana wa Kitanzania ujuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inatambua umuhimu wa Somo la Biashara na hivyo somo hili limepangwa kuwa ni somo la lazima kwa wanafunzi wote kuanzia Kidato cha kwanza hadi cha nne kwa mikondo yote miwili ya elimu ya jumla na elimu ya amali. Aidha, kwa ngazi ya elimu ya msingi darasa la I - VI mitaala imetilia mkazo elimu ya fedha pamoja na elimu ya ujasiriamali ambapo elimu ya fedha imechopekwa kwenye somo la Hisabati na elimu ya ujasiriamali imechopekwa kwenye somo la sanaa na michezo, lugha, jiografia na mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, Vyuo Vikuu vya Serikali na Binafsi kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (Higher Education for Economic Transformation – HEET) vimepata mafunzo mbalimbali ya kuandaa programu zinazoendana na vipaumbele vya nchi na mahitaji ya soko la ajira. Kupitia utaratibu huu, zaidi ya programu 300 zitaanzishwa na kuhuishwa ikiwemo somo la biashara ili kuendana na mahitaji ya sasa ya kijamii, kiuchumi na soko la ajira. (Makofi)