Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 1 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 2 2023-08-29

Name

Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza: -

Je, lini Serikali itamaliza ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kata ya Kizazi – Kibondo?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa leo ni siku yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kwa takribani miezi mitatu tangu nipate changamoto za kiafya, naomba kwa dhati ya moyo wangu nitoe shukrani zifuatazo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, namshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aliyenijalia uhai, afya njema na kuniwezesha kurejea kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu katika kulijenga Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pili, kwa dhati ya moyo wangu, nitumie fursa hii ya Bunge tukufu kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo ameniwezesha kwa upendo wake na wema wake kwangu na Watanzania wote na kuniwezesha kupata matibabu na hatimaye kurejea kuendelea kulijenga Taifa letu. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais na tunamwombea sisi Watanzania aendelee kuwa na afya njema aendelee kuliongoza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, nawashukuru sana Viongozi Wakuu wa Serikali, nikianza na Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ninamshukuru sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Namshukuru sana kwa ushirikiano wake.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana wewe mwenyewe binafsi Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Spika wa viwango mwenye upendo. Ninakushukuru sana sana kwa ushirikiano wako na Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumshukuru Bosi wangu, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Jasmine Kairuki, alikuwa nami muda wote na katika kila hatua ya matibabu yangu; na pia Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu, Mheshimiwa Deo Ndejembi; Katibu Mkuu Ndunguru; na timu nzima ya Ofisi ya Rais TAMISEMI; ninawashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Mawaziri wote, Waheshimiwa Naibu Mawaziri wote na Waheshimiwa Wabunge wenzangu, nawashukuru sana, sana kwa upendo wenu na Mwenyezi Mungu awabariki sana kwa maombi yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru viongozi wangu wa Chama cha Mapinduzi wa Jimbo langu la Wanging’ombe, Baraza la Madiwani, viongozi wa Serikali, wananchi wenzangu wa Jimbo la Wanging’ombe kwa maombi yao siku zote. Niwahakikishie kwamba nitaendelea kuchapa kazi kuijenga Wanging’ombe na pia kujenga Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, mwisho lakini siyo kwa umuhimu, namshukuru sana mke wangu mpenzi, Alafisa Moses Dugange kwa namna alivyokuwa karibu nami katika kipindi chote cha matibabu. Ninawashukuru sana, sana na Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, sasa naomba nianze kujibu maswali ya Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Kizazi Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo. Bajeti hiyo itatekeleza ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD), jengo la maabara, jengo la wazazi, jengo la upasuaji na jengo la kufulia, ahsante sana.