Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Saashisha Elinikyo Mafuwe (19 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nianze kumshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ametupa uzima na zawadi ya kuwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli, Rais ambaye amefanya mengi na ambaye tunategemea ataendelea kuyafanya mengi kwa kipindi cha miaka mitano iliyobaki. Pia nishukuru sana viongozi wenzake Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani za pekee ziende kwa watumishi wa umma Tanzania nzima. Hawa ndiyo wanaotekeleza mipango ambayo sisi tunaipanga hapa na kama ambavyo wamemsikia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba wasiwe na wasiwasi Serikali yao inawapenda na kama alivyosema Mheshimiwa Rais yeye haongezi vibaba vibaba ataongeza mzigo wa kutosha, kwa hiyo, waendelee kushirikiana nasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, lipo jambo nimeliona hapa. Wakati najiandaa kuchangia hapa, nimesoma kwanza Mpango uliopita yale mapendekezo yaliyoletwa humu Bungeni, nikasoma Hansard za Wabunge walivyochangia na nikapitia kwenye changamoto ambazo zimesababisha Mpango ule usitekelezwe kwa asilimia 100, nikajifunza kitu ambacho naomba sasa wakati Waziri anakuja kuhitimisha atuambie hapa ni kwa asilimia ngapi hii michango ya Wabunge hapa inaenda kufanya mabadiliko kwenye rasimu hii tunayoijadili na kuleta Mpango ulio kamili? Tusipopata asilimia ya namna ambavyo michango yetu inaingizwa kwenye Mpango huu na mabadiliko yakatokea tutakuwa tunazungumza hapa halafu hayafanyiwi kazi. Kwa hiyo, niombe sana wakati anakuja kuhitimisha atuambie michango yetu imeingizwa kwenye Mpango huu kwa asilimia ngapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo lingine, wote hapa tunasema, hata dada zangu kule wanakiri kwamba Mheshimiwa Rais anafanya kazi nzuri mno ya kutukuka lakini swali langu, hii kazi nzuri inayofanywa na Mheshimiwa Rais itakuwa sustainable, itaendelea kuishi? Hii miradi mikubwa inayoanzishwa na Serikali itaendelea hata kama yeye hayupo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachokishauri sasa tuweke mifumo ambayo itasaidia hizi shughuli nzuri zinazofanywa ziendelee kuishi. Hapa kuna wanasheria na Mwanasheria wa Serikali atusaidie, huko kwenye nchi zilizoendelea wana vitu vyao kama interest za Taifa lao, hivi hapa Tanzania hatuwezi kuwa na mambo yetu ambayo ni interest ya Tanzania na yakae kwenye Mpango wa muda mrefu hata kama ni miaka 50 kwa kuanzia baadaye twende miaka 100 ili tuwe na Mipango ya muda mfupi ya mwaka mmoja kama tunavyojadili sasa hivi lakini tuwe na Mipango ya miaka mitano?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nayasema haya kwa sababu tunafahamu namna siasa zetu zinavyoenda. Mara nyingi unakuta viongozi wanacheza beat kulingana na mpigaji anavyopiga ngoma. Sasa tunataka tutengeneze ngoma ya Watanzania ambayo tunaweza kuipiga kwa kipindi cha miaka 50 tuone hayo mambo ambayo yamewekwa yawe ni msingi na yaendelee. Namna ya kuyafanya yawe endelevu ni sisi Wabunge kuweka sheria za kubana lakini pia kuwa na taasisi ambazo ni strong zinazoweza kufanya maamuzi na kuyasimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo tutakuwa tumemfaidi Mheshimiwa Rais tuliyenaye sisi wa kizazi hiki na kizazi kijacho. Tukiacha haya, iko hatari kwamba akiondoka Mheshimiwa Rais na haya yataondoka, atakuja mwingine tutacheza ngoma nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe pia hebu tutazame mfumo wa elimu ya Tanzania, je, unatupa output nzuri kwa watu wetu? Wapo Wabunge wamechangia hapa na utaona kuna kitu ambacho tunakifanya. Sisi tuna-base kwenye kuangalia mazingira zaidi lakini ubora wa elimu bado hatujauweka vizuri. Je, mtaala tulionao una-reflect National objectives maana yake ni kwamba hii Mipango ya Taifa tunayoipanga tukienda kwenye mitaala yetu tunaikuta? Tunataka Serikali ya viwanda, je, mifumo ya elimu inatupeleka huko kuandaa watu waje wafanye kazi kwenye viwanda hivi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe pia wakati tunapanga Mipango hii tutazame pia suala la mitaala yetu. Kwa sababu moja ya changamoto iliyosababisha Mpango ule usitekelezwe kwa asilimia 100 ni kwamba nchi hii hatuna wataalam wa kuandika maandiko. Hii siyo sawa, watoto wanamaliza vyuo kila siku tunawezaje kuweka challenge kama hii, kwa hiyo, kuna shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine hapa tunaangalia michango yetu na hili siyo zuri sana ninavyolitazama mimi. Nitoe mfano mtoto wangu aliniuliza swali juzi hapa, akaniuliza baba hebu niambie, mle Bungeni kuna Mbunge anaitwa Musukuma na Mbunge mwingine wa Kahama, wanachangia vizuri kweli lakini wao wanasema darasa la saba. Zaidi ya hivyo, tunaambiwa wamefanikiwa kwenye maisha, hivi kuna sababu ya kusoma?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili swali ingekuwa ni wewe, ungemjibuje mtoto akikuuliza kitu cha namna hiyo? Iko sababu ya kupita kwenye mfumo wa elimu ili tuweze kuwa na wataalam ambao wana output nzuri. Hata hii tunayosema kuwa sisi tuna sera nzuri, sera nzuri ni ile ambayo ina strong tools of implementation ambazo zinaleta output nzuri. Kwa hiyo na hili pia tunapoangalia tulitazame. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nimetaka kuchangia ni kwenye kilimo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda hauko upande wako Mheshimiwa.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kilimo…

MWENYEKITI: Dakika tano tayari zimeisha.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo nilikuwa naanza? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa dakika moja tu tafadhali sana, kwa kuwa Jimbo la Hai lilifanya kazi kubwa sana, naomba niongezee.

MWENYEKITI: Haya, dakika moja.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwenye eneo la kilimo. Pale Hai tukiamua kuna vyanzo vya maji vya kutosha, kuna ardhi nzuri tuko tayari kufanya kazi. Tukipewa vyanzo hivi vya maji tutalima na tutachangia kwenye Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye Vyama vya Ushirika, kaka yangu Mheshimiwa Nape tumezungumza sana, iko shida. Kule Hai hatuna ardhi ya kutosha lakini tuko tayari kufanya kazi lakini Vyama vya Ushirika vimekumbatia mashamba yetu, wanachokifanya mle ndani hatujui, ukiwaambia ni wataalam wa kufanya lobbying za kutosha. Tafadhali sana ile team niliyoomba iende kule Hai, Mheshimiwa Waziri Mkuu uko hapa, iko shida, uko utajiri mkubwa kule Hai kama tukiamua kufanya kazi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana Mungu ambaye ametupa afya na uzima. Pia kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Hai, naomba niishukuru sana Serikali kwa namna ambavyo wanatujali, sasa hivi tunaona raha ya kuchagua Chama cha Mapinduzi. Raha hiyo tunaiona kwa sababu tayari tumekwisha kutengewa fedha kwa ajili ya mradi wa maji pale Kikafu, naishukuru sana Serikali.

Pia tumefanyiwa ukarabati wa shule zetu mbili; Lyamungo na Machame Girls. Vilevile tumeonja angalau lami japo kwa mita chache lakini ndiyo zimeingia kwa sababu tulichagua Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kubwa sana hili ambalo tumelipata tumetengewa shilingi bilioni 1.6 kwa sababu ya kufufua Kiwanda cha Machine Tools. Hii ndiyo raha ya kuchagua Chama cha Mapinduzi, nawashukuru sana. Si hivyo tu, kwenye Wizara hii ambayo naenda kuchangia muda si mrefu tumepelekewa shilingi milioni 280 kwa ajili ya ukarabati wa Shule za Narumu, mabaara lakini na ujenzi wa nyumba za walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijielekeze kwenye kuchangia hoja iliyopo mezani. Nianze kwa kuunga mkono hoja kwa sababu nina imani kabisa na Mheshimiwa Waziri dada yangu Ummy pamoja na wasaidizi wake wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi si mahiri sana wa kusifia lakini ninazo sababu za kumsifia Mheshimiwa Waziri huyu kwa kazi nzuri anayoifanya. Majuzi wakati wa Pasaka nilitembelea Kituo cha Afya pale Kisiki, aliona kwenye taarifa ya habari yeye mwenyewe akanitafuta na akaniambia kituo hiki tunaenda kukitengeneza kiwe cha kisasa ndiyo maana namsifia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwa Naibu Waziri Silinde majuzi tukiwa humu Bungeni alitoka akaenda kufanya ziara kule Hai. Ndiyo maana nasema hakika tuna timu nzuri ambayo inatusaidia hapo TAMISEMI. Mheshimiwa Naibu Waziri Dkt. Festo naye leo asubuhi ameniambia tukimaliza Bunge hili tunaenda naye Hai. Kwa hiyo, ninayo sababu ya kupongeza timu hii nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa elimu, pamoja na mazuri hayo machache ambayo tumefanyiwa kwa kipindi cha miaka 15 tuliyakosa sasa tumeyaanza kuyapata, naomba niseme kwenye elimu bado tunashida. Shule zetu za msingi pale Jimbo la Hai zimejengwa kuanzia mwaka 1950 na kurudi nyuma na sasa hivi zimechakaa sana, tuna shule 106 ni chakavu mno.

Mheshimiwa Naibu Spika, Pasaka nilitembelea Shule ya Mafeto ukienda pale Mheshimiwa Waziri ni aibu na wewe nilikutumia clip ile uone shule ile imechakaa kabisa si rafiki. Shule zote hizi 106 zimechakaa kweli kweli. Niombe Serikali ielekeze nguvu hapo ili pamoja na nguvu za wananchi na mimi mwenyewe tunazozitumia kwa ajili ya kuboresha miundombinu hii lakini Serikali itusaidie kupeleka fedha pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni pamoja na shule za sekondari. Tunayo Shule yetu ya Lemila pale na yenyewe imechakaa. Shule hii kimkakati kwa sababu inazungukwa na Kata nne tunaomba sana Serikali itutazame tuwe na shule ya kidato cha tano na kidato cha sita kwa sababu shule ile mazingira ni rafiki lakini tunalo eneo la kutosha; tuna hekta ishirini kwa ajili ya ujenzi wa kidato cha sita pale. Naomba pia nikumbushe pamoja na shule hizo nilizozitaja tuna Shule ya Uduru imechakaa san ana Shule ya Mkwasangile imechakaa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tuna eneo lingine ambalo niombe Serikali ilitazame sana. Pale Jimbo la Hai tulikuwa na shule tano, hizi shule tano zinaitwa shule za msingi za ufundi. Shule hizi zilikuwa zimejengwa mahsusi kwa ajili ya kuandaa vijana wetu kupata ufundi wa aina mbalimbali. Shule ya pale Mshara inaitwa Shule ya Msingi ya Ufundi Mshara, mle ndani kuna vifaa kwa ajili ya kufundisha watoto wetu kushona cherehani, kufuma lakini pia mafundi seremala. Ile shule imesimama, vifaa vipo mle ndani, watoto walianza kusoma lakini tangu mwaka 2019 walisitishiwa kufanya mitihani, hili linahusisha Wizara ya Elimu lakini pia TAMISEMI. Shule ya Mshara, Mkwasangira, Sare, Mroma lakini pia tuna shule moja ilijengwa kwa kusudio hilo na mradi wa TASAF na yenyewe imelala naomba ziangaliwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, shule hizi zitatusaidia kuwaibua vijana wetu kwenye eneo la ufundi lakini wakati huo huo Wizara ya Elimu ijiandae kufungua shule hizo ili watoto hawa waweze kufanya mitihani ya ufundi lakini pia waweze kupewa vyeti. Hii itaendana sambamba na fedha nyingi ambazo Serikali imepeleka kufufua Kiwanda cha Machine Tools, tutapata watoto wa kwenda kufanya kazi kwenye kiwanda hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nililotaka kuchangia, nafahamu tumetengewa fedha kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya pale Lundugai. Niombe sana Wilaya ya Hai tunayo changamoto kubwa, tuna mahitaji ya vituo vya afya 12. Bahati nzuri tumeshatenga maeneo, haya maeneo naihakikishia Serikali yapo, hayana mgogoro na sisi tupo tayari kuchangia pale ambapo itakuwa tayari na wao kutuletea fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa niombe sana pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri ameshanikubalia hiki Kituo cha Kisiki hatuna gari la wagonjwa, watumishi hawatoshi lakini pia hatuna jengo la mama na mtoto. Hii ni sambamba na Hospitali yetu ya Wilaya na yenyewe gari la wagonjwa hakuna, hakuna Jengo la Maabara wala Jengo la Mama na Mtoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze kidogo kuhusu TARURA, wenzangu wamesema sana lakini kwa Jimbo la Hai kwa kweli mtutazame kwa jicho la huruma. Pale tuna mtandao wa kilometa 600 na mita 200 lakini bajeti ambayo tumewekewa makadirio ni shilingi bilioni 1.7 haiwezi kutusaidia. Wenzangu wameshashauri namna ya kufanya, niombe kwa mahsusi wake mtusaidie. Tuna barabara inayotesa wananchi kutoka pale Kwa Sadala - Uswaa, Kivuko cha Mkalama – Kikavu Chini lakini Boma Ng’ombe - TPC na barabara zingine ambazo nimekwisha kuzisema.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine kwa haraka haraka, niombe sana Serikali tuna soko la kimkakati pale Kwa Sadala. Soko hili sipumui, simu yangu inajaa picha kwa sababu ya soko hili. Kila siku wananchi wanapiga picha wananiambia limechakaa halifai lakini tunalo eneo ambalo tumeshatenga kwa ajili ya soko hili. Ikumbukwe Wilaya hii kwa asilimia 78 tunategemea kilimo, wananchi wako tayari kulima soko lile liwe la kimataifa ili tuweze kukaribisha wawekezaji waje wanunue lakini pamoja na kuwa na viwanda vidogo vidogo vya kuongeza thamani.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumejenga Kituo cha Afya Longoi na Naibu Waziri amekitembelea. Sasa tunaomba vifaa tiba na watumishi ili tuweze kufungua kituo kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nizungumze jambo ambalo wenzangu wamesema pia. Haya yote tunayoyapanga na hizi bajeti tunazozipitisha wanaoenda kusimamia ni watumishi wa umma. Naomba sana Serikali ione haja ya kuongeza mishahara ya watumishi. Pia watumishi wale ambao wamepandishwa vyeo na wana barua zao mishahara yao irekebishwe. Changamoto kubwa tunayoiona hapa wakati mwingine tunalaumu sana Maafisa Utumishi lakini tujue sisi Wabunge hapa ndiyo tunaopitisha bajeti. Pale Wizarani naomba TAMISEMI mtashirikiana na Utumishi kuona namna ya kuongeza ma-approver wengi ili kazi inapofanyika huku kwenye level ya Halmashauri watumishi hawa mishahara yao iweze kuruhusiwa mapema na kuondoa kuwa na malimbikizo mengi ya mishahara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nisisitize barabara moja muhimu sana. Tuna barabara ya kutoka pale Mferejini – Narumu - Makoa ni kilometa 13 tu. Hii barabara inatupasua kichwa. Barabara hii iliitwa ya ng’ombe nimekuwa nikiisema sana na ni ahadi ya Rais, niombe sana mnifungue kwa barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine kwa kuhitimisha, nimeona kwenye hotuba imeleeza kuwa na maeneo ya uwekezaji. Jimbo la Hai tunayo maeneo ya uwekezaji lakini changamoto yapo kwenye Vyama vya Ushirika 17. Jambo hili nimekuwa nikisema sana na hapa nasema mapema kabisa kwa Wizara ya Kilimo tutakapofika kwenye Wizara ya Kilimo ile shilingi nitaitazama mno namna ya kuifanya. Juzi hapa tumekuwa na Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro, Waziri wa Utalii na Maliasili tumetembelea kule amejionea mwenyewe namna ambavyo kuna mikataba ya hovyo kwenye ushirika.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele imegonga Mheshimiwa.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tena kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hotuba hii nzuri na kihistoria. Nianze kwa kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo ameanza vizuri; kwanza kuendeleza miradi mikubwa ile ambayo awamu iliyotangulia ilikuwa imeanza nayo. Nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza pia Mheshimiwa Waziri na Watendaji wote wa kwa bajeti nzuri waliyotuletea, iliyochukua mawazo ya Waheshimiwa Wabunge. Niliwahi kusimama hapa nikauliza, ni kwa asilimia ngapi michango ya Wabunge inachukuliwa kufanya matengenezo kwenye mipango ya Serikali? Sasa naomba nipongeze sana kwamba wamechukua kwa asilimia kubwa mawazo yetu. Kwa msingi huo, nianze kwa kuunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Siyo tu kwamba naunga mkono hoja, ni wa sababu nimeona kwenye bajeti hii Jimbo letu la Hai tumetengewa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sekta ya viwanda tumetengewa shilingi bilioni 1.6 kwa ajili ya kufufua kiwanda cha Machine Tools. Siyo hivyo tu, tumepelekewa fedha kwenye elimu na barabara. Wananchi wa Jimbo la Hai wameniambia niunge mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuunga mkono, narudia tena kumpongeza Mheshimiwa Rais. Niseme, akina mama popote mlipo Tanzania, huu ni wakati wenu wa kuiga mfano mzuri na kila mmoja ambaye anafanya shughuli yake afanye kwa ujasiri kwamba akina mama wanaweza. Siyo kwa sababu mimi ni kinara wa kutetea haki za akina mama na watoto, siyo hivyo tu ni kwa sababu ya kazi nzuri wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme jambo, kwa msingi huo huo tu, tunaye baba yetu ambaye ndiye anamshauri Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kufanya haya. Naye nampongeza sana. Kwa heshima hiyo, namwomba Waziri; sasa hivi tunajua kwenye mikopo ile ya Halmashauri asilimia zile 10, akina mama wanapata, walemavu wanapata na vijana. Kwa msingi huo huo kwa sababu kuna baba anayemshauri vizuri mama, hebu akina baba na wenyewe waingizwe kwenye kundi hilo wapate mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nishauri kuhusu bajeti hii. tumeambiwa hapa tunapanga kuongeza pato la Taifa mpaka kufikia kwenye asilimia sita na ushee. Mimi naona hii ni ndogo kwa sababu kama tutafuata maelekezo ya Mheshimiwa Rais kuwekeza kwenye kilimo, tunaweza kuvuka lengo hili. Hakuna namna yoyote tunaweza kuepuka kuinua uchumi wetu tukaacha kilimo nyuma, haiwezekani. Tunaambiwa asilimia 25 ya pato la Taifa linatokana na kilimo, lakini ukienda kuangalia ni wangapi wanashughulika na biashara hii? Utakuta ni eneo dogo sana. Naomba tuamue kwa dhati bajeti hii, fedha ambazo zimetengwa kwenye eneo la kilimo zije kwa asilimia 100 zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo zuri tumeliona hapa. Wananchi wa Hai wamekuwa wakinipigia simu, vipi kuhusu tozo iliyowekwa kwenye umwagiliaji? Ile asilimia tano? Niseme, naiunga mkono Serikali tozo hii iwepo kwa sababu imehamishwa kule kwenye ushirika, imeletwa kwenye umwagiliaji. Kazi yake ni nini? Ni kuhakikisha wanajenga miundombinu, lakini fedha hii asilimia tano itafanya matengenezo. Jambo ambalo sasa hivi Serikali inajenga ile mifereji na zile skimu, lakini fedha za matengenezo haipo. Kwa hiyo, hii tozo iliyowekwa hapa itaenda kufanya kazi hiyo. Naomba ibaki hivyo hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri nimezungumza vizuri na Naibu Waziri, Mheshimiwa Bashe akanihakikishia ile Mamlaka ya Umwagiliaji inaenda kuanzishwa, itafanya kazi hii. Kwa hiyo, naomba sana kwenye eneo la kilimo tuwekeze nguvu ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wetu wengi wapo huko kwenye majimbo yetu. Hawa tukiwawezesha kwa hatua ya kwanza; kwanza kufanya utafiti. Tuweke fedha nyingi kwenye utafiti, naona zimewekwa, zije kama zilivyo. Wakipewa fursa ya kufanya utafiti, tukahakikisha tunayo mbegu yetu, tuna watalaam wa kutosha kwenye kilimo, tuna maji ya kutosha, eneo linalobaki ni kuhakikisha tuna viwanda vya kuongeza thamani ya mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna namna tunaweza kuinua uchumi huu kama hatuongezi uzalishaji. Hili linawezekana. Mheshimiwa Mama Samia Suluhu leo akisimama akitamka kwamba jamani Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya, Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa mlioko huo, kila Mkuu wa Wilaya kwenye wilaya yake tunampa malengo ya kukusanya, kwamba kila msimu tunataka tani 300,000 za mahindi, hizi lazima zipatikane; za maharagwe kadhaa, baada ya kufanya utafiti, kila mmoja tunampa lengo lake. Watatuletea hizi tani. Wale ambao tunaona wanasuasua, basi zile kadi ambazo Mheshimiwa Waziri ulishauri, itumike moja. Wakipigwa wawili, watatu speed itaongezeka kuhakikisha wananchi wanafanya kazi ya kulima kuongeza uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kilimo hiki kitatusaidia mno. Pale Jimbo la Hai Mheshimiwa Waziri, mimi nakuhakikishia, nyie tuleteeni fedha. Fedha yenu itarudi. Tuleteeni fedha za kujenga skimu za kutosha zile tano za kimkakati, tuleteeni viwanda vya kuongeza thamani ya mazao sisi tulime, tuuze. Siyo tu kwa kuuza, kwa sababu pale Jimbo la Hai tumeweka mkakati, tuna soko hili naomba sana, sijaliona kwenye bajeti lakini uone namna ya kutafuta fedha popote lile soko la kwa Sadala lijengwe. Lile soko letu lina tofauti kidogo na masoko mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lile soko tume-design litauza yale mazao ya wananchi lakini kutakuwa na viwanda vidogo vidogo vya kuongeza thamani ya mazao haya. Kama ni nyanya, inaondoka pale ikiwa imepakiwa vizuri kwenda nje ya Nchi. Kwa hiyo, hapa tutatengeneza fedha. Lile soko ni la kwako kabisa, ni la kimkakati, ukilitumia vizuri litatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumze kuhusu kazi nzuri ambayo Serikali imefanya kwenye maslahi ya watumishi. Bajeti hii tunayoijadili hapa wanaokwenda kutekeleza ni watumishi. Nawashukuruni sana kwa kupokea mawazo yetu. Waheshimiwa Madiwani mmewajali, Maafisa Tarafa; na nakumbuka mimi ni Afisa Tarafa Mstaafu, kwa hiyo, nililisema kwenye Kamati na mmeliweka hapa. Endeleeni kuboresha maslahi ya watumishi kwa sababu hawa ndio ambao wanatufanyia kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine hapo kwa watumishi, kuna jambo ambalo halijakaa vizuri kuhusu promotion. Fedha zimeshatengwa hapa, mara nyingi sana humu ndani tunasimama tunasema shida ipo kwa Maafisa Utumishi. Naomba leo tuweke kumbukumbu sawa. Maafisa Utumishi wakimaliza kazi yao, kuna watu wanaitwa Approver wako pale Utumishi. Hawa lazima tutenge fedha za kutosha ili wawepo wa kutosha na speed ya kupandisha watu madaraja iongezeke na watumishi wetu waweze kufanya kazi kwa bidii na kwa speed ambayo inategemewa. Tukifanya hivyo, itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona mikakati ambayo mmeweka ya kuongeza mapato ni nzuri sana. Awamu iliyopita kwenye tathmini tumeweza kukusanya kwa asilimia 86 mpaka kufikia Aprili, lakini mikakati tuliyoweka hasa pale bandarini, mmefanya jambo zuri sana la kutumia mifumo kukusanya. Ninaomba kuweka tahadhari kubwa ya kuangalia, hii mifumo tuhakikishe inafanya kazi masaa 24. Kwa sababu kosa linalotupata hapa ni kwamba wakati ambapo mifumo hii inasimama, ndiyo wakati tunapopigwa. Kwa hiyo, kama tumeamua kutumia hii mifumo, basi tuhakikishe mifumo hii inakuwa kamili kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sito tu pale bandarini, huku kwenye mahospitali yetu kuna makusanyo kwa kutumia mfumo wa GoT-HOMIS, ndiyo hali ipo hivyo hivyo, pale mfumo unapo-shake, tunaposema tunataka kwenda paperless, hawajajiandaa. Umeme unazimika, ndiyo fursa inatumika kutupiga. Kwa hiyo, naomba sana watu mitandao na mifumo wahakikishe tunakuwa na mifumo ambayo imesimama vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongezee hapa jambo. Niliwahi kusema humu ndani, hivi kuna shida gani kama tukiamua kuwa na mipango yetu ambayo itapangwa kwa kipindi cha miaka 50 na miaka 100? Nimejaribu kufanya tafiti, nimezungumza na maprofesa wa uchumi wananiambia jambo hili linawezekana. Ifike mahali Mheshimiwa Waziri, alika Maprofesa, alika wataalam wa uchumi, alika nchi nyingine duniani ambazo zimeweza kuwa na mipango hii. Hii itatusaidia sana kuwa na mipango ambayo itatekelezwa kwa kipindi cha muda mrefu lakini kuondoa utashi wa Kiongozi kufanya yale anayoyapenda yeye. Hii mipango itatusaidia kusukuma. Tunakuwa na mambo haya, tunasema hizi ni interest za Tanzania, ziwekwe hapa, tutatekeleza kwa kipindi cha miaka 50. Aje mweusi, aje mweupe atatekeleza, atalazimika kwa misingi ya sheria kuweza kutekeleza hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. Hongereni sana kwa bajeti nzuri inayogusa maisha ya wananchi. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. SAASHISA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Pia kabla ya kusema chochote, nitoe pole sana kwako wewe, kwa Mama Samia Suluhu kwa kuondokewa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, familia ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli na Watanzania wote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ndiye aliyetuletea mwenyewe Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Hii kwangu naitafsiri kama ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu kuja kwa Watanzania. Leo nasimama hapa kushukuru na kurudisha sifa na utukufu kwa Mwenyezi Mungu kwa zawadi hii ambayo alitupa ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtoa hoja ameeleza mambo makubwa ambayo yamefanywa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, lakini Watanzania kwa hakika wanajua mambo haya makubwa yaliyofanywa na Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Ukiangalia kipindi cha maombolezo, ukianzia safari ya kuaga pale Dar es Salaam, hii ni dhahiri kwamba Watanzania wanajua haya mambo makubwa ambayo Hayati Dkt. Magufuli aliyafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawakujali ukubwa wa uzito wa uzio ulipo pale Uwanja wa Ndege. Wakatafsiri, ndege ni zetu wenyewe, Rais ni wetu wenyewe na sasa tunaingia wenyewe kwenye uwanja wetu. Waliingia kuonyesha mapenzi yao kwa Rais wao mpendwa wanayempenda. Vile vile kila mahali msafara ulipopita, wananchi walijitokeza kwa wingi. Hii ni ishara kubwa kwamba wananchi walimwelewa, walimpenda na hili ni zao la Watanzania kwa hakika. Naomba nishauri, haya mambo makubwa yaliyofanya tuyaweke kwenye kumbukumbu, niishauri Serikali ikiona inafaa itenge siku maalum iitwe Magufuli Day kwa ajili ya kumuenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, Serikali ione namna ya kufanya hapa Dodoma, jiji ambalo mwenzangu aliyepita ameshaeleza namna ambavyo alipambana kuhakikisha linakuwa Makao Makuu ya Nchi; kijengwe kituo maalum kwa ajili ya kutunza kumbukumbu zake. Hii itakuwa ni sehemu kubwa ya kuendelea kuenzi hayo mambo mazuri aliyoyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tayari alikuwa ameshaelekeza namna Wizara ya Elimu itakavyotengeneza mtaala wa kutengeneza historia yetu, basi kwenye mtaala wetu tuweke pamoja na viongozi wengine historia yake ili Watanzania waweze kuisoma vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme, tunalo jambo la kujivunia kwa haya mambo makubwa ambayo wenzangu wameeleza. Leo tunazungumza uwepo wa reli, treni ya umeme; haya ni mapinduzi makubwa ya kihistoria ambayo yamefanyika wakiwa pamoja na Mheshimiwa Mama Samia Suluhu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naenda moja kwa moja kwenye Azimio la pili. Haya mambo tunayoyataja leo, haya mambo tunayoyaona leo na kuyafurahia, barabara za chini na za juu zimejengwa, Vituo vya Afya vimejengwa, Mahakama wamejengewa ofisi nzuri. Kama wamejengewa Ofisi nzuri, watoto wanasoma kupitia Mfumo wa Elimu Bure, yamefanyika sambamba kwa kushirikiana na aliyekuwa Makamu wa Rais wakati huo ambaye leo ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sina mashaka hata kidogo kwamba miradi ile yote ambayo ilikuwa imepangwa itaendelea vizuri kabisa bila wasiwasi wowote. Tumeona katika kipindi cha muda mfupi, ndani ya siku tano, cha uongozi baada ya yeye kuapishwa kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amefanya mambo makubwa ndani ya siku hizo tano. Kule Bandarini tumeona kilichotokea, hii ni ishara kwamba kiatu kilipotoka kimeingia kiatu kingine chenye size ile ile kwa speed nyingine kubwa. Kwa hiyo, tunayo matazamio makubwa sana. Hili lililotokea leo, nadhani wale ambao wanafuatilia kwenye mitandao, hapa kuna watu wamepigwa chenga ya mwili. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walichokuwa wanadhani kwamba sasa tunafika mahali tunaenda kuyumba kama nchi, wamepigwa chenga ya mwili mzima. Leo tumeletewa tena Mtumishi mwingine wa Mungu, mtu ambaye ni mzalendo, amechukua nafasi ya Makamu wa Rais. Nasi hapa bila tashwishi tumempitisha kwa asilimia mia. Nawapongeza sana ndugu zangu upande ule kule kwa namna ambavyo tumeungana kwenye jambo hili. Huu ndiyo msingi wa kuanzia leo, tuendelee kuungana kwenye mambo ambayo ni ya Kitaifa ili hata wale wengine walioko huko, ambao wamebaki na kazi ya kujifungia ndani, kazi yao ni WhatsApp, Twitter, kukashifu, kutukana nchi yetu, wajifunze kuanzia leo kwamba sisi ni Watanzania, tunaenda kusimama kuhakikisha Rais wetu anaenda kutekeleza yale yaliyopo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na vile vile yale yote ambayo waliandika katika hotuba.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutakumbuka hapa, Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli alituletea hotuba hapa Bungeni inayoonyesha mwelekeo wa Serikali. Hotuba ile kwa hakika waliandaa pamoja na Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu. Kwa hiyo, haya yote yanaenda kutekelezwa kwa speed ile ile. Kwa hiyo, niwatumie salamu pia wale waliodhani kwamba tunaenda kukwama, Mungu ameshusha tena baraka nyingine na leo tumeshuhudia hapa namna ambavyo tunaenda kukimbia kwa speed. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono na nawaomba sana Watanzania, tumwombee sana Mheshimiwa Rais wetu ili ayafanye yale ambayo ni matarajio yetu. Nasi kama Wabunge tusimame imara kuisaidia Serikali na kumshauri ili yale matarajio ya Watanzania yapate kutokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na naunga mkono hoja zote. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu ambaye ametupa afya na uzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, ambaye kwa hakika anafanya kazi kubwa sana ndani ya nchi yetu. Mheshimiwa Rais wetu anakidhi matarajio ya Watanzania, Watanzania ambao wana matarajio makubwa sana, lakini wanatuombea sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru wale waliotengeneza Wimbo wa Taifa, kila siku asubuhi watoto wetu wakijipanga mstari pale wanasema wabariki viongozi wote, maana yake na sisi tunaombewa. Sasa utaratibu wa kubarikiwa maana yake na wewe ufanye mambo mema, usipofanya mambo mema maana yake ni kinyume chake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mheshimiwa Rais anafanya mambo mema kwa hakika na wale ambao ni wasomaji wa Biblia ukienda kwenye Mathayo 25 kuanzia mstari ule wa 40 utaona kuna jamaa pale waliambiwa: “…nilikuja kwako nikiwa na kiu hukunipa maji, nilikuja kwako nikiwa na njaa hukunipa chakula…”

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mama Samia kwa kweli haya yote sisi watu wa Hai tunasema anastahili baraka maana kama ni maji ametuletea mradi wa bilioni 3.5, lakini kama kwenye upande wa chakula ametupa, tumepata fedha za skimu, tumepata fedha za maji. Kwa kweli, anafanya kazi kubwa sana, nimpongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze Makamu wa Rais na Waziri Mkuu. Hapa kwa Waziri Mkuu niseme jambo; nilikuwa nahangaika sana masuala ya ushirika hapa, lakini kupitia yeye na Wizara ya Kilimo na Naibu Waziri leo nasema Ushirika wa Hai umeanza kufufuka. Ile mikataba ya hovyo iliyokuwepo tulienda na Naibu Waziri tukazungumza, mengine tukayavunja tukaweka utaratibu mzuri kwa vile vyama 20 ambavyo tumeanza navyo bado vingine 20. Sasa haya ni mafanikio mazuri ya kazi nzuri anayofanya Mheshimiwa Rais wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajielekeza kwenye mchango wa leo, naomba nitumie nafasi hii pia kuwashukuru watumishi wote wa Serikali wanaomsaidia Mheshimiwa Rais kuanzia ngazi ya juu mpaka ya chini. Hawa watu wakati mwingine tunawasahau, wanatusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upekee, watumishi wa afya ambao wametuvusha kwenye kipindi kigumu sana cha corona. Wametuhudumia vizuri, hawakuogopa, hawakurudi nyuma, naomba niwapongeze leo na ikae kwenye kumbukumbu kwamba, tunawashukuru sana kwa kazi nzuri waliyoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mchango wangu niipongeza pia, Kamati yetu. Kamati hii imefanya kazi kubwa sana na kama Mheshimiwa Waziri atachukua maoni haya tunaenda kutoboa, tunaenda kuinua kilimo chetu na tunaenda kubadilisha nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niboreshe eneo moja tu na niwaombe kama wanaweza kwenda kufanya review ili iingie kwenye kumbukumbu, fedha zile walizosema ziongezwe milioni 450 hazitoshi. Kama kweli tunataka kubadilisha uchumi wa nchi hii kwa sababu, formular ya uchumi ni rahisi sana, hapa ili uchumi ukue tunatakiwa kuongeza uzalishaji, productivity. Sasa tunaongeza uzalishaji wapi, lazima twende kwenye kilimo, hatuna ujanja mwingine. Sasa hii milioni 400 waliyopendekeza, nasema iende kwenye trilioni moja, ikishindikana bilioni 800. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe na bahati nzuri leo umekuwa ukiweka chumvi vizuri sana kwenye michango yetu. Naomba na hili tuisimamie, isipungue bilioni 800 ili kweli haya yote tunayoongea yaweze kutekelezeka fedha hii iongezwe. Kwa hiyo, niombe ile Kamati itafute namna nzuri ya kusahihisha au wewe Mwenyekiti wetu utuongoze fedha hiyo iongezwe ili ikafanye kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi zenyewe tunazozisema, kama tunataka kilimo, lazima hatua ya kwanza tuupime udongo wetu. Kwa sababu, wananchi wanalima, lakini wanalima kienyeji wanapata shida; tujue kuna calcium kiasi gani, kuna potassium, sijui vitu gani, udongo wetu tupime. Tukitoka hapo tuwe na maji ya hakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru Mama Samia Suluhu ametuambia tunaletewa magari yale. Magari haya yawekwe kwenye mfumo mzuri, tuna skimu za kutosha ambazo zikijengwa tunaweza kupata maji, kwa hiyo, fedha hizi tunazoziomba zielekezwe kwenye maji. Tukitoka hapo tuhamie kwenye hatua nyingine ya kuwa na mbegu sahihi, za kwetu. Hawa Maprofesa wanaosemwa ni kweli wamejaa pale Wizara ya Kilimo wa kutosha na wameandika mavitabu kibao, ukienda pale kilimo utakuta lundo la mavitabu. Tunataka yale mavitabu yatoke Wizarani yaje huku tuyaone, watusaidie, wafanye utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ifike mahali suala la mbegu liwe ni suala la kiusalama wa nchi yetu. Kwa nini nasema hivyo? Ni kwa sababu mbegu hizi wanazonunua wananchi hatuna uhakika nazo. Sawa zinafanyiwa utafiti, ile movement ya mbegu kwenda kumfikia mlaji wa mwisho hatuna ulinzi nazo. Mtu anaweza kutengeneza mbegu fake hapa, hebu fikiria mtu analima shamba eka 10, lakini anaenda kupanda mbegu fake, kwa nini mbegu fake? Sawa imefanyiwa utafiti, kule mlaji wa mwisho nani anayejua?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningetamani mbegu hizi zipite kwenye mkondo wa Kamati zetu za Usalama, zilinde mbegu yetu ifike kule kwa mlaji ikiwa ile mbegu iliyokusudiwa. Ukishakuwa na mbegu sahihi tunaendelea maeneo mengine ya kuongeza ubora wa mazao yetu. Nilitembelea nchi jirani hizi za kwetu hapa, nikakuta mazao yetu, hizi mbogamboga zinakwenda nchi Jirani, zinaongezewa thamani ya mazao na wanauza kwa fedha nyingi, sisi kwetu tunauza kabla ya kuongeza thamani ya mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana sisi pale Hai tume-design soko letu tofauti kidogo. Kwenye soko letu tukasema hapana, sisi tunataka kuwe na viwanda vidogo kama mtu analeta bidhaa yake sokoni, akinunua kwa bei ya jumla kuwe na viwanda vya kufanya sorting, kuwe na viwanda vya kufungasha, ili bidhaa ikitoka hapa iende sokoni kwenye soko la kimataifa ikiwa imekamilika, maana yake imefungashwa vizuri. Ndio maana tunaiomba sana Serikali itusaidie fedha za kusaidia soko la Kwa Sadala ambalo litakuwa ni soko la mfano. Sisi hatujaweka sijui maeneo ya saluni, sijui maeneo ya ukumbi, tumesema hapana tunataka soko letu limsaidie mkulima na huu ndio uwekezaji mzuri ambao nauzungumza hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamezungumza kuhusu habari ya mbolea. Hili ifike mahali tuamue, tulisimamie kabisa kama ni kutafuta wawekezaji, kama ni Serikali kuingilia ndani. Hizi fedha ninazoziomba bilioni 800 au trilioni moja zifanye kazi ya kuwa na kiwanda hiki. Wameshafanya study ukiwauliza watakwambia, ukienda vizuri unauliza enhee, hivi kwani kutengeneza kiwanda cha mbolea ni shilingi ngapi? Wanazo analysis vizuri, wameandika kwenye vitabu, lakini sasa nani afanye?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ifike mahali tukishindwa kupata mwekezaji Serikali ifanye kwa maslahi mapana ya kuinua uchumi wetu. Hii asilimia tunayoambiwa asilimia 65 kwamba, hawa ndio wamepata ajira. Kama asilimia 65 ndio wamepata ajira, pengo linatokea wapi kwenye pato la Taifa tunabaki na asilimia 26? Maana yake kuna watu wanatoroka hapa. Wanatoroka kwa nini, hatuwawezeshi. Tuwawezeshe warudi ili uwiano uliopo kwenye ajira uwe ndio uwiano ulioko kwenye pato la Taifa, hapo tutakuwa tumeinua uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze hapa wakati wa bajeti iliyopita, wakati tunajadili Mpango uliopita tuliambiwa kutakuwa na Bodi ya Uwagiliaji. Niombe Waziri atakaporudi hapa atuambie mchakato wa kuanzisha hii Bodi ya Umwagiliaji ambayo naamini itaenda kuhakikisha wakulima wetu wana vyanzo vya kutosha vya maji, Bodi hii itaanza lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, wenzangu wamechangia sana kwenye kilimo, niombe ifike mahali utuongoze, umesema Bunge hili linaenda kuwa la kuimarisha kilimo, kweli tukafikie hapo na tusimame imara kabisa kwa sababu huu ndio ufunguo wa kuinua uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihame kidogo niombe.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda hauko upande wako. (Kicheko)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye taarifa hizi za Kamati ambazo zimewasilishwa mbele ya Bunge lako Tukufu. Kabla sijachangia, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya katika nchi yetu. Sisi wananchi wa Jimbo la Hai kwa kweli tuna msemo wetu, ‘Mama ametuletea miradi kedekede na tunamshukuru sana’. Kila eneo limeguswa na tuna miradi mingi inatekelezwa ndani ya Jimbo la Hai, jambo ambao halijawahi kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niwapongeze wasaidizi wake wote, nikianza na Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mawaziri wote na Wakuu wa Mikoa wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Wakuu wa Wilaya wakiongozwa na Mkuu wa Wilaya ya Hai, Wakurugezi na Watendaji wote, Wenyeviti wa Halmsahauri na Madiwani mpaka Mwenyekiti wa Kitongoji, kwa kweli wote tunashirikiana kuijenga nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na mambo makubwa anayoyafanya Mheshimiwa Rais, nimesoma taarifa hizi, lakini natokea Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, hiki kinachoendelea kuhusu Matumizi ya Fedha za Serikali, kimenistua, na kikanifanya nijiulize sana. Dhamira ya hawa wasaidizi wa Mheshimiwa Rais ni ipi, ikiwa Mheshimiwa Rais anahangaika huko kutafuta fedha, anazileta hapa hiki kinachoendelea huku ni kitu gani, leo tumeona namna amehangaika ameleta hela za UVIKO. Watu wameenda kujificha, yale mapato ya ndani ambayo yalipaswa kutekeleza miradi hayafanyi kazi iliyokusudiwa, maana yake wanajifika kwenye UVIKO na vitu vinavyofanana na hivyo.

Mheshimiwa Spika, ukisoma taarifa hii ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa, ukurasa wa sita, utaona mambo yalivyo magumu sasa hivi. Kwanza wamesema ununuzi wa bidhaa za thamani ya shilingi bilioni 7.9 ulifanyika bila idhini ya Bodi, kwamba taasisi zinajiendesha zinavyotaka, mamlaka imeteua Mwenyekiti wa Bodi pale ambaye ni Mteule wa Rais, lakini wao wanaenda kufanya matumizi bila kushirikisha bodi. Hii ni hatari kama tutaiacha.

Mheshimwa Spika, wameenda mbali zaidi, hapa kuna bilioni 3.84, hizi ni ununuzi wa bidhaa ambazo zimenunuliwa bila kuwa kwenye mpango. Hapa halmashauri 24 zimehusika. Ukisogea tena kuna bilioni 5.34 katika halmashauri 39, wamefanya manunuzi bila ushindanishi wa bei. Hizi zote ninazotaja ni fedha, lakini ukienda kuna bilioni 1.2 zimetumika bila kuwa na hati ya kuagiza vifaa (LPO) kwenye halmashauri 14. Wamesogea mbali, ununuzi wa thamani ya bilioni mbili bila kushindanisha wazabuni.

Mheshimiwa Spika, hii ni hatari kama tutaacha jambo hili. Niliombe sasa Bunge lako Tukufu, kwa kweli tuone namna ya kuchukua hatua, kama hatutachukua hatua hii ni hatari, tutakuwa hatumsaidii Mheshimiwa Rais. Hawa wote ambao wamehusika wawajibishwe kwa mujibu wa sheria, ili iwe fundisho. Naomba kabisa Bunge lako hili Tukufu, safari hii tusiache kuchukua hatua kwa hawa watu. Tutoe maelekezo thabiti ya kuhakikisha Serikali inafanya kazi yake ya kuwawajibisha hawa ambao wamehusika na vitu hivyo.

Mheshimiwa Spika, pia, mambo yanayofanana na hayo hayo yapo ukurasa wa 11 kuhusu asilimia 10 ambayo inatengwa kutokana na mapato ya halmashauri. Kimsingi fedha hizi kanuni zinaeleza wazi, sheria inatamka wazi kwamba ukishakusanya mapato yasiyolindwa, asilimia kumi nenda kakopeshe kwa akina mama, vijana na watu wenye ulemavu. Kanuni inasema kakopeshe 4:4:2 ambaye hatumii formular hii, huyu ana jambo baya na sisi, hamtakii Mheshimiwa Rais mema. Sisi kwenye Kamati yetu ya USEMI, tumesema sana na hizi halmashauri, lakini hawatekelezi kwa sababu wana jambo lao na jambo lao ni hili, halmashauri 154 zimeshindwa kukusanya bilioni 47.01 ambazo zilipaswa kurejeshwa kwenye vikundi.

Mheshimiwa Spika, fedha hizi ni nyingi, sisi tumepiga hesabu kwenye Kamati yetu tumebaini karibu bilioni 65 kila mwaka zinatengwa kwenda kukopeshwa. Hizi fedha ni mtaji wa kuanzisha benki kabisa, lakini fedha hizi haziendi kama ambavyo kanuni inataka na hazikopeshwi kwa kuzingatia utaratibu. Sasa naomba, kwa sababu Kamati yako ya USEMI tumekuwa wabobezi sana kwenye eneo hili. Tupe fursa twende ndani tupate muda wa kutosha, tukuletee taarifa sahihi kwenye asilimia hii 10 tu; kwa sababu hizi ni fedha nyingi ambazo kusudio la Serikali ni fedha hizi zikasaidie kule chini: pamoja na kwamba tumeshashauri hapa, sheria hiyo iletwe, ifanyiwe marekebisho ili kundi la wanaume nao wanufaike. Sasa kama kundi hili linapokwenda kunufaika kama hatuna mechanism ya kusimamia na tunaletewa na CAG taarifa hii, hii sio sawa, hatumsaidii Mheshimiwa Rais kwa namna hii.

Mheshimiwa Spika, wameenda mbali, wamesema bilioni 1.2 zimetolewa kwenye akaunti ya Amana bila kuzingatia utaratibu. Wamesogea mbele zaidi wamesema, halmashauri 17 zimetoa mikopo, bilioni 3.26 bila uwiano unaotakiwa kwa maana ya 4:4:2. Wanafanya hivi sio kwa bahati mbaya, siyo kweli. Kuna taarifa tulikuwa tunaletewa unaambiwa halmashauri nzima hakuna walemavu, siyo kweli, halmashauri nzima hakuna watu wenye sifa, siyo kweli. Nia ikiwa njema kukiwa na utayari wa kumsaidia Mheshimiwa Rais, hivi vitu vipo na wenye mahitaji ni wengi mno, hatuwezi kusema kwamba kuna fedha zinaweza kurudi kwamba hazikutumika.

Mheshimiwa Spika, sasa nishauri kwenye eneo hili, nafahamu Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMi amekuja vizuri na ameanza vizuri na wamezindua mfumo ambao utatusaidia kwenda ku-control, wameshauzindua mfumo wa kieletroniki ambao utajumuisha Tanzania nzima. Wale waombaji wataingia kwa NIDA zao, maombi yao na vikundi, kwa kweli umeonyesha vizuri. Hata hivyo, bado nasema kwa kuwa fedha hizi ni nyingi na hao wanaoandaa mfumo huu tuliwashauri kwenye Kamati washirikiane na e-government, ili ku-control, namna ya kudhibiti. Bado tunahitaji kutafuta proper mechanism, bilioni 65 sio ndogo, lakini lazima tutafute mechanism ya hizi fedha ambazo zimeachwa hazijakusanywa ziweze kurejea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nirejee kukuomba tena Kamati ya USEMI na LAAC ziungane pamoja ziende kwenye mambo haya ya msingi, zikatazame hizi asilimia kumi, zikatazame kuna kitu kinaitwa bakaa kwenye taarifa za halmashauri. Wanafanya mambo yao, mwishoni unakuta bakaa milioni 35, halmashauri ndogo kabisa, halafu hizi zinaenda kutumika, wakati mwingine hata Waheshimiwa Madiwani hawashiriki. Ndio maana Bunge lililopitwa Madiwani hawa tuwatazame, tuwape nguvu, tuwawezeshe ili waweze kuzisimamia vizuri halmashauri zetu. Bila kufanya hivyo hivi vitu vinapita, unakuta bakaa milioni 60, hii inaitwa bakaa, Madiwani walishamaliza kazi yao, hao wanaenda kupanga mapato na matumizi kadiri wanavyotaka.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli naomba nihamie kwenye eneo lingine ambalo lilizungumza hapo jana kuhusiana na eneo la uwekezaji, tumepitisha mabadiliko ya sheria, lakini bado kuna changamoto. Kwa halmashauri zenye mapato machache ambayo ni wanufaika na mpango wa uwekezaji. Wale wawekezaji kupitia mfumo wa EPZ, wanakuja kwenye halmashauri zetu, wanalipa centrally kwa Serikali Kuu, zile halmashauri kule chini hazinufaiki. Kwa mfano, Jimbo la Hai, asilimia 78 sisi tunategemea kilimo na ufugaji, anakuja mwekezaji kupitia mashamba ya ushirika, anachukua anaweka mashamba ya kupanda maua kama mwekezaji kupita mfumo wa EPZ, pale Halmashauri ya Hai hachangii chochote.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, unakuta maeneo yetu, ukienda kule kuna wawekezaji wengi wana mashamba huku na huku, lakini halmashauri haipati kitu. Naomba turejee, watakapoenda kuandika kanuni, waseme kwamba na sisi halmashauri zilIzopo kule, hawa watu wawajibike kwetu. Hata zile bodi zilizoundwa pale zimeweka level ya Kitaifa kwenye level ya ngazi ya halmashauri hakuna kitu. Hakuna mwakilishi wetu, sasa sisi ambao tunapokea ile miradi mtu anaweka shamba la maua pale, sisi ndiyo tunampa maji, sisi ndiyo tunamsaidia kila kitu lakini halipi kodi. Niombe sana hili litazamwe kwa jicho la huruma, kwa sababu halmashauri nyingi ambazo zinahusika na maeneo ya uwekezaji zinaenda kuwa maskini.

Mheshimiwa Spika, naomba niende moja kwa moja nizungumze jambo ambalo lilizungumzwa jana hapa kuhusiana na KADCO. Uwanja wa Ndege wa Kilimanjaro ni mali ya Serikali, mwanzoni kulikuwa na wabia mbalimbali pamoja na KADCO, lakini Serikali ilinunua hisa zile na kwa mkopo wa CRDB na ikalipa. Kwa hiyo, picha iliyopo ili tusichanganye wananchi wa Jimbo la Hai ambao kule kuna suala linaendelea chini ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, wakadhani uwanja wa ndege sio mali ya Serikali, naomba tuweke sawa hapa. Ule uwanja ni mali ya Serikali, eneo lile ni mali ya Serikali, mradi unaoendelea pale ni mali ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, sasa kama kuna changamoto ya yule anayeendesha pale kwa maana ya msimamizi na anaye-run ile activity, KADCO, tuone namna ya kuutunza vizuri ili tusiwachanganye wananchi wakaona kwamba ule uwanja sio mali ya Serikali. Ni vizuri hilo likawekwa sawa, uwanja ule ni mali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na kama nakosea utanielekeza namna gani ya kufanya, lakini taarifa sahihi ni hizo ili tusiwachanganye wananchi kwa sababu kuna suala la fidia linaendela.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba nisisitize tu, hiki kitu kinachoitwa bakaa, Waziri atakapokuja kusimama hapa, atutolee mwongozo kwamba, huu utaratibu wa kubakisha hela kwa makusudi fulani, maana yake ni nini na atoe maagizo sahihi kwenye jamobo hili.

Mheshimiwa Spika, lingine, kumekuwa na ubadilishwaji wa matumizi wa fedha za Serikali kwenye hizi halmashauri zetu, wanakuja hapa, wanaleta bajeti, tunaipitisha hapa, nendeni mkajenge madarasa kadhaa. Tunawapitishia kwa asilimia 100, wanaenda wanakusanya. Hili tena niseme hapa, upo ujanja sasa hivi, kila halmashauri utaambiwa imekusanya zaidi ya asilimia 100. Ukija kwenye utekelezaji wa miradi hawatekelezi, hawapeleki fedha na hizi asilimia 100 zinawekwa kimkakati, halmashauri ina uwezo wa kukusanya bilioni tatu, watakuambia tunakusanya bilioni mbili ili wafikie malengo haraka na wasifiwe, lakini hata wale walioshindwa hawapeleki fedha.

Mheshimiwa Spika, TAMISEMI iende ku-review mifumo ya kupeleka makadirio ya makusanyo kwenye halmashauri zetu. Kuwe na vipimo ambavyo ni bayana vya kupeleka haya, vinginevyo tutaumiza halmashauri nyingine ambazo zinafanya kazi na hili la bakaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho kubadilisha miradi pasipo kufuata utaratibu, wanafanya reallocations ya funds. Kwa mfano, sasa hivi tulikuwa tunaangalia fedha zilizokuwa zimepelekwa za UVIKO na fedha nyingine ambazo zimepelekwa kwa ajili ya kujenga zile shule za kidato cha tano na sita. TAMISEMI imepeleka fedha, kila halmashauri inasema hazitoshi, kwanza kabla hawajenga na ukiwauliza hebu tuambieni, ukiwauliza TAMISEMI hii BOQ mliopeleleka huku ndugu zetu mlikuwa mnakadiria ifanye kitu gani na sasa mnasema fedha hazitoshi, tuleteeni basi BOQ ya kusema hapa sisi tunaongeza bilioni mbili au milioni 200. Kwa mfano, Halmashauri ya Bahi, wao wamesema milioni 58, wengine 150, wengine 200, fact za ki-engineer zipo wapi na ukienda kuangalia hizo unakuta ramani inasema jambo lingine, yaani ramani inasema ina milango nane, ukienda kwenye BOQ kumi na mbili.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nasema, pamoja na kwamba tulishauri kwenye Kamati nasema hapa ili Mheshimiwa Waziri akaweke mikasi mikubwa ya kuwabana hawa watu, wafanye kazi kwenye uhalisia, warudi kwenye neno lao, wanasema ni wataalam wafanye kazi kitaalam ili tuweze kumsaidia Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kwa kuhitimisha, niombe, sote tunaijenga nchi yetu, kila mmoja aliyepo hapa, tusiposhirikiana na kupenda nchi hii na kumsaidia Mheshimiwa Rais kwa dhati, hakuna mtu mwingine atatoka nje ya Tanzania kuja kufanya kazi hii, huu wajibu ni wakwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuunga hoja zote mkono na mchango wangu ndiyo huu. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na ninashukuru sasa umetaja vizuri jina langu ni jepesi tu Saashisha Elinikyo Mafuwe.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ndiyo nimepata nafasi ya kuchangia na kupata fursa ya kuweza kusema neno la shukrani kwa ajili ya wananchi wa Hai walionipa heshima kubwa sana ya kunichagua kuwa Mbunge wa Hai. Pia wametupa heshima kubwa sana kumchagua Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu kwa kura nyingi za kutosha 92%, lakini wametuchagulia madiwani wa kutosha sana. Nawashukuru sana wananchi wa Hai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kuunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyotoa kwenye Bunge lako Tukufu. Hotuba hii ya Mheshimiwa Rais inatoa mwanga na mwelekeo wa Serikali kwa kipindi cha miaka mitano. Ukisoma kitabu hiki kinajibu matarajio ya wananchi wa Jimbo la Hai na wananchi wa Tanzania. Hii ni ishara kwamba Mheshimiwa Rais ni zawadi ya Watanzania, mambo anayoyafanya kwa nchi yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mambo ambayo katika historia ya nchi hii hayatasahaulika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayo sababu ya kumshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyetuletea zawadi ya Dkt. John Pombe Magufuli. Miradi mikubwa inayotekelezwa na Ilani ya Chama cha Mapinduzi iliyopita na hii ambayo tunaandaliwa tena ya miaka mingine mitano inaonyesha kwa kweli Mwenyezi Mungu ametupa zawadi ya Rais mwema. Nichukue nafasi hii kuendelea kumwombea Mungu ampe afya njema ili haya yote yaliyoandikwa na yaliyosomwa kwenye hotuba yake yaweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ya jambo ambalo limenigusa sana ni habari ya kilimo. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais amesema sasa tutaenda kupandisha thamani ya mazao kwenye kilimo ambacho tunafanya. Kwetu kule Hai 78% tunategemea shughuli za kilimo. Nashukuru sana hotuba hii miongoni mwa mazao ya kimkakati yaliyotajwa, zao la kahawa limetajwa kama zao la taifa la mkakati.

Mheshimiwa Spika, sasa niseme kidogo, kule kwetu Hai zao la kahawa limepunguza tija kidogo kwa sababu ya utitiri wa vyama vingi vilivyopo kabla ya zao hili kufika sokoni. Pia zao hili limepunguza uzalishaji kwa sababu ya kukosekana kwa maji ya kumwagilia.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kuunga mkono hoja hii na kuiomba Serikali ihakikishe tunapata maji ya kumwagilia ili tuweze kufufua zao hili la kahawa. Ikumbukwe kwamba mbegu za kahawa au chanzo na utafiti wa kahawa unafanyika ndani ya Jimbo la Hai. Taasisi ya Uchunguzi wa Zao la Kahawa (TaCRI) iko ndani ya Jimbo la Hai. Nashangaa utaona maeneo mengine zao hili linapandwa lakini pale Hai limefifia. Niombe sana Serikali yangu sikivu, tumeomba na nimepeleka ombi maalum la kupatiwa mito ya umwagiliaji mitano inayopatikana ndani ya Jimbo la Hai. Tukipata mifereji hii mitano itatusaidia sana kufufua zao hili la kahawa.

Mheshimiwa Spika, lakini siyo hilo tu, Jimbo la Hai Mungu ametujalia tunavyo vyanzo vikubwa sana vya maji lakini tatizo ni namna ya kuvifikisha kwa wananchi. Tunayo ardhi nzuri ya kilimo lakini tatizo ni namna gani tuitumie.

Mheshimiwa Spika, nilianza kwa kuomba wenzetu wa TARI Mlingano wafanye utafiti wa udongo, kazi ambayo imekwisha kukamilika. Kwa hiyo, kazi iliyobaki ni kuiomba Serikali iweze kutuletea maji kwa ajili ya kumwagilia maeneo haya mazuri.

Mheshimiwa Spika, niseme kilimo cha mazao ya mbogamboga katika Jimbo la Hai ni biashara ambayo Serikali tukiwekeza tutakusanya kodi nyingi sana, tunaweza tukafanana na wanaochimba madini. Sasa hivi ukiangalia mazao mengi yanaenda nchi nyingine sisi Hai tunazalisha lakini wanapeleka nchi nyingine kwa ajili ya kwenda kuongezewa thamani na thamani yanayoongezewa ni kufanyiwa packing tu. Kwa hiyo, naiomba Serikali sasa kule Hai tumekubaliana kuwa na ari mpya ya kilimo na viwanda, tupatiwe msaada wa packing, baada ya wananchi kulima tuweze kuyaongezea thamani kwa kufanya packing. Bahati nzuri tunao uwanja wa ndege tutaweza kusafirisha nje ya nchi ambapo kuna mahitaji makubwa ya chakula cha ziada kinachozalishwa katika Jimbo la Hai.

Mheshimiwa Spika, hotuba hii imezungumza pia habari ya kuendelea kujenga miradi ya maji. Nashukuru sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, namshukuru Mheshimiwa Rais, Makamu wa Rais, Waziri Mkuu kwa kutuletea Naibu Waziri wa Maji pale Hai. Tulikuwa na tatizo kubwa sana la maji; moja katika Jimbo letu la Hai huduma ya maji inasimamiwa na Bodi za Maji kulikuwa na shida kubwa sana. Nashukuru Naibu Spika alifika pale dada yangu akafanya kazi kubwa na nzuri ya kurekebisha matatizo yaliyokuwepo kule. Kwenye bodi hizi kulikuwa na shida amezinyoosha vizuri mno.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nasimama hapa kushukuru kwamba tulikuwa na mradi wetu wa Kikafu ambao ulishathaminiwa siku nyingi wa shilingi bilioni 3.6. Nimepewa taarifa tayari Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli imetupelekea shilingi milioni 500 kwa ajili ya mradi huo, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kule Lundugai tumepata shilingi milioni 200, hii ndiyo raha ya kuchagua CCM. Nataka niwaambie wananchi wa Hai walifanya maamuzi sahihi kabisa ya kuchagua Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kule Romu tumepata shilingi milioni 200. Naomba sana Serikali mradi huu wa Kikafu Chini utatusaidia kuondoa tatizo la maji. Pale Hai tunashida kubwa ya maji ya kunywa ukanda huu wa tambarare. Boma Ng’ombe, Mnadani, Weruweru, KIA hawana maji. Naomba sana Serikali fedha hizi shilingi bilioni 3.6 zikija kwa wingi zitatusaidia kuondoa tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nashukuru sana Serikali kulikuwa na mradi wa visima 18 vilikuwa vinapeleka maji Arusha imesema sasa kwa kuheshimu Sera ya Maji ni vizuri pia Hai baadhi ya maji yakabaki pale. Nashukuru sana kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema mchangiaji mwenzangu mama Anna Kilango Malecela, kwa kweli tunatakiwa kuongezea TARURA fedha ili waweze kufanya kazi. Miundombinu imeelezwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais lakini bado tunayo changamoto na mimi kule kwenye Jimbo la Hai hali si njema kwa habari ya barabara. Bado hatujafikia kiwango cha kukidhi matarajio ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, hapa niombe Mheshimiwa Waziri anayehusika, tunayo barabara moja ambayo inalalamikiwa sana sana na wakati Mheshimiwa Rais ananiombea kura pale aliwaambia nileteeni Saashisha hii barabara nitaitengeneza, ni kilometa 13. Barabara hii iliitwa barabara ya ng’ombe, jambo hili linawachukiza sana wananchi kwamba ile barabara tuliambiwa ni ya ng’ombe. Sasa hii barabara ni ya watu, tunaomba barabara ile iweze kuwekwa lami, ni kilometa 13 tu kuanzia mferejini kupita TaCRI, Lyamungo kwenda kutokea Makoa.

Mheshimiwa Spika, lakini tunayo barabara nyingine ambayo hata ninyi mkishuka kwenye ndege pale KIA mkiwa mnaenda Moshi ni rahisi, inakuwa ni barabara mchepuko inaweza kutumika kilometa 25 tu inaanzia Boma ya Ng’ombe kwenda TPC. Ziko barabara nyingi ambazo kwa kweli kama TARURA itaongezewa uwezo wataweza kufanya kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumepeleka maombi maalum ya kupandisha hadhi barabara tano zilizoko ndani ya Jimbo la Hai kutoka TARURA kwenda TANROADS. Nashukuru sana kikao cha RCC kilipitisha barabara hii. Naiomba Serikali iongeze spidi kwenye mchakato huo ili barabara hizi ziweze kuhudumiwa chini ya TANROADS.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo limezungumziwa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais ni kuhusu umwagiliaji. Naomba sana, kwa kuwa nimeeleza hapo awali Jimbo la Hai linaweza kutumika kukusanya kodi nyingi kwenye mazao haya miradi hii ya umwagiliaji iweze kufanyiwa kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini iko changamoto, niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Maji na TAMISEMI tunayo miradi iliyoko kwenye kata yetu ya Weruweru na pale Kikafu Chini, ni Jumapili tu nimetoka kwenda kutembelea miradi hii, iko shida. Serikali imeleta fedha pale shilingi milioni 91 lakini ule mradi umetulia, hakuna kinachoendelea. Tayari Serikali imeshaweka fedha ziko shilingi milioni 700 kwenye Kata yetu ya Weruweru kule Mijengweni, Serikali imeweka mashine zimefungiwa kule, naomba sana Serikali itoe pesa ili miradi hii iweze kukamilika wananchi waweze kunufaika. Hii ni miradi ya muda mrefu, Kikafu Chini ni miaka nane lakini huu mwingine wa Mijengweni ni miaka 15 mashine zimefungiwa kule na bado zina uwezo wa kufanya kazi. Naomba sana Serikali itusaidie ili kuweza kukidhi matarajio na shauku kubwa aliyonayo Mheshimiwa Rais ya kuweza kuisaidia nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo limezungumzwa kwenye hotuba hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais kupata umeme kwenye vijiji vyote. Wakati wa kampeni Mheshimiwa Rais alitoa ahadi ya kwamba maeneo ambayo hayajafikiwa na umeme wa REA yaweze kufikiwa. Niombe sana kwa kuwa Serikali imeshafanya kwa kiwango cha 84% hii asilimia iliyobaki Mheshimiwa Waziri ni ndogo sana. Wewe unafahamu na asubuhi nimezungumza na wewe kwamba yule mkandarasi pale Hai anatupa shida. Mimi naomba sasa Serikali mfanye maamuzi ili ile ahadi ya Mheshimiwa Rais iweze kutokea.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ni kengele ya kwanza?

SPIKA: Tayari muda wako umeisha.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, haya naomba kuunga mkono hoja.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa, lakini kabla ya kusema nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutupa afya na uzima. Kwa sababu ya muda nitachangia maeneo mawili tu kwenye mpango huu, nitachangia eneo la kilimo, lakini nitachangia eneo la viwanda. Na hii ni kubeba azma yetu, ndani ya Jimbo la Hai tumekubaliana kuwa na Hai mpya ya kilimo na viwanda.

Mheshimiwa Spika, Wabunge wenzangu wametangulia kueleza sana azma hii ya kuwa na kilimo cha biashara kama ambavyo imeelezwa kwenye ukurasa ule wa 65 wa mpango huu kwamba, tunadhamiria sasa kuwa na kilimo-biashara. Sasa tunazungumza sana, niombe ifike mahali sasa tuamue kwa dhati kuwekeza kwenye kilimo. Mpango huu unataja kwamba, ni eneo linalotoa ajira kwa Watanzania wengi zaidi ya asilimia 66.3 kwa hiyo, ninaomba sasa hebu tufanye kwa kudhamiria kabisa tukijua ni eneo ambalo linaenda kuokoa uchumi wetu Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwa kufanya hivyo niombe tuanze kwa kufanya utafiti wa tathmini ya udongo nchi nzima. Ninajua ziko taarifa hizi, lakini sio kwa maeneo yote na kwetu sisi pale Hai tuliomba taasisi ya TARI Mlingano wakatufanyia tathmini ya udongo ndani ya Jimbo la Hai. Faida ya kuwa na tathmini ya udongo kwenye eneo hili ni kuondoa changamoto wanazokutananazo wakulima.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, nitoe mfano, mkulima wa nyanya anapambana sana na ugonjwa wa kuungua kwa nyanya yake, lakini bila kujua kuungua kwa nyanya kinachosababisha ni aina ya udongo alipopanda. Pengine PH yake calcium iliyoko kwenye udongo sio rafiki kwa hiyo, tukiweza kufanya tathmini ya udongo tukatoa taarifa kwa wananchi itatusaidia sana.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuwa na mbegu ya hakika. Wananchi wanawekeza kwa nguvu kubwa sana kwenye kilimo, lakini je, tuna uhakika na mbegu wanayoipanda? Lakini pia mifumo ya kudhibiti mbegu zinazoingiziwa barabarani ikoje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba sana Waziri wa Kilimo unanisikia. Wekeni mifumo Madhubuti ya kuwa na mbegu zetu sisi zinazozalishwa hapa Tanzania ambazo ni rafiki kulingana na aina ya udongo tuliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuwa na maji ya hakika ya kumwagilia. Mikoa mingi ukitazama, Mkoa wa Kilimanjaro, Mkoa wa Mbeya, Mkoa wa Iringa na Mikoa mingine inayofanana na hiyo ina maji ya hakika ya kumwagilia. Tatizo ni miundombinu ya kutufikishia maji kwenye mashamba yale. Kwa mfano kule kwetu Mkoa wa Kilimanjaro na hasa Jimbo la Hai, tunavyo vyanzo vya maji, mifereji mitano. Tukipata mifereji hii namhakikishia Mheshimiwa Waziri wa kilimo tunaenda kuchangia vizuri sana kwenye pato la Taifa na tunaenda kutokomeza umasikini ndani ya Jimbo la Hai.

Mheshimiwa Spika, tuna Mfereji wa Mtambo, Isimila, Kimashuku, Makeresho, Longoi, Metro, lakini pia tunalo bwawa la kihistoria ambalo limefanyiwa utafiti na wenzetu wa China, lina maji ya kutosha, Bwawa la Boluti. Kwa hiyo, nikisema pamoja na mengine kwenye mikoa mingine tuhakikishe tuna maji ya hakika na tuweke fedha nyingi kwenye bajeti inayokuja, ili wananchi walime kilimo cha biashara ambacho hakitegemei mvua kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuwa na wataalam wa kutosha. Maeneo mengine tumeweza kupeleka watumishi wa kutosha, eneo hili la kilimo na mifugo ninaomba bajeti hii inayokuja tutenge fedha kwa ajili ya watumishi wa kutosha, ili wakatoe ushauri kule wananchi waweze kulima kilimo hiki cha biashara ambacho ndio tunalenga huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuongeza thamani ya mazao. Na hii ndio dhana yangu ya kilimo na viwanda. Eneo hili linatusababishia umasikini na wananchi kutokunufaika na mazao yao kwasababu, tunalima hatuongezi thamani. Mfano pale kwetu tunazo taarifa kwamba, wapo wakulima wafanyabiashara kutoka nje ya nchi wanakusanya mazao yetu, nyanya, mbogamboga, wanapeleka nchini kwao wanaenda kufungasha. Wakifungasha wanaturudishia sisi kununua nyanya ileile, kununua karoti ileile kwasababu tu, wameongeza thamani ya mazao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba sasa kwenye mpango huu Waziri wa viwanda tuhakikishe tunakuwa na viwanda vingi vya kuongeza thamani ili mazao yetu yaweze kuuzika ndani ya nchi na nje ya nchi yakiwa yamefungashwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine tuimarishe taasisi zetu, hii taasisi ya TARI, Mlingano na taasisi nyingine zinazofanana na hivyo zijengewe uwezo. Tunao wataalamu wengi ukienda Wizara ya Kilimo pale utakuta wapo wataalamu wengi na wengi wamesoma nje ya nchi. Huko kwenye mashamba makubwa duniani wamesoma huko, lakini wamekaa ofisini pale tunataka watoke ofisini…

SPIKA: Asante sana Mheshimiwa…

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: …aai.

SPIKA: Dakika tano zimekwishapita. (Makofi)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Hotuba ya Waziri wa TAMISEMI na nianze kwanza kwa kupongeza wananchi wote wa Tanzania kwa namna ambavyo kwa kweli wanaiunga mkono Serikali pale ambapo Serikali inapeleka fedha wao wanaongezea. Tumeona ambavyo Serikali inapeleka shilingi milioni 12 kujenga madarasa wao wanaweka nguvu kazi na michango yao, nawashukuru sana. Lakini niwashukuru watumishi wote wa umma ambao ndiyo wanaosimamia fedha ambazo tunapitisha hapa, nasema ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niwapongeze wasaidizi wa Waziri nikianza na Katibu Mkuu, Naibu Makatibu Wakuu kwa kazi kubwa wanayoifanya, tunawashukuru sana. Lakini majemedari hawa watatu, Naibu Mawaziri wawili na Waziri wao, sisi watu wa Hai tumewapa majina; ndugu yangu Festo kule wanamuita mzee wa nkwansira na anajua kwa nini wanamuita nkwansira na ndugu yangu Silinde hapo wanamuita mzee wa makeresho anajua kwa nini wanamuita hivyo, Waziri nitakupa jina lako nikimaliza kuchangia hotuba yangu wanakuitaje kule Hai. (Makofi)

Kwa kweli kwa ujumla tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kutuletea vijana hawa wenzetu wachapakazi ambao kwa kweli wanabeba sura nzuri ya Tanzania, kazi zinakwenda kwa viwango vya hali ya juu. Mheshimiwa Rais tunakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niombe pia nimshukuru sana Waziri. Ninakushukuru Waziri na watu wa Narumu watu wa Hai kwa ujumla wanasema ahsante sana. Tulikuwa na barabara yetu ya kuanzia Mferejini kwenda Makoa kilometa 18 imeanza kujengwa kwa maandalizi ya kupokea lami, wewe umeniahidi unaenda kumaliza fedha zile ili lami ikamilike ya barabara ile, tunakushukuru sana. Lakini tunakushukuru umetuahidi barabara ile ya Bomango’ombe kwenda TPC kilometa 25 na yenyewe itajengwa kwa kiwango cha lami. Tunasema ahsante sana Mheshimiwa Waziri na sisi tunakuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijikite kwenye hotuba ya Waziri na nianze na eneo ambalo tumelijadili sana, mimi ni mjumbe wa Kamati ya USEMI. Eneo la asilimia 10 fedha ambazo zinatokana na mapato ya Halmashauri; fedha hizi zinakopeshwa makundi matatu, kundi la vijana, kundi la walemavu na kundi la wakinamama. Lakini wakati tunapitia taarifa hii kumekuwa na changamoto, fedha hizi zina matatizo makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninasimama hapa kumshauri Waziri, na Waziri wewe umeshiriki kwenye Kamati umeona kilicholetwa pale. Fedha hizi zinatumika visivyo, fedha hizi taarifa zake haziko sahihi. Sasa ninaomba sasa hivi ukitazama kuanzia Januari mpaka leo kuna shilingi bilioni 35 ambazo zimekwishakopeshwa. Kwa hiyo, utaona ni fedha nyingi sana, lakini Mikoa imeleta taarifa ambazo zina mapungufu mengi sana ambazo hazioneshi marejesho kiasi gani yamerejeshwa, fedha kiasi gani zimerejeshwa na vikundi. Sasa ninachoshauri hapa; moja, ninaomba tulete sheria ile hapa ifanyiwe mabadiliko. Tufanye mabadiliko kwanza kuongeza kundi la wanaume, maana wakina baba wamesahaulika kwenye hili, nimeshashauri tena Bunge lililopita, lakini narudia tena na kwenye kamati tumesema tuongeze wigo mpana ili na wanaume nao waweze kukopesheka na wanufaike na hizi pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa Waziri kanuni zako ziongeze makali ili kuwe na akaunti maalum ya kupokea fedha hizi, lakini na akaunti maalum ya kupokea fedha za marejesho ili mwisho wa siku tuweze kuona kwenye 10 percent tumekata kiasi gani, zile za marejesho ziko wapi tujumlishe za marejesho, tujumlishe zile asilimia 10 lakini tutoe fedha zao za usimamizi. Hizi zinazobaki tuone zinakopeshwa kwa kiwango gani. Lakini pia kama ambavyo tulishauri kwenye Kamati, naendelea kusisitiza ni muhimu sana tuwe na mfumo wa ku-capture mambo haya. Fedha hizi zitolewe kwa mfumo wa TEHAMA ambavyo Wizara inaweza kuona, level la Mkoa inaweza kuona na level ya Halmashauri na kwenye level zote hizo kuwe na watu ambao wana-approval ili kuondoa watu kukopa mara mbili, lakini kuweza kuwabana wale wanaokopeshwa waweze kurejesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba pia nizungumze kuhusu Tume ya Utumishi wa Walimu; Tume hii inafanya kazi nzuri, lakini Tume hii haijawa kamilifu. Walimu nchi hii wana mabosi wengi mno. Sasa nilikuwa naomba hapa Waziri tuone namna sahihi ya kuifanya Tume hii iwe bora, tuiongezee nguvu ili kama tukiamua ndiyo Tume ya kusimamia walimu ifanye hivyo kuliko mwalimu anasimamiwa na TAMISEMI, kila mtu ni kiranja wa mwalimu. Sasa mwisho wa siku tunajikuta hawa Walimu tunawapa mzigo mzito ambao wanashindwa kuisimamia kazi yao ya kitaaluma.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana sana kaeni chini muone namna ya kutuletea tufanye mabadiliko, walimu wawe centralized somewhere wasimamiwe na chombo kimoja ambacho kwa mawazo yangu Tume ya Utumishi wa Walimu ingefaa kuwa chombo sahihi cha kusimamia walimu Tanzania na kuwaacha walimu kutokusimamiwa na watu wengi kama ilivyo sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia naomba nishauri jambo linguine, tunaenda kupitisha hapa bajeti na kwenye bajeti hii vifungu vya usimamizi vimeongezeka sana na kupelekea matumizi ya miradi kushuka zaidi ya asilimia 14 jambo ambalo ni zuri na ofisi ya ma-DC zimepata fedha za kutosha.

Naomba kushauri hapa ofisi za Maafisa Tarafa ambapo ni kiungo kati ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa hao Maafisa Tarafa wamekuwa watu wa kuishi kwa hisani kitu ambacho siyo sawa, sasa ofisi za ma-DAS zimepewa fedha. Mimi niombe wapewe special vote ya kwao. Kwa sababu ofisi ya Afisa Tarafa inajitegemea wapewe sub-vote yakwao ili kwamba kama wanahitaji matumizi yao fedha ziende kule kuliko ilivyo sasa hivi pesa zinapelekwa ofisi ya DC halafu inakuwa ni utashi wa DAS kuwapa au kutokuwapa. Kwa hiyo, niombe sana hawa watu wanatusaidia kwenye usimamizi wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niombe tutazame tena, wenzangu hapa wamezungumza kuhusu posho za Madiwani. Mimi niseme kwa Madiwani tumefanya vizuri, lakini tuone namna ya kuwaongezea na Wenyeviti wa Mitaa. Tufike mahali pia tutazame hata Watendaji walioko kule, tunafahamu wanapata mishahara yao, lakini hebu tuwatazame namna ya kuwapatia mafunzo ili na wao waweze kufanya kazi kwa wakati. Wakati mwingine tunapeleka tu, tunashindilia maagizo kule kwa Watendaji wa Vijiji, Watendaji wa Kata lakini hatuwapi taaluma ya nini kinatakiwa kufanyika kwa wakati ule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ninaomba nizungumze kuhusu miradi ya kimkakati; hii miradi ya kimkakati wenzangu hapa wameeleza masoko maeneo mengi hayakufanya vizuri, kwa sababu walioibua mikakati ile hawakutufikisha mwisho.

Mimi niseme Mheshimiwa Waziri pale Hai tuna soko la Kwa Sadala tayari tumeshakuletea ramani hapo. Mimi niombe hebu tukajifunze pale Hai kwa kujenga hilo soko. Lile soko letu lina kitu cha tofauti, mle ndani tumeweka sorting industry, mle ndani tumeweka viwanda vya kufungashia, mle ndani tumeweka viwanda vya kuongeza thamani mazao. Lakini pia tumeweka sehemu ya wakinamama kuwaacha watoto wao wapumzike pale kama day care center, na soko liko mjini pale Kwa Sadala. Soko ambalo ukitazama linapokea karibu kata zote na nchi nyingi zinakuja kununua pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niombe huu mradi Mheshimiwa Waziri tafadhari sana mtusaidie na ni ahadi ya Mheshimiwa Rais. Rais mwenyewe ameahidi pale mara mbili soko hili la Kwa Sadala, tafadhalini sana mtusaidie lijengwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme jambo moja jana nilikuwa kwenye msiba kwenye Kata Uroki pale Uswaa. Mheshimiwa Waziri kila aliyekuja kunipa mkono pole Mheshimiwa Mbunge alikuwa ananiambia tuna barabara yetu; barabara ya Uswaa – Kwa Sadala; Uswaa - Bwani kuna mahali ambapo pale Uroki pa kupandia juu hapapitiki kabisa na ile barabara ndiyo tunategemea ipitishe ndizi zile Kwa Sadala, ipitishe ndizi zije Dar es Salaam, zije kwetu hapa Dodoma. (Makofi)

Niombe sana, inawezekana nimekuomba maombi mengi ya lami na wewe umeniahidi lakini hii basi hata changarawe, angalia fungu chochote unachoweza kupata hata kwa kipande kile kidogo cha pale kwenye bonde la kushuka Uroki.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye mawasilisho ya Kamati hizi mbili.

Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa na niwapongeze Mawaziri wote wanao-appear kwenye Kamati yetu wanatoa ushirikiano mkubwa na wanapokea ushauri.

Mheshimiwa Spika, mimi nilitaka nishauri jambo la kwanza hapa kuhusiana na mikopo ya asilimia 10 inayotolewa kwenye mapato yote ya halmashauri kwa ajili ya kwenda kukopeshwa kwenye makundi ya Vijana, akina mama na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa tukishauri na ninaomba sasa Serikali ikubali kupokea ushauri huu, kuongeza kundi la akina baba. Inatuletea migogoro na sasa hivi imefika mahali wakina baba wanalazimika hata kama hana mpango wa kuoa inabidi aoe ili apate mama ambaye atapata sifa ya kwenda kukopesheka maisha yaendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, matatizo haya ya kijinsia tunayohangaika nayo mengine psychologically yanasababishwa na sisi wakina baba kukosa kitu mfukoni.
Sasa unaona mama ndiye anayetoka anaenda kwenye VICOBA, mama ndiye anayetoka anaenda kukopeshwa, sisi wababa tunabaki ndani tusubiri mama alete. Hili jambo linatuathiri akina baba kisaikolojia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Serikali ifanye mabadiliko, sheria hii wakina baba waingizwe, makundi yote yaweze kukopeshwa na uzuri mfuko huu umeshakua sana, sasa hivi kwa mwaka zinatolewa zaidi ya shilingi bilioni 68. Kwa hiyo, naomba nianze na hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, kuhusiana na soko la Kariakoo; sheria iliyoanzisha soko hili la Kariakoo ni ya mkoloni, imefanyiwa mabadiliko mwaka 2002, lakini hapa kwenye Kamati tumeshauri soko hili sasa tufanye mabadiliko ili liweze kusimamia masoko yote nchini bila kuathiri mapato ya halmashauri husika. Maana wasiende kusimamia halafu wakachukua na mapato ya halmashauri, hapana wasimamie.

Mheshimiwa Spika, sasa wakati tunapitia kwenye taarifa za utekelezaji wa soko la Kariakoo nilihangaika na wenzangu kutafuta wapi madalali wanaingia kuchangia Serikali, hatukuwaona. Kwenye organization structure hawamo, lakini leo ukienda pale Kariakoo umelima nyanya yako kutoka kule Ng’uni, Mkalama, ukibeba pale Kariakoo kuna watu wananitwa madalali. Hawa watu ndio wanaopanga bei, Wizara ya Kilimo hawawajui, uongozi wa soko wenyewe hawawajui, lakini ndio wenye sauti.

Mheshimiwa Spika, leo tunazungumza Mheshimiwa Rais ametupatia bilioni 958 zimeenda kwenye Wizara ya Kilimo, lengo ni nini? Zikamguse yule mkulima wa chini. Sasa tusipomlinda huyu mkulima wa chini ambaye ndiye mzalishaji anufaike, leo analima kuna mtu anakuja kumpangia afanye nini.

Mheshimiwa Spika, kule kwangu kuna terminology kubwa sana za madalali na lumbesa. Mkulima akishalima, yaani kazi ya mkulima wa nchi hii yeye analima, akishavuna tu sio kazi yake. Kuna mtu pale anaitwa dalali yeye ndiye anayeamua nini kifanyike, kuna mtu anaitwa mchambuzi; kwanza bidhaa yake akishavuna kama ni kitunguu anapokea mchambuzi, anachambua ni cha aina gani? Anampa dalali na moja ya sifa/principle ya dalali ni marufuku mkulima kukutana na mnunuzi, yaani yeye analima anamkabidhi dalali, dalali ndiye apange. Hiki kitu naomba tukitazame vizuri, kinaua uchumi wa wakulima wetu kule chini.

Mheshimiwa Spika, kama tunawapenda hawa madalali basi kuwe na mfumo rasmi wa kuwasimamia, wachangie pato la Taifa, lakini na wao wajue kwamba Nyanya inalimwa shilingi ngapi, kuna process ngapi za kulima nyanya, sio kusubiri nyanya wachukue wao wapange bei.

Mheshimiwa Spika, imefika mbali sana, wakati mwingine mpaka watu wanatoka nje ya nchi wanaingia ndani mwetu, tunapenda kweli kufanya nao biashara, wanakwenda kununua kule kwa mkulima chini kupitia dalali. Jambo hili naomba sana Serikali ichukue hatua za haraka. Jitihada hizi kubwa za Mheshimiwa Rais za kuhakikisha anamkomboa mkulima, kama hatutaangalia mwisho wa kazi anayoifanya, maana hapa tunapanga, peleka mbegu, peleka sijui umwagiliaji, peleka sijui vitu gani mwisho wa siku hatuangalii anaenda kuuzaje. Ninaomba sana Serikali ituangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili la lumbesa kule kwangu kuna majina mengi kweli kweli tumepewa, kule kuna aina nyingi; moja inaitwa neti ya kuvuta, hii inabeba ndoo kumi na mbili na anayepanga ni dalali na mchambuzi ndiye anayekwambia weka hapa, mkulima hana shida. Yule dalali anakuja tayari akiwa na risiti ya faini ya lumbesa, ameshalipa Serikali/halmashauri. Kwa hiyo, hakuna mtu wa halmashauri anayemfanya chochote kwa sababu ameshalipa faini.

Mheshimiwa Spika, kuna nyingine inaitwa shishimbi, hii inabeba ndoo kumi na nne na mimi niseme tu Mheshimiwa Mwigulu haya ndio uchumi wetu. Hizi principle zenu za uchumi na theory mnazo, maana jana nilimsikia hapa anasema Wabunge kama hujasoma uchumi sijui usichangie mambo ya uchumi. Uchumi ni haya maisha haya tunayoyazungumza na bahati nzuri Wabunge wote waliopo humu wako makini na wanajua uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu kwa tafsiri nyepesi tu ukisoma wakina Smith, wakina nani, wataalamu wa uchumi duniani, wanahitimisha kwamba uchumi ni shughuli zote za binadamu zinazolenga kutekeleza mahitaji yao. Kwa hiyo, humu ndani Waheshimiwa Wabunge wote ni wachumi pamoja na wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yaani uchumi tunazungumza nyanya hapa, tunazungumza vitunguu, Mheshimiwa Mwigulu ndio uchumi huu na uchumi ukipanda au ukishuka tunauona kwenye hivi vitu. Nikiona nina kuku wangu wawili wakiongezeka wakiwa watatu ndio uchumi huo kwetu sisi. Sasa hayo ma-principle makubwa nendeni nayo huko duniani mtuletee fedha sisi tunataka hivi vidogo vidogo vya kwetu. Tukilima vitunguu vyetu tupate fedha ndio uchumi. (Makofi)

Kwa hiyo, translation ya uchumi ishushwe ije kwa mwananchi wa kawaida ili tukizungumza uchumi tuelewane sote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitaka nishauri hilo na kuitisha kwa kuomba sana mtusaidie hawa madalali wasiwe na sauti, ikiwezekana mkulima ndiye amwambie dalali fanya hiki na sio dalali amwambie fanya hiki na sifa ya dalali na yeye alime, akiwa analima kama ni dalali wa kitunguu tuone shamba lake, halafu ndio tumpe kazi ya kuwa dalali kwa sababu atakuwa anajua uchungu wa kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumze kidogo kuhusiana na Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, hii Bodi ni ya muda mrefu na yenyewe, imeanzaishwa tangu mwaka 1953...

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Mafuwe, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kenneth Nollo.

T A A R I F A

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe tu taarifa mzungumzaji kuwa hoja ya dalali kwamba lazima awe na shamba, anapokuja tu point yake kutofika mwisho ni kwamba tuimarishe Vyama vyetu vya Ushirika viwe strong ili wananchi wetu wawe na uhakika wa sehemu kwenda kuuza, ahsante sana.

SPIKA: Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, huyo ni shemeji yangu, kwa hiyo, sina namna ya kuacha kuipokea.

Mheshimiwa Spika, Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa imeanzishwa mwaka 1953.

SPIKA: Mheshimiwa Mafuwe unapokea taarifa ya Mheshimiwa Kenneth Nollo?

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ninaipokea. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30 nakuongezea umalizie kengele ya pili imeshagonga.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nashauri Bodi hii ya Mikopo ya Serikali za Mitaa sheria yake imekuwa ni ya muda mrefu sana, yaani ina sura bado ya kikoloni na bado ina madeni mengi sana. Huu mfuko mpaka sasa hivi una kama bilioni 14.6 lakini una madeni ya bilioni nne na bado ni kama Waheshimiwa Wabunge hapa tukizungumza ni kama haueleweki eleweki hivi.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nashauri kwa kuhitimisha mfuko ufanyiwe reforms ili ufanane na mazingira yetu.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja zote. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu sana. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye amebeba dhana hii ya mahitaji ya maji kwa Watanzania na kwenye hotuba yake akaeleza kinagaubaga kwamba ataenda kusimama kuhakikisha Watanzania wanapata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama niliwahi kusema hapa sio mzuri sana wa kusifiasifia, lakini huwa nasifia kwa sababu. Sasa naomba sana nimsifie Mheshimiwa Waziri kwa namna ambavyo anapambana na wale wazinguaji, hongera sana. Pia Naibu Waziri kwa kazi nzuri aliyoifanya wakati amekuja kwenye ziara yake pale Hai. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Hai tulikuwa na watu wanaotuzingua sana kwenye zile Bodi za Maji walikuwa na utaratibu wao wamejiwekea, wanalazimisha wananchi kununua vifaa kwenye maduka yao, lakini alivyokuja pale alitoa tamko la Serikali na leo wananchi wa Hai wanafurahia, wananunua vifaa kwa bei ya soko na sehemu wanayoitaka, nipongeze sana kwa hilo. Nipongeze ziara ya Naibu Waziri pia ilinisaidia sana tukapata maji kule Rundugai. Sio hivyo tu nafahamu kwamba chanzo chetu ambacho kilikuwa kimesimama muda mrefu pale Kikapu Chini na chenyewe kimetengewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana pamoja na hayo mazuri machache ambayo wameyafanya ndani ya Jimbo la Hai, lakini bado tunayo changamoto kubwa ya maji. Wakati wa kampeni, Mheshimwa Hayati Dkt. Pombe John Pombe Magufuli, aliwaambia watu wa Hai wakati anaomba kura, mmenifunga kwa kipindi cha muda mrefu, naomba nileteeni Saashisha na Madiwani wake mnifungue niwaletee maji. Sauti hiyo bado ipo kwenye mwangwi wa masikio ya watu wa Hai, pale Jimbo la Hai tunashida ya maji sana nadhani na sisi tunapaswa kuingizwa kwenye maajabu ya dunia, kwa sababu tunavyo vyanzo vya maji vya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mlima Kilimanjaro unatiririsha maji mazuri ya kunywa lakini tunalia kwamba Jimbo la Hai hatuna maji. Chini wataalam watatuambia tuna maji ya kutosha, lakini hatuna maji, hususani kata za tambarare, kuanzia Kata ya KIA, Muungano, Bondeni, Boma Ng’ombe, Weruweru, Rundugai, mpaka Mnadani hakuna maji; nazungumza hakuna maji kabisa na Mheshimiwa Waziri anajua. Tunafahamu kulikuwa na jitihada mradi mkubwa wa Serikali wa kupeleka maji Arusha, nikawaomba jamani huwezi kupeleka maji Arusha ukaacha watu wa Hai hawana maji, kuna visima 18 vinachimbwa ndani ya Wilaya ya Hai, lakini vinapeleka maji Arusha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawapenda sana ndugu zetu wa Arusha, lakini nashukuru nilizungumza na Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Arusha akaniahidi kwamba vyanzo vile vya maji vitapitisha maji pale Hai. Hili ni jambo la sera ya maji kwamba maji yanapogundulika yanaanzia basi wale wanufaika wapate maji. Niiombe sana Serikali pamoja na kwamba najua ni gharama kubwa kuyaleta maji pale lakini chanzo hiki kitumike watu wa Bomba Ngombe na KIA waweze kupata maji, maana hii ndio changamoto kubwa tuliyonayo Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, suluhisho lingine ambalo tunaweza kutumia tuna chanzo cha hakika na kimeshafanyiwa upembuzi yakinifu, thamani yake ni bilioni 3.5. Hii Serikali ya mama Samia Suluhu ina hela, tunaomba watusaidie pale fedha za kutosha. Nafahamu jitihada ambazo wamefanya wametutengea milioni 500, milioni 500 kwenye bilioni tatu bado ni ndogo. Niombe sana kama inawezekana kwa level ya Wizara tafuteni mkandarasi, chanzo hiki kianze kujengwa, tuna shida kubwa ya maji na kwetu kukosa maji wakati tunaona Mlima Kilimanjaro pale na tunaona vyanzo kibao vya maji kwa kweli ni aibu niombe sana Mheshimiwa Waziri atusaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, tunazo Bodi za Maji pale. Bahati nzuri baada ya ziara ya Naibu Waziri tulifanya vizuri sana, tukarekebisha zile bodi. Niombe zile bodi zinaweza kulelewa vizuri na zikafanya vizuri sana. Kihistoria tumeanza nazo tangu tukiwa watoto. Kwa hiyo niombe Waziri asiziguse sasa hivi kwa sababu zimeanza kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine niombe, wakati Mamlaka ya Maji Wilaya ya Hai haijaanzishwa tulikuwa na mali zetu na hapa nilizungumza na Waziri, naomba nirudie tena kusema, tuna mali zetu zilipelekwa Mamlaka ya Maji Moshi Mjini, pesa taslimu milioni 357 na ushee, lakini kulikuwa na madeni ya milioni 300 ambayo waliambiwa wakakusanye, kulikuwa na magari sita, kontena ambalo lilikuwa na vifaa vya watu wa Hai vyenye thamani ya bilioni mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine niombe, wakati Mamlaka ya Maji Wilaya ya Hai haijaanzishwa, tulikuwa na mali zetu. Na hapa Waziri nilizungumza na wewe, naomba nirudie tena kusema; tuna mali zetu ambazo zilipelekwa Mamlaka ya Maji Moshi Mjini; pesa taslimu milioni 357 na ushehe. Kulikuwa na madeni ya milioni 300 ambayo waliambiwa wakakusanye; kulikuwa na magari sita; kulikuwa na kontena ambalo lilikuwa na vifaa vya watu wa Hai vyenye thamani ya bilioni 2.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Serikali itujereshee vitu vyetu, hizi ni hela za watu wa Hai na Siha ambazo waliweka ili ziweze kuwahudumia kwenye eneo la maji. Na nina wasiwasi na hizi fedha kama kweli bado zipo, kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja kuhitimisha hapa utuambie hizi fedha zetu tutazipata lini. Kwako siwezi kushika shilingi kwa sababu wewe na Naibu Waziri mmetusaidia sana watu wa Hai.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ninataka nichangie; hivi karibuni tumepata mafuriko makubwa ndani ya Jimbo la Hai. Mafuriko haya yamesababisha maafa makubwa; tumepoteza ndugu zetu watatu, na nyumba karibu 1,500 watu wamekosa sehemu ya kuishi, kwa hiyo, sasa hivi kule tuna njaa haswa. Tunashukuru Serikali imetupelekea chakula lakini bado wananchi tathmini ya mazao yao na vitu vingine vilivyoharibika havijaguswa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye eneo la maji tuna vyanzo ambavyo vimeharibika na hakuna maji kabisa. Mto wa Nau ambao ni chanzo cha maji hakuna maji kwasababu kimeharibiwa na mvua; Mto wa Semira chanzo kile cha maji kimekufa; Mto Alonzo chanzo cha maji kimekufa; Makoa chanzo hiki kimekufa; pale Kalali tuna chanzo chetu cha maji na chenyewe kimekufa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana wananchi wanalia, shule za sekondari pale Msufini hakuna maji, pale Kalali hakuna maji, shule nyingine za Machame Girls na shule kubwa hizi zote hakuna maji kwasababu vyanzo vile vya maji vimeharibika sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, na miundombinu hapa katikati ukiachilia kule kwenye vyanzo vya maji na vyenyewe vimeharibila kwasababu ya mvua hizi. Kwa hiyo, niombe sana Serikali iingilie kati iturejeshee maji. Ukanda huu wa juu hakuna maji, kule chini hakuna maji, lakini kama nilivyosema vyanzo vya maji ni vingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni shauri, ni kwa faida ya nchi si kwa Jimbo la Hai tu. Hapa tuna mahitaji ya maji lakini vifaa vya kusababisha tupate maji ni ghali mno; tuone namna ya ku-regulate bei za hivi vitu kwa kupitia ruzuku, watu watuletee vifaa vya kuchimba kisima na mitambo hii ili tuondoe tatizo hili kwa level ya Kitaifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia na nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais, pongezi zangu za kazi nitawapa baada ya kumaliza matatizo ya Ushirika.

Mheshimiwa Spika, pia, ninawashukuru wataalam wakiongozwa na Katibu Mkuu, kwa kweli nimepita kwenye hotuba hii kuna mambo nimeyaona mazuri mazuri hasa ujenzi wa skimu, kwa hiyo, kuna msemo mmoja wa Machame wanasema nyamnya mwishanyo hufoo angalau kuna mambo tumeyaona.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumze kuhusu Ushirika, lakini naomba nizungumze taratibu kabisa leo Mheshimiwa Waziri kaka yangu na Naibu Waziri, wanielewe kwamba huku kuna shida. Katika maeneo yana majizi ni kwenye Ushirika na hao ndio wanaoturudisha nyuma, hao ndio wanafanya kilimo nchi hii kisiendelee. Ukisoma Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, imeeleza vizuri nia njema ya chama na Serikali kuhakikisha Ushirika unabadilisha maisha ya watanzania. Naomba kwa ruhusa yako uniruhusu nisome mistari michache tu, kwenye Ilani hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ukurasa wa 30 pale wanasema, Chama Cha Mapinduzi kinaamini kuwa, Ushirika ni njia ya uhakika ya kuwezesha wanachama kuwa na uwezo mkubwa wa kutatua matatizo yao ya kiuchumi, kijamii kwa kutumia juhudi zao za pamoja katika kufikia malengo, hiyo ndio Imani ya Chama Cha Mapinduzi lakini ndio imani ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, uhalisia ni kinyume kabisa na hiki kilichoandikwa hapa, haya Maushirika sasa hivi sio Ushirika tena Mheshimiwa Waziri na wewe unajua, ni watu wachache 7 wanaitwa Bodi za Ushirika ndio wanaoendesha mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawa wanaingia mikataba ya ovyo duniani hujapata ona, anakuja mtu anaitwa mwekezaji, anapewa shamba kwa bei ya kutupa, humo ndani yaliyoandikwa kwenye mikataba ni mambo ya hovyo, ukijaribu kuwaambia naomba tuone wanakuambia sheria ya Ushirika ya mwaka 2013 haimruhusu Mbunge kujua kinachoendelea, haimruhusu Mkuu wa Wilaya, haimruhusu Mkuu wa Mkoa, haimruhusu Mwenyekiti, haimruhusu Diwani, hii kitu gani hii! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri majuzi nilienda ziara ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii. Tumekwenda kwenye ziara ile na Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii na Naibu Waziri, kwenye chama kimoja cha Ushirika cha Makoa Waziri alipofika kule akaniambia Saashisha sasa nimekuelewa. Ule mkataba ni aibu, vitu vinavyofanyika pale havifai kusema hapa, maana duniani wanatusikiliza watatushangaa kwamba, Tanzania kuna kitu cha namna hii.

Mheshimiwa Spika, mtu anapewa mkataba miaka 60, miaka 30 halafu kwenye ule mkataba kuna madalali zaidi ya saba. Nilisimama pale namueleza Naibu Waziri yuko hapa, dada yangu nilikuwa naye Masanja, nawaambia hebu niambieni ninyi wataalam mmesomeshwa kwa fedha za nchi hii hiki ni nini?

Mheshimiwa Spika, mtu amepewa vibali vya kwenda kuhudumia wanyama hana document yoyote na Vyama hivi vya Ushirika, bado hapa tunasema watu wanaona sijui vitu gani? Ukizungumza kule Hai moja ya kero na iliyosababisha umasikini ni vyama hivi vya Ushirika. Kihistoria nilishasema nia ya Serikali ilikuwa ni nini na sisi kwenye mashamba haya kupitia Ushirika huo huo. Sisi Ushirika wetu kule unachukua Kijiji kizima wanakuwa ni sehemu ya Ushirika. Tulikuwa tunalima kwenye haya mashamba sisi hatuna ardhi ya kutosha kwa hiyo, kwetu sisi nusu heka ni kitu kikubwa mno. Kwenye nusu heka ile tulikuwa tunalima tunapata mahindi, tunapata maharage, tunapata alizeti, tunapata chakula cha ng’ombe.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, mazingira yetu ya kulima eneo letu limegawanyika kuna sehemu makazi ya watu, lakini kuna sehemu maalum ya kulima. Kule wanapolima watu ndipo ambapo mashamba haya yameshikwa na Ushirika. Asilimia 78 ya mashamba yetu yako chini ya Ushirika, yanaamuliwa na watu saba tu kitu hiki ni hatari. Ni hatari kubwa kwa sababu wao ndio wanaoamua, leo hii tunazungumza mashamba, shamba kama la silver day amepewa mtu pale hajalipa miaka mitatu. Lakini yumo ameshikilia na sisi hatuna pa kulima, ndio maana ilifika mahali nikasema sisi tutaenda kugawana kazi yangu rahisi sana kwasababu, mashamba tunayaona Mheshimiwa Waziri wewe unajua yaani ukifungua moyo wako unajua matatizo yaliyoko kwenye Ushirika tutaenda kugawana mashamba yale sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwape mfano mmoja, Jumapili moja nilikuwa naingia kanisani tena bahati mbaya nimeingia kwa kuchelewa. Nimefika katikati mama mmoja bibi akanishika shati nikamcheki huyu mama vipi! Ikabidi nitoke naye nje akaniambia Saashisha sikiliza, mimi nimeshiriki kwenye vita ya Uganda niko tayari kupigana tunataka shamba letu la Silver Day. Huyo ni mwananchi wa kawaida tena bibi halafu mnataka Mbunge nije hapa niwasikilize, mimi kuna siku mtaniweka ndani kwenye mambo haya ya Ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana kama mashamba tunayaona si tunaenda kugawana tu, hatua 20 nusu heka Masawe chukua, Kimaro chukua tunagawana halafu mtakuja kukutoa na polisi. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, haiwezekani namna hii watu wachache wanafanya maamuzi kwa sababu yetu, tunawaambia hapa fedha zinazolipwa kule hiyo heka moja inakodishwa kwa shilingi 65,000 dola. Tena wanatuwekea viingereza vigumu vigumu, ili kuwababaisha watu dola 65 yule mtu anaenda kumpangisha tena mwananchi kwa shilingi 300,000/= mpaka 350,000/= kwa hiyo, fedha yake aliyokuja nayo inarudi pale pale na mengine yako tupu.

Mheshimiwa Spika, hiyo fedha yenyewe dola 65 haifiki kwa mwananchi, hata kama inafika kwa mwaka kwa mfano, analipwa shilingi 45,000,000/= zinapigwa, zinapigwa mpaka kufika kwenye kile kijiji kinachohusika, inafika shilingi 5,000,000/= unaambiwa ikajenge choo cha shule. Kweli leo tunabadilishana mahindi, maharage, chakula cha ng’ombe na kuondoa ujinga maana mtu asipofanya kazi atakuwa mjinga. Vyote hivi tunabadilishana kwa kujengewa choo cha shule ya msingi! Hapana. Niiombe sasa Serikali ikubali na Mheshimiwa Waziri hili unalimudu kwani hivyo Vyama vya Ushirika kuna miungu si ni watu! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwani ukitamka kuanzia leo Mkoa wa Kilimanjaro nasimamisha viongozi wote wa Ushirika tuunde upya. Nimekaa na Mrajisi nikapita naye document hii hapa nikamuambia Mrajisi hebu tazama yeye mwenyewe anaumia kama mimi. Nimekaa na wewe Mheshimiwa Naibu Waziri na wataalam wako unaumia kama mimi, wale wataalam wako uliosema wakachunguze kule nimekaa nao wanalia kama mimi, hivi kwa nini hatuchukui maamuzi? Kama wote tunaona tuna majizi! Hebu ifike mahali niiombe Serikali iingilie kati, tufanye na sio kwamba nachukia Ushirika napenda Ushirika. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Saashisha muda, unga mkono hoja. (Kicheko)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa naunga mkono hoja kwa sababu, ameniwekea fedha za umwagiliaji, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Wizara hii muhimu sana na nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya na kwa kweli kwenye hotuba yake nimepita nimeona miradi kadhaa wameweka kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Hai, ahsanteni sana.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba nianze kwa kuchangia kwenye eneo la Vyama vya Ushirika Maziwa na hapa niwapongeze sana wenzetu wa Vyama vya Ushirika ndani ya Mkoa wa Kilimanjaro, lakini hususani Jimbo la Hai wanafanya vizuri sana na wanafanya vizuri kwa sababu wamejiratibu vyema na sasa hivi tuna mradi wa kutengeneza chakula cha mifugo pale Uduru ni kwa sababu ya ushirika mzuri; huko haufanani na kule kwingine nilipokua napigia kelele, lakini hapa wanafanya vizuri sana.

Nimuombe Mheshimiwa Waziri tafadhali tusaidie kuratibu vyama hivi vya ushirika kwa sababu viko tofauti tofauti vikae pamoja na wawe na mipango ambayo inatuwezesha kuwa wamoja, kama wakiweza kuunganisha nguvu yao tunaweza tukapata kiwanda cha maziwa na bahati nzuri walishaanza mchakato wa kutafuta eneo la kujenga kiwanda cha maziwa. Kwa hiyo, mtusaidie kuwa coordinate vizuri ili wawe na mpango uliofanana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye ushirika huo kumekuwa na changamoto kwa sababu hawajakaa pamoja kwa hiyo vyama viko scatterd, Mheshimiwa Waziri labda nikueleze kidogo namna ambavyo sisi tunafuga; katika Jimbo la Hai tuna ufugaji wa aina mbili tofauti, tuna wafugaji wa Kata hizi za upande wa Kaskazini wanafugia ndani. unakuta mwananchi ana ng’ombe wake wawili/watatu anawafugia ndani, kwa hiyo unalazimu kuwa tafutia chakula na madawa kwa kuwaletea ndani.

Mheshimiwa Spika, lakini upande huu wa tambarare wananchi wanafuga kwenye jamii ya Wamasai kwa kutafuta malisho. Sasa changamoto zao kubwa hasa sasa hivi wale ng’ombe ambao wanafugiwa ndani ni wale ng’ombe wa kienyeji.

Sasa niwaombe sana mtutafutie namna ambavyo tunaweza kupata mbegu mpya kwa sababu tunapata shida sana sasa hivi hata kupandisha wale ng’ombe, mwananchi ili aweze kupata mbegu ya kupandishwa ng’ombe anahitaji shilingi 20,000; hii ni changamoto kwa mwananchi wa kawaida.

Mheshimmiwa Spika, lakini pia analetewa mtaalamu anakuja kubandisha ng’ombe huyo anapandisha zaidi ya mara tatu/mara nne na hiyo shilingi 20,000 ni kwa wale ambao wako karibu na mjini; vijiji kama Ng’uni ambavyo viko nje ya mji kidogo wanakuwa-charged mpaka shilingi 50,000 kuweza kupandishiwa ng’ombe mmoja. Kwa hiyo niombe kwa sababu wenzetu wa Tengeru wapo pale karibu na Arumeru, basi tuleteeni mazingira haya yawe rafiki na ikiwezekana mtuletee mbegu ambazo zinaweza kufugika ambazo tunapata maziwa ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunayo changamoto nyingine kwenye vyama vyetu hivi vya ushirika; maziwa tunayoya kutosha na niwapongeze sana wenzetu wa kule Mronga kwa kweli chama kile kimejiimarisha vizuri, wamefika mahali mpaka wameweza kutengeneza kiwanda kidogo cha kuzalisha maziwa, kule Mronga na kule Ng’uni wamefanya vizuri sana. Sasa tunafikiria badala ya kuendelea kufanya vyama vidogo vidogo waungane pamoja tujenge kiwanda kikubwa na kizuri na pale Uduru wenzetu wa Tanga Fresh walikuwa wameweka cooler yao wanakusanya maziwa.

Mheshimiwa Spika, lakini kumekuwa na changamoto, hawa wakusanya maziwa wamekuwa wengi sana, tunaomba sasa tutafute namna ya ku-centralize awe mkusanyaji mmoja ili tuweze kuuza kwa tija. Sasa hivi huku mtaani wananunua shilingi 700, lakini ukiangalia kwa bei ya soko tuna uwezo wa kununua lita kwa shilingi 1,000 kama watakaa pamoja ikiwa ni pamoja na kupata wataalamu. Tunayo shida sana ndani ya Wilaya ya Hai wataalam tulionao hawatutoshelezi. Lakini kwa upande wa tambarare huku bado kuna shida tunahitaji wataalam wa kuwafundisha ndugu zangu na bahati nzuri mimi ni Laigonan nilipewa hishima hiyo na ndugu zetu Wamasai, sasa nina kazi ya kuwalea vizuri ili tufuge kwa faida.

Mheshimiwa Spika, mimi siyo muumini wa kupunguza mifugo, mimi ni muumini wa kuongeza, lakini tufuge kwa tija na maeneo tunayo tukifunga vizuri pamoja ya kwamba eneo lile la KIA lina mgogoro wa aina yake, lakini bado tunaweza kujipanga vizuri kama tutapata wataalamu. Lakini tunayochangamoto ya kuwa na majosho ya kuweza kuwahudumia wanyama wetu, niombe sana yale yalioko pale mengi yamekufa, hatuna hata moja linalofanya kazi.

Kwa hiyo, niombe na nimejaribu kupita kwenye bajeti yako sijaona jambo hili Mheshimiwa Waziri pamoja na kwamba nilikuandikia, sasa nikuombe sana utusaidie maeneo yale ya wafugaji upande wa tambarare waweze kupata maeneo ya kulishia, lakini pia waweze kupata majosho ili waweze kufuga kwa kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa tunalohitaji upande ule ni elimu wapewe elimu kwa sababu ng’ombe ni deal, ukianza ngozi yake, ukienda maziwa, sasa tunafuga kwa upande wa tambarare tunajikita sana kwenye upande wa nyama maziwa tumesahau…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Saashisha Mafuwe…

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii. Kabla sijaendelea, naomba nitoe pole nyingi sana kwa wananchi wa Jimbo la Hai, kwa kuondokewa na mama yetu mpendwa ambaye alikuwa ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Mkoa wa Kilimanjaro, lakini ni mke wa Waziri Mstaafu baba yetu Msilo Swai.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pole hizo, niungane na wenzangu kupongeza sana uongozi wa Wizara hii. Bahati nzuri nilikwishasema mimi sio mwepesi sana wa kupongeza, ila napongeza kwa sababu. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, kwa namna ambavyo anasimamia Wizara hii na taasisi zake. Pia nimpongeze kwa sababu, yeye anafikika na anasikia akiambiwa, ni Mawaziri wenye sifa za pekee pamoja na huyu. Hata hivyo, nimpongeze Naibu Waziri kwa namna ambavyo na yeye pia ni mtu anayefikika, mama mwema kabisa huyu, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze pia watendaji wa taasisi wakiongozwa na Katibu Mkuu. Isipokuwa wale wa TAWA wao sitawapongeza kwa sababu, nina jambo nao. Vile vile nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri tulienda naye kwenye ziara kwenye Jimbo la Hai na tulitembelea eneo lile la Makoa kwenye Chama cha Ushirika. Nimshukuru sana kwa kusimamisha mkataba ule uliokuwa mbovu na leo sitaki kuzungumza jambo lile kwa sababu najua Waziri anaendelea na uchunguzi. Nimpongeze kwa hatua za awali kusimamisha mkataba ule ambao ulikuwa hauna maslahi kwa wananchi wa Jimbo la Hai. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe pamoja na pongezi hizo sasa nishauri. Tumekuwa tukipokea mapato makubwa sana kwenye Serikali kuu kwenye vyanzo vinavyotokana na maeneo ya utalii. Hata hivyo, imekuwa bahati mbaya, wananchi wanaozunguka maeneo haya, hawanufaiki moja kwa moja pamoja na kwamba, tunapokea fedha kutoka Serikali Kuu. Hili linaongeza kutokuwa na upendo na maeneo yale. Ili wananchi hao wanaozunguka maeneo haya wawe na upendo na watunze vyanzo vyetu, lazima tuone namna ya kuwa-motivate na kuwafanya wawe na upendo na vivutio hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, tuna Mlima Kilimanjaro pale, utashangaa sana wale wanaoenda kusaidia watalii wanaowapandisha mlima wanatoka nje ya maeneo yale. Lakini vile Vijiji vya Foo na vingine vinavyozunguka Mlima Kilimanjaro, wale vijana hawapati kazi hizi. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri, mimi niko kwenye mchakato naandaa database ya vijana wanaozunguka vijiji vya Mlima Kilimanjaro, ambao wana sifa za kupandisha watalii kwenye Mlima huu waweze kupata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nitakabidhi database hiyo ya vijana wa Hai, wako tayari, wana afya njema na wana sifa za kupanda Mlima Kilimanjaro. Wizara iwatumie na ipeleke maelekezo maalum kwa makampuni yanayopanda Mlima Kilimanjaro, ili waweze kuwatumia vijana hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kushauri, tuna mageti kadhaa yanapanda Mlima Kilimanjaro, lakini ukiyaangalia najua tumepita kwenye kipindi cha mpito ambacho ugonjwa ya Corona umesababisha idadi ya watalii ishuke. Hata hivyo, najua mungu ni mwema atatusaidia na watalii wanaongezeka. Kwa sababu hiyo naomba sasa tuwe na geti lingine jipya ambalo litaanzia pale barabara ya kutoka Kwa Sadala, litapita pale Ng’uni, litapia Mula kwenye Kata ya Masama Mashariki na Masama Kati. Lengo ni nini, ni kupanua wigo wa utalii kuelekea Mlima Kilimanjaro.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifungua barabara hii kuna vivutio vingi vya tofauti na barabara ile ya Machame na barabara nyingine zilizoko kwenye wilaya nyingine. Kwa hiyo naomba sana hili pia walitazame. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo napenda kushauri, Waheshimiwa Wabunge wengi hapa wamesema. Utaratibu wa kutoa vibali kusafirisha nje ya nchi lazima tubadilishe mfumo huu, tumeshatoa vibali vingi ndege wetu, wanyama wetu wanapelekwa nje ya nchi. Swali la kujiuliza hapa, hawa wanyama wanakwenda huko nje ya nchi tuna-control vipi kuzaliana kwao. Nataka niwaambie kuna siku hapa tutakosa watalii kwa sababu wanyama hao wakienda kule wanazaliana wanaongezeka na bahati nzuri wenzetu hawa wanateknolojia ya kutushinda sisi. Watakwenda kutunza hawa wanyama watatengeza zoo kubwa kubwa, mwisho wa siku huku nchini tutakosa watalii wakuja kututembelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hali ya kawaida, wewe mwenyewe huko hapa ukiona kwamba leo tutakushangaa eti unatoka hapa Tanzania kwenda kushangaa au kutembelea Zoo ya Simba nje ya nchi. Ndivyo itakavyokuwa simba watakuwa wengi, vyura watakuwa wengi, ndege watakuwa wengi na mamba watakuwa wengi kule kwao, huku hawatakuja. Kwa hiyo niombe sasa imetosha, vibali tulivyowapa vimetosha. Hili ni sambamba pia na wanyama wanaokuja kuletwa huku kwetu, iwe ni kuja kutunzwa au vinginevyo. Najua kwenye hili kuna shughuli inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi vibali vya kuruhusu wanyama kutoka nje ya nchi kuja huku kwetu tutazame. Tusije tukaletewa wanyama wa kuja kuharibu wanyama wetu. Tunafahamu hapa Tanzania sisi ndio tunaongoza kwa idadi kubwa ya simba lakini tunaletewa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niunge mkono hoja. Nashukuru sana sasa, lakini nimalizie kwa kuomba Wizara hii ishirikiane na wizara nyingine…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijatoa mchango wangu, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia Suluhu Hassan ambaye majuzi alifanya ziara yake akapita kwenye Jimbo langu la Hai na kwa kweli ametuachia ahadi kubwa sana na kukidhi matarajio ya Wananchi wa Jimbo la Hai. Namshukuru sana na Mungu ambariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Azimio hili naona limechelewa na limechelewa kwa nini? Kwa sababu tunalihitaji sana na sisi tuingie kwenye Soko la Dunia. Sasa ningependa nishauri mambo yafuatayo; Azimio hili litakuwa na faida kwetu kama tutafanya mambo yafuatayo;

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kwenye Ibara ile ya 5 inazungumza habari ya usalama wa nyama, mimea na chakula. Sasa kwenye eneo hili, sisi tumejiandaaje kuingia kwenye soko baada ya kusaini Mkataba huu? Nitaanza na eneo la Wanyama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, twende tukaimarishe Sera zetu hapa; tumekuwa tukiletewa wanyama kutoka nje ya nchi kuingia kwetu lakini pia tumekuwa tukipeleka wanayama wetu nje ya nchi baada ya muda wanarudi. Sisi tuna sheria gani ya kuweza kukinga na kuhakikisha hatupati specie mpya zinazoingizwa kwenye nchi yetu pengine zinaweza kuja kuharibu aina ya wanyama tulionao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kupitia Itifaki hii tunayoenda kusaini lazima na sisi tujiandae tuweke standard, tuweke maabara za kisasa ndani ya nchi yetu kupima vinasaba vya wanyama wanaotoka ndani ya nchi na wanaoingia ili tujiridhishe kwamba kama ni Simba wa Tanzania ana vinasaba vya aina hii asije Simba mwingine akaja kuleta kitu cha tofauti. Kwa hiyo, tuwe na Sera ambazo zitaweza kutufungia. Kwenye eneo la mimea hali kadhalika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nisimame hapa kwenye chakula. Hivi tulivyo tupo hivi kwa sababu ya chakula tunachokula. Sasa tuna usalama/sheria gani ambayo inalinda aina ya chakula tunachokula? Chakula sio tu kikiwa mezani; lazima tuangalie kuanzia namna ya kupanda, kuvuna na kukisafirisha. Hivi ukienda kwenye masoko yetu, tunayo miundombinu inayoweza kutufanya tukala chakula salama? Tunapojenga masoko yetu tunazingatia usalama wa chakula? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa nashauri ili twende vizuri na tuweze kunufaika na Itifaki hii, basi tuhakikishe suala la usalama linakaa kisheria na kwenye miundombinu linazingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumze, ili tuweze kufanikiwa, hebu tukimbie haraka sana kwenda kurekebisha Sera yetu ya Kilimo. Sera hii ya Kilimo ifanane na uhalisia wa sasa hivi na ili tuweze kufanikiwa tuziimarishe pia zile taasisi zetu. Hii ni kwa sababu ili tuweze kuingia kwenye Soko la Dunia, wenzetu wanatazama sana usalama wa chakula ambao unatengenezwa kuanzia hatua ya awali. Tuimarishe Taasisi yetu ya Mlingano iliyopo Tanga ili iweze kufanya utafiti wa udongo; ni eneo ambalo tumelisahau. Tufanye utafiti tujue kwenye udongo huu tunaweza kupanda kitu gani ili tulime kwa tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutazame sasa kuongeza thamani ya mazao yetu. Hapa tulipo ili tuweze kufaidi hii hakuna namna unaweza kuingia kwenye Soko la Dunia kama huwezi kuongeza thamani ya mazao yetu. Ndio maana utaona sasa hivi wenzetu wa nchi za Jirani wanakuja hapa wanachukua mazao yetu, wanaenda kwenye viwanda vyao vidogo wanaita sorting industry, hizo sorting industry ukitazama; bahati nzuri nimefanikiwa kufuatilia mazao yanayotoka pale kwetu Hai yanaenda nchi Jirani nikaenda mpaka huko kwao wanachokifanya wana vibanda tu wanaita sorting industry. Wanachokifanya kama ni karoti imeletwa pale wanapima karoti ukubwa huu inaitwa ni grade one, ukubwa huu grade two; hii itaenda nchi fulani, hii itabaki hapa watakula Watanzania, hili jambo tunaweza kulifanya kwetu sisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana wakati tunasaini Mkataba huu, tukimbie haraka kuimarisha sheria na taasisi zetu ili na sisi tuweze kufaidi kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo ningeshauri, ili tuweze kunufaika pia hebu Serikali itazame namna ya kuwa na kiwanja kimoja cha ndege ambacho kitawavutia watu kuja kununua mazao kwetu kupitia usafiri wa anga. Na kiwanja chenyewe tukitumie kile cha Kilimanjaro Airport, tuondoe kodi ndege zinapotua pale iwe ni free, kodi iwe ni bure pale ili tuwavutie kwa sababu changamoto iliyopo sasa hivi, mizigo kutoka huku Tanzania kwenda nje ya nchi ipo ya kutosha lakini mizigo ya kutoka nje ya nchi kuja huku haitoshi. Sasa ili kuwavutia watu waweze kuja kununua mazao yetu, tuweke Kiwanja cha KIA kile kiwe cha mkakati tuwaambie leteni ndege zenu msilipe kodi. Tukiamua hivi, itatusaidia sana kuhakikisha tunafaidi kwenye Itifaki hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho; niombe hebu tutazame sasa hivi. Tumeshazungumza muda mrefu Serikali yenyewe pamoja na kwamba tunafanya kwa ubia, hebu tengenezeni kiwanda kimoja cha mfano cha kuongeza thamani ya mazao yetu. Wananchi, tunaweza tukafanya kwa mfumo wa ushirika kama tunavyofanya kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda kwa ukanda wa kaskazini pale Hai mnajenga kiwanda cha kufungasha mazao, wanaotoka Tanga wanakuja wanafungashia pale yanaingia kwenye cold room ya KIA iliyopo pale yanaenda nje ya nchi, ili uwekezaji wa aina huu utatusaidia sana lakini kama tutasaini Mkataba huu na hatutaangalia taasisi zetu, hatujajiandaa kuingia kwenye Soko la Dunia ambalo na lenyewe lina standard ya bidhaa zinazotakiwa kuingia huko, tutakuwa hatujafaidi Mkataba huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilikuwa nashauri sana tuzingatie mambo haya, tuimarishe Sera yetu ya Kilimo, tuwafundishe wakulima wetu kulima kisasa, tulete sheria hizi tatu kwa maana ya wanyama, mimea na chakula tuzitengeneze hapa na tuhakikishe miundombinu yetu inakuwa salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye taarifa za Kamati hizi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natokea Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, tumepokea taarifa kutoka halmashauri zote nchini juu ya utekelezaji wa Miradi ya UVIKO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Raisi Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa kwa kweli aliyoifanya na ubunifu mkubwa sana, lakini niwapongeze Mheshimiwa Waziri na watumishi wote kwa namna ambavyo wamesimamia fedha hizi. Tumepokea taarifa kutoka kwenye halmashauri kwa kweli wamefanya kazi nzuri, hongereni sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo madarasa yamejengwa, vituo vya afya vimejengwa, miradi ya maji imekwenda, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri aliyoifanya na niseme kwa style hii hii Mheshimiwa Rais atafute fungu lingine alitupie kule kilimo. Kule kilimo tukipata kama shilingi trilioni moja naamini sasa tumemaliza kazi nchi hii itasonga kwa speed kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri kwenye eneo la asilimia 10; fedha hizi ambazo ni nyingi tumeambiwa hapa ni karibu ni bilioni 70 zimekopeshwa. Utaratibu wake bado hauridhishi, tumepokea taarifa kwenye kamati yetu, tunaona namna halmashauri inavyojikanganya wengine wanakiri kabisa hawana taarifa sahihi kwenye jambo hili. Sasa mimi nashauri mambo yafuatayo: -

(i) Taasisi yetu inayohusika na TEHAMA kwa maana ya e-government watengeneze mfumo wa ku–capture taarifa zote kutoka kwenye Halmashauri ili tuweze kujua fedha ambazo zimepatikana ni asilimia 10, fedha za marejesho ni kiasi kadhaa, vikundi vilivyokopeshwa ni kiasi kadhaa na majina yao ili kukwepesha ujanja ujanja, hii kazi e-GA wanaweza kuifanya waifanye ili tuweze kufanya maboresho. (Makofi)

(ii) Pia tutazame sheria, hii sheria imefanya vizuri, lakini kuna kundi linaachwa, tunasema vijana wanaokopeshwa ni kuanzia umri wa miaka 18 mpaka 35, lakini miaka 35 na kuendelea na tunaamini miaka 35 – 45 ndio kundi lenye sasa limetulia linataka kufanya kazi, kundi hili la wababa halimo. Niombe tutazame namna ya kufanya marekebisho ili na hao wanaume nao waweze kukopesheka wafaidi fedha hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana na mimi kwenye jimbo langu la Hai wamenituma, wakina baba wanasema tumeaacha kwenye eneo hili. Tafadhalini sana tulete hiyo sheria tuifanyie mabadiliko hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme hili ambalo limejitokeza, sasa hivi tunapokea taarifa ya masoko yetu kuungua na wenzangu wamechangia hapa. Niende kwenye suluhu, baada ya matukio haya nimejifunza kitu nikaenda kwenye historia; kwanza nikatazama majukumu ya Jeshi letu la Zimamoto, nikajiuliza hivi tunahitaji makamishna, tunahitaji mabrigedia, tunahitaji maafisa kwenye kuzima moto kweli. Nikagundua mwaka 1950 kazi ya kuzima moto na uokoaji ilikuwa inafanywa na halmashauri, na ilifanya vizuri, baadae mwaka 1982 wajibu huu ukahamishwa TAMISEMI, wakaendelea kufanya vizuri. Sasa hivi najiuliza administrative cost za chombo hiki zingeweza kuhamishwa zikaenda kukunua magari ya fire. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri sasa Serikali itazame upya namna ya kurudi kule kwa mwaka 1950, jukumu hili lishushwe halmashauri ambayo inakusanya, inaweza ku-manage na kuajiri watu ambao wanaweza kufanya kazi ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini watumishi au vibarua wanaweza kufundishwa ukiancha ile top layer wakafanya kazi hii kuliko kuwa na maafisa wengi wana consume a lot, halafu tunashindwa ku operate. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana watuletee sheria tuone upya namna ya jukumu hili lirudishwe kwenye Halmashauri, mfano Halmashauri za Jiji la Dar es Salaam zikipewa jukumu hili zinaweza kufanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda naomba niishie hapo na niunge hoja mkono, ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Mapendekezo ya Mapendekezo ya Mpango ulioletwa hapa mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nami nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa maandalizi mazuri yaliyoanza na uwasilishwaji wake mzuri. Ila naomba nirejee jambo ambalo nimewahi kusema humu ndani. Sioni tuna shida gani ya kukubali kupokea ushauri mpya. Mipango hii tunayoendelea nayo na utaratibu tunaoutumia wa kuandaa kwa kipindi cha miaka mitano, tunaandaa mwaka mmoja mmoja, hatuwezi kufikiria kusogea mbele zaidi? Nilishauri hapa tuwe na mipango ya miaka 50, itakuwa na tija ili vitu vyetu tunavyovipanga, vikamilike kwa ukamilifu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hapa dhima yetu inayotuongoza inasema, kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya Taifa. Sasa kama tunazungumza viwanda, hii ni process ya muda mrefu. Naomba Waziri anapokuja, hizi dhima zilizopita huko nyuma, angalau arejee basi kutupa tathmini, walifikia malengo kwa kiwango gani? Ili michango hii tunayoitoa hapa, iwe na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili nalisema kwa utangulizi tu. Tunapotoa mawazo hapa, wakubali kupokea vitu vipya; na hili litatuondoa kwenye hii hali ya watumishi kufanya kazi kwa mazoea. Wakiambiwa nendeni mkaandae mpango, wanarudi kwenye laptop zao, wanabadilisha mwaka na figure pale, wanatuletea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Mheshimiwa Waziri, hebu wakati unapokuja mwaka mwingine, fikirieni namna ya kutuletea mpango wa kutumia watu wetu wenye akili. Mindset za watu tuone, wote tuna akili ndiyo, lakini wapo watu wenye uwezo mkubwa kuliko sisi. Hata huko kwenye Wizara zenu mna watu ambao wana uwezo mkubwa lakini bahati mbaya hatuwatumii kwa sababu hatuna mpango wa kuwatumia hawa watu. Sasa shida tuliyokuwa nayo ndiyo hii tunayokutana na watu ambao kazi yao ni kujaza maboma, yaani yuko pale Wizarani, anatuma taarifa ana-edit, anatuletea. Tuwape watu uwezo wa kufikiri waje na vitu vipya, kama hivi ambavyo nasema tuwe na mipango ambayo itatekelezwa kwa kipindi cha miaka 50, miaka100 na kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze kwa namna ambavyo kwa kweli Wizara ya Kilimo imepokea mawazo yetu na imeanza kufanya kazi. Nimefurahi kuona kwenye mpango huu tumeanza mashamba maalum kwa ajili ya kulima mbegu zetu, nipongeze sana. Nimpongeze pia Waziri wa Kilimo, kwa kweli kwa hili anatupa heshima sana. Wametenga hekta 853 na mchakato uko kwenye tathmini. Sasa nikawa najiuliza, ina maana tangu tumepata uhuru ndio tunaanza kutengeneza mashamba yetu ya mbegu? Basi kwa kuwa tumeanza, niombe sana Mheshimiwa Waziri kwa kweli aongeze speed ili tuwe na mbegu sahihi za kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishauri Bunge lililopita kwamba, hili suala la mbegu lichukuliwe kama suala la

