Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 22 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 183 2021-05-04

Name

Najma Murtaza Giga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA aliuliza:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuwa na Sera na Mitaala shirikishi ili kuwa na msingi wa aina moja kuanzia elimu ya maandalizi, elimu msingi na sekondari kati ya Tanzania Bara na Zanzibar ili kuongeza ufaulu zaidi kwa upande wa Zanzibar?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kabla sijajibu swali la Mheshimiwa Mbunge, naomba kuchukua fursa hii kuwatakia heri wanafunzi wetu wote wa kidato cha sita walioanza mitihani yao siku ya jana ambayo itaendelea mpaka tarehe 25. Tuna watahiniwa wa kidato cha sita 81,343 katika vituo 808 kote nchini. Sambamba na hao vilevile tuna watahiniwa 6,973 wa vyuo vya ualimu ambao nao vilevile wanafanya mitihani yao katika vyuo 75 nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imekuwa ikishirikiana vizuri na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika masuala mbalimbali ikiwemo suala la elimu hususan katika utekelezaji wa mitaala na kutoa elimu bora kwa watoto wa Kitanzania.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Sera na Mitaala shirikishi baina ya pande mbili za Muungano, Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) hushirikiana na Taasisi ya Elimu Zanzibar (TEZ) katika masuala mbalimbali yahusuyo utekelezaji wa mitaala. Ushirikiano huu hutoa fursa mbalimbali ikiwemo mijadala kuhusu utekelezaji wa mitaala na jinsi ya kukabiliana na changamoto mbalimbali zitokanazo na ufundishaji na ujifunzaji wa wanafunzi. Aidha, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inafanya mapitio ya Sera ya Elimu ili kuweka uwiano wa miaka kwa Elimu ya Msingi baina ya Tanzania Zanzibar na Tanzania Bara. Hivyo, nitoe rai kwa Watanzania wote kutumia nafasi hii ili kutoa maoni yao kuhusu mfumo huo. Ahsante.