Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 1 Energy and Minerals Wizara ya Madini 12 2023-08-29

Name

Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Primary Question

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawasaidia wanawake na vijana wa Kata za Mitesa na Nanjota wanaojihusisha na uchimbaji madini Lulindi?

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Lulindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Mtwara umebarikiwa kuwa na madini mbalimbali yakiwemo madini ya ujenzi ambayo huchimbwa zaidi na wananchi hasa wanawake na vijana. Aidha, Tume ya Madini imetoa leseni za uchimbaji madini ya ujenzi na chumvi kwa vikundi 11 vya wanawake na vijana. Vikundi hivyo ni pamoja na Mtazamo Group, Wazawa Group, Mwambani Group, Wasikivu, Songambele Group, Tusaidiane, Nguvu Kazi Youth Group katika Halmashauri ya Mji wa Masasi na Kikundi cha Kiumante kilichopo katika Manispaa ya Mtwara – Mikindani; Vikundi vya Makonde Salt Group, Mapinduzi na Umoja wa Vijana vilivyopo katika Halmashauri ya Mtwara Vijijini.
Mheshimiwa Spika, ili kuweza kuwasaidia wanawake na vijana wanaojishughulisha na uchimbaji wa madini katika Kata za Mitesa na Nanjota, tunawashauri Wanawake na Vijana wajiunge kwenye vikundi na kusajiliwa katika Halmashauri husika. Kufanya hivyo itakuwa rahisi kuwahudumia na kuwasaidia kupatiwa leseni za uchimbaji na mikopo kutoka Halmashauri husika na hata mabenki.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Madini tutaendelea kutoa elimu kwa wananchi ikiwa ni pamoja na kuwahamasisha kujiunga katika vikundi ili kuweza kupatiwa huduma kwa ufanisi na kwa haraka zaidi.