kiusalama kwa sababu, bila mbegu sahihi hatuwezi kufanya kilimo kilicho sahihi na bila kilimo hatuwezi kuongeza uchumi wetu, kwa sababu unapoongeza uzalishaji ndio unakuza pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho kimenishangaza ni kwamba wameanzisha mashamba hizi block farming hapa Dodoma, lakini wameweka changamoto kwamba mashamba yametengwa lakini hakuna maji. Sasa niombe Waziri atakapokuja kuhitimisha atueleze kwamba katika hayo mashamba kuna maji ya uhakika, tuweze kupata kauli yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo pia wamefanya vizuri na ningependa kuchangia. Kwenye umwagiliaji wametenga fedha na kule Hai tunashukuru tumepata miradi mingi ya umwagiliaji. Sasa naendelea kumwomba Mheshimiwa Waziri atazame na pale Metrom tukipata ile tutafanya kazi kubwa sana ya kuinua uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni sambamba na masoko, tumeshaanza vizuri sana kuimarisha kilimo na tumewekeza huko. Hali ya masoko ikoje? sisi pale Hai na soko la Kwa Sadala limeshakuwa sasa ni kila siku nazungumza. Soko hili la Kwa sadala jamani sio tu la Hai, hili litahudumia kanda yote ya kaskazini na ni kama soko la kimataifa. Nilisema hapa ramani tuliyotengeneza siyo ya kawaida tumeweka vitu vingi humo ndani, kuna sorting industry, humo ndani kuna grading, kuna kufungasha. Hebu watutengenezee hela watuletee ili soko lile liweze kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri uwanja wa ndege ule wameshaukubali uwe wa kimkakati wa kilimo. Wameshatuletea fedha za kujenga common use facility pale. Kwa hiyo hili soko likijengwa litatusaidia sana kwenda sambamba na hiki ambacho tunakifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme jambo moja kabla muda haujaisha. Sisi Mlima Kilimanjaro pale ni chanzo cha mapato. Mapato yale yanakusanywa kupitia Serikali Kuu lakini sisi tulioko pale, kama ilivyo maeneo mengine, watu walioko migodini humo wanakusanya service levy, lakini sisi pale hatupati. Niombe sana kwenye eneo hili la mipango Waziri atakapokuja hapa atuambie, kama ambavyo maeneo mengine wananufaika na sisi tunataka tupate walau service levy kutokana na Mlima Kilimanjaro. Hili naomba sana sana Mheshimiwa Waziri atusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo natamani niseme hapa ni kuhusiana na NIDA. Kwenye taarifa NIDA ili waweze kutoa vitambulisho vya utaifa kwa wananchi wetu, wanahitaji bilioni 42.5 ambayo haijapelekwa. Sasa hapa tunapanga mipango mingi na tunatoa maelekezo mengi, mpaka tumesema ile asilimia 10 inayoenda kukopwa na vikundi, wale wanaoingia wanatakiwa wawe na NIDA. Sasa najiuliza, kama hawa hawana fedha hizi za kuweza kutengeneza vitambulisho, hali itakuwaje kwa wale wanaoenda kukopa? Hiki ni kikwazo. Kwa hiyo niombe sana hizi fedha zitafutwe na NIDA wapewe ili Watanzania wote waweze kuwa na vitambulisho vya Utaifa na waweze kupata huduma kama ambavyo tumezungumza hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo linafanana na hili ambalo nilikuwa nazungumza hapa, ni la kuanzisha Tume ya Mipango ya Taifa. Tunapozungumza hapa naona Wabunge wengi wamechangia, tuanze taasisi hii lakini kuwe na watu wenye uwezo, hili ni muhimu sana. Tumekuwa na mazoea tunaanzisha taasisi tunapeana, hapa twende na watu wenye uwezo ili watusaidie yaani kwa maana wenye akili sio tu wenye vyeo ndio namaanisha namna hiyo. Kwa sababu wengi kwenye utumishi wamo lakini wenye akili hawapati nafasi. Shida kwenye taasisi hizi mtu mwenye uwezo anafichwa chini chini. Ninyi ni mashahidi angalieni hata kwenye…

MHE. JANEJELLY J. NTANTE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. JANEJELLY J. NTANTE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba Serikali haiajiri watu wasiyo na akili. Watumishi wote wa Serikali wana akili sawasawa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, unapokea taarifa hiyo?

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa ya mama yangu, wala sina tatizo. Ninachokisema mimi, wote tuna akili siyo tu watumishi wa umma hata sisi wote tuna akili ila tupishana uwezo, ndio ninachokisema. Sasa wale wenye uwezo wapewe nafasi ya kutumika na ukitaka hapa Mawaziri hapa waite Wakurugenzi wao, Wakuu wa Idara, wawanyanganye simu, halafu wawape laptop mpya, waqambie tutengeneze mpango waone tutakachokipata. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna vijana wako kule wadogo ambao hawaonekani kwenye vyeo vyao, ndio wanaofanya kazi, hawa wana vyeo ndio, lakini uwezo wa kueleza humu hawana. Si huwa wanaingia kwenye Kamati, unauliza swali anauliza dogo unasemaje? Ndio anatoa majibu. Sasa tuwape madogo wakalie viti wafanye kazi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naomba kuunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hoja hii. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa afya na uzima. Pia nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanyia Taifa hili. Tumeshuhudia miradi kemkemu imeingia ndani ya Wilaya ya Hai na nchi nzima. Kubwa ni hili la filamu ya Royal Tour ambayo imefanyika. Uzinduzi huu kule kwetu Hai tayari tumeshaanza kuona matunda. Watalii wameongezeka kwa kiwango kikubwa sana. Kwa hiyo, tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri, dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya pamoja na Katibu Mkuu, Dkt. Ndumbaro na watumishi wote kwa ujumla. Mheshimiwa Waziri, kule Hai wanakuita wewe ni mtu bingwa sana. Wanakuita mtu bingwa kwa sababu pale Hai Rundugai tulikuwa na chuo cha ufundi, kilijengwa miaka 11 kikatelekezwa pale. Nilipokuja kwako nikakuomba, umetuletea fedha na kile Chuo cha Rundugai kinajengwa sasa hivi. (Makofi)

Vilevile wewe ni mtu bingwa kwa sababu Kata ya Bondeni kulikuwa hakuna kituo cha afya, wala zahanati. Kupitia TASAF umetuletea fedha pale, tunaenda kujenga zahanati pamoja na vifaa tiba. Nakushukuru sana. Hizi ni sambamba na kumshukuru Mkurugenzi wetu wa TASAF kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya USEMI, tumetembelea Zanzibar, tumetembelea Tanzania Bara huku, tumeona ufanisi (value for money) kwenye miradi. Nazungumza kwenye eneo la miradi, sijazungumza kwenye ile ruzuku wanayotoa kwa wananchi. Kwenye eneo la miradi kwa kweli wanafanya vizuri sana. Kama kuna eneo la kwenda kujifunza, TAMISEMI wanatakiwa waende wajifunze hapa kuona namna ambavyo miradi hii imekuwa sahihi. Hayo makofi unayoyasikia ni ya Wajumbe wenzangu wa USEMI tumeona miradi inavyotekelezwa vizuri na TASAF. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya pongezi hizo, naomba niende moja kwa moja kwenye kuchangia hoja yetu. Nianze kwa kazi kubwa ambayo Mei Mosi watumishi wa Umma nchini wanategemea kusikia jambo moja tu, ongezeko la mishahara. Naomba sana, ninafahamu hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais mwenyewe, lakini nawe Waziri mfanye mfanyavyo, Mei Mosi hii watumishi waongezewe mishahara pamoja na kupandisha kima cha chini. Sababu za kuwaongezea mishahara, wanafanya kazi nzuri. Kwa hiyo, naomba sana hilo kwa kweli mwaka huu tujitahidi ili kazi iweze kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ningependa kushauri kuhusu Muundo wa Utumishi wa Umma wa Mwaka 2002. Nadhani kuna haja ya kufanya marekebisho kwenye maeneo kadhaa. Moja ya eneo hili ni zile sifa zinazomtaka mtumishi kupandishwa cheo. Wako watumishi ambao kwenye kada tofauti wanatakiwa waende shuleni, wakasome na wafaulu ndipo wapandishwe cheo. Wakati kuna kada nyingine hicho kitu hakipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe mfano kwenye kada ya Maafisa Tarafa na Maafisa Tawala, nafahamu zipo na kada nyingine. Ukienda kwenye ule Muundo wa Utumishi wa Mwaka 2002, sifa za kumpandisha Afisa Tawala kutoka Daraja la Kwanza kuwa Mwandamizi, moja ya sifa inayotakiwa, anatakiwa akafanye mtihani unaitwa Qualified Examination Test. Ukisoma kwenye kanuni hii inasema, siyo tu kufanya mtihani, anafanya mtihani halafu afaulu ndiyo apandishwe daraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo hili kwanza linaleta tofauti kwenye Utumishi wa Umma. Kuna kada nyingine hazifanyi, kuna kada nyingine zinafanya. Pia hebu tupime umuhimu wa mitihani hii. Mimi nimefanya huu wa Maafisa Tawala, unaenda pale umetoka kazini; hili linawasumbua sana watumishi wa kada zile. Kwanza Serikali yenyewe haiwalipii kupata hicho kibali cha kwenda kufanya mitihani hii. Ni changamoto kubwa. Kwa hiyo, mtu anaacha kupanda daraja tu kwa sababu hakuruhusiwa kwenda. Pia hana hela ya kwenda kulipia mitihani ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kulipia na kujitahidi kufanya hivyo, akienda darasani, mtu huyo anaenda kusoma vitu vingine tofauti. Mtu amesoma degree ya kwanza, degree ya pili, halafu unampeleka katikati ya utumishi wake, ameshakaa zaidi ya miaka mitano huko mtaani, aende akafanye mitihani ambayo ni administrative law, anatakiwa kwenda kumeza madude pale, ajibu kwenye mtihani na afaulu, lakini lina-embarrass sana watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtumishi anaomba ruhusa kwa Mkuu wake wa Mkoa, anaaga kwamba anaenda kusoma, anafika kule bahati mbaya anafeli, akirudi huku mtaani hapakaliki. Wewe fikiria Afisa Tarafa anaenda kwenye mtihani huo, anaaga Kata zote zinajua bosi kaenda kwenye mtihani. Anaenda kule anakwama, anarudije kufanya kazi? Naomba, kama ni muhimu sana, basi kile kipengele cha kufaulu kifutwe. Waende wafanye kama refreshers course, lakini kusiwe na kigezo kwamba lazima afaulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihamie kwenye eneo lingine kuhusu madeni ya watumishi. Ni kweli Serikali inalipa, lakini bado watumishi wanadai. Mheshimiwa Naibu Waziri, wewe ulikuja kule Hai, uliona wale wamama wanatulilia na kila siku wanatuma jumbe, wanapiga simu. Wamelipwa kiwango kidogo sana. Naomba ifike mahali madeni ya watumishi hawa myamalize. Fanyeni kazi hii mhakikishe tunamaliza, siyo jambo zuri, mtu ameshatutumikia vizuri, amemaliza utumishi wake wa Umma, bado tunaendelea kumsumbua na madeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na pesa yao ya kustaafu, wanazungushwa mno wanapodai. Bahati nzuri na Spika naye amekuwa akilipigia kelele hili. Mtu anakuwa kwenye Utumishi wa Umma, Serikali imetumia fedha nyingi kufanya data cleaning, kwa hiyo tunaamini taarifa za watumishi ziko safi. Sasa anapostaafu unaenda kumdai taarifa, zipi tena wakati unazo wewe? Tayari tuna mifumo ambayo inachukua taarifa zao? Naomba hili na lenyewe tulishughulikie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia mafunzo elekezi; kwenye Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma za Mwaka 2009 zinazungumza mtumishi kabla hajaingia kazini apewe mafunzo elekezi. Naomba Serikali itenge fedha ya kutosha kwenye eneo hili na kazi hii wapewe Chuo cha Utumishi wa Umma. Tunaenda kuwalaumu watumishi kwa sababu hatukuwafundisha vizuri na ni kinyume na sheria ili mtumishi aajiriwe, tuhakikishe lazima aende apate mafunzo ili aingie kazini akijua ni jambo gani anaenda kulifanya. Hili ni pamoja na viongozi wote, hata viongozi wa kuteuliwa ni muhimu sana wakapata haya ili kuepuka mambo ambayo hayafai ya kinidhamu yanaoendelea kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizungumze pia kuhusu e-GA. Nawapongeza sana e-GA. Tulienda kutembelea pale tukaona vijana wa Kitanzania wamechukuliwa kutoka nchi mbalimbali walikokuwa wanasoma, wamekusanywa pale; na wale ambao bado wako mashuleni wanakuja kufanya mafunzo kwa vitendo pale. Kwa kweli hili jambo la kizalendo tunawapongeza sana. Bado naendelea kuwasisitiza, mifumo hii iunganishwe iseme, izungumze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda hapa Dodoma Jiji kulipia kiwanja chako, utakaa hapo masaa mawili au matatu; na wakati mwingine unaambiwa mtandao umeshuka, mtandao sijui umefanya vitu gani. Hii siyo sawa, watafute backup ya kudumu. Tumesema kwenye Kamati lakini narudia humu tena kwamba hii mifumo tunayoitengeneza tuwe na backup ya hakika. Serikali inapoteza pesa nyingi, lakini tunawasumbua wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe mwenyewe ukienda hapo Dodoma Jiji sasa hivi utakuta foleni ya kutosha pale. Jambo hili halifai, Serikali inakosa pesa kwa sababu ya kukosa backup. Kwa kukosa backup inatoa mianya ya watu kuweza kucheza na hii mifumo na kutumia fedha za Serikali. Mfano, mfumo wa GoT-HoMIS ukienda kule umeme ukizimika hawana backup ya kuweza... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu kwa kazi kubwa anayoifanya lakini wananchi wa Jimbo la Hai wameniambia nimshukuru kwa sababu nadhani ni Jimbo pekee nchi hii limetembelewa Na Mheshimiwa Rais mara tano, juzi alikuwa pale kwetu kwa ajili ya kuzindua Royal Tour na alizungumza na wananchi pale tunamshukuru sana na kila akija anatuachia miradi kedekede tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya na mimi pongezi zangu zinaambatana na ahadi yako kwamba magari yanayokuja na pale Hai tutapata gari moja ya Polisi na wewe ni mtu rahimu huwezi kusema uwongo. Pamoja na Naibu Waziri nakupongeza lakini nakupongeza uliniahidi hapa kwamba utatusaidia nyumba za Polisi pale Hai na asubuhi umerudia kuniahidi, kwa hiyo na wewe nakupongeza nikiamini ahadi hiyo utateikeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapongeze pia uongozi wa usalama pale kwetu nikianza na Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ya Hai, Katibu Tawala Dada yangu Ndugu Pendo Wela lakini pia pale kwetu umetuletea OCD mzuri sana anafanyakazi nzuri nakupongeza sana. Baada ya hayo naomba nijielekeze kwenye hoja iliyoko mezani na nianze na Jeshi la Zimamoto.

Mheshimiwa Spika, ukisoma humu kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri utaona namna ambavyo fedha zimepelekwa kwa uchache sana kwenye Jeshi la Zimamoto lakini fedha za maendeleo zimepelekwa kwa asilimia Sifuri (0%) kuanzia Februari mpaka hapa tulipo hii ni hali mbaya sana iliyoko kwenye Jeshi la Zimamoto.

Mheshimiwa Spika, niliwahi kushauri hapa na leo naomba wanielewe, kwamba Jeshi hili la Zimamoto jamani kazi hii imewaelemea tutafute namna nyingine na siyo vibaya tukarudi kule tulipotoka, mwaka 1985 ilikuwa TAMISEMI, Jeshi la Zimamoto kazi ya zimamoto na uokozi ilikuwa inafanywa chini ya TAMISEMI, lakini mwaka 1982 kazi hii ilipelekwa Halmashauri mimi nashauri tuende kule na ninashauri kwa sababu tunaona namna ambavyo Jeshi hili limeelemewa. Hivi tukiuliza wana magari mangapi ya kuzima moto na ndiyo core objective ya kazi yao. Sasa kama ile kazi ya msingi tu vifaa hawana!

Mheshimiwa Spika, pale kwetu Hai tuna watumishi watatu tu, hawana gari hawana kifaa chochote, maskini wa Mungu wamekodishiwa pale kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ndiyo wanakaa pale hawana ofisi, pamoja na kutokuwa na ofisi wameomba pikipiki mbovu pale Halmashauri, tunataka tuwatengenezee hiyo mbovu ndiyo watumie. Yule Afisa anajitahidi anafanyakazi nzuri juzi tumepata tukio la moto pale kwa Sadala, akaenda kufundisha wananchi pale kuzima moto kwa kutumia vumbi! Sasa kweli kwa nini tusikubali kwamba jamani tumeelemewa? Turejeshe Halmashauri ambao wana nguvu waweze kufanyakazi hii.

Mheshimiwa Spika, najua Makamanda pale wananiangalia kwamba baada ya kurudishwa Halmashauri sijui tunaenda wapi! Bado ninyi ni Polisi kuna Majeshi mengine mtaenda huko, lakini ninyi mtafanyakazi ya kuratibu jambo hili.

SPIKA: Mheshimiwa Mafuwe, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Nusrat Hanje.

T A A R I F A

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba anachokizungumza ni sahihi sana na ukizingatia...

SPIKA: Ngoja ngoja, unajua hata mwanzo nilikuvumilia hiyo sentensi siyo kazi yako kujua yeye anasema uwongo ama sahihi, wewe nenda mueleze taarifa kwa sababu ukisema ni sahihi maana yake kuna mtu labda mwingine anazungumza ambayo siyo sahihi. Kwa hiyo wewe nenda mpe taarifa.

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, nashukuru naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba kipindi cha karibuni hapa kumetokea kuungua kwa masoko makubwa kwenye Halmashauri ambazo zina uwezo wa kununua facilities za kwao za kuzima moto. Kwa hiyo ni kitu ambacho ni valid kabisa tunatakiwa Halmashauri zipewe uwezo huo, zipewe mamlaka zinunue zenyewe. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ninaipokea na mimi naomba niendelee.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni kwamba sasa ifike mahali tufanye tu-review tena mfumo huu na wakubali tu wenzetu hawa inawezekana hiki ninachokishauri waende waboreshe zaidi kuona namna ambavyo tunaweza tukawa kweli na jeshi la zimamoto la hakika. Hebu fikiria eneo la Hai ambapo kuna uwanja wa ndege wa Kimataifa hakuna Wilaya ile haina gari, haina hata pikipiki, kwa hiyo ni vema wakapