Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 22 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 184 2019-05-07

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Mapema mwaka 2016 Waziri wa Nishati alifanya uzinduzi wa Mradi wa Umeme wa REA na kuagiza Vijiji vya Sarakwa, Tingirima, Rakana, Nyang’aranga, Nyamakumbo, Saba–Osanza, Mmagunga, Nyabuzume, Bukama, Tiring’ati, Bigegu, Nyaburundu, Masaba, Nyansirori, Nyamuswa A, Saloka-Guta, Mahanga, Manchimweru, Nyangere, Makongoro A na B na Nyamuswa kupatiwa umeme:-

(a) Je, ni lini kifanyike ili miradi ya vijiji 21 ikamilike kwa wakati kama Serikali ilivyoahidi?

(b) Je, ni nani aliyepanga kijiji A kipate kilomita tatu, transfoma mbili au nguzo 20 na umeme upitie eneo bila kushirikisha vijiji na hata bila kujali wingi wa kaya?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja, kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendeelea kutekeleza mradi wa kupeleka umeme katika Vijiji vya Bunda vikiwemo vijiji 21 kupitia kampuni ya Derm Electric Company Limited. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2019, mkandarasi alishawasha umeme katika Vijiji vya Nyangere, Bukama, Mugaja Centre, Marambeka, Bunere, Shule ya Msingi Mugaja pamoja na kuunganisha umeme wateja wa awali 289.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa mkandarasi anaendelea na kazi ya kusimika nguzo, kuvuta nyaya na kufunga transfoma katika Vijiji vya Sarakwa, Tingirima, Rakana, Nyang’aranga, Nyabuzume, Tiring’ati, Bigegu, Nyaburundu, Guta B, Mahanga, Manchimweru na Makongoro A na B. Kazi za mradi wa kupeleka umeme katika vijiji hivyo inahusisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 74.8; njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 120; ufungaji wa transfoma 53 za KVA 50 na 100; pamoja na kuunganisha umeme kwa wateja wa awali 1,141. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 7.08 na kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi itakamilika ifikapo mwezi Juni, 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Vijiji vya Nyamakumbo, Saba – Osanza, Mmagunga, Masaba, Nyansirori na Nyamuswa vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III, mzunguko wa pili, unaotarajiwa kuanza Mwezi Julai, 2020 na kukamilika mwezi Juni, 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya upimaji hufanywa na Serikali kupitia TANESCO, REA na viongozi wa Serikali za Vijiji husika. Kipaumbele ni kupeleka umeme katika maeneo yasiyokuwa na miundombinu ya umeme na katika taasisi zinazotoa huduma za kijamii kama vile vituo vya afya, zahanati, shule na kadhalika. Hata hivyo, ukubwa wa wigo wa mradi wa usambazaji umeme katika mkoa, wilaya na kijiji husika hutegemea zaidi upatikanaji wa fedha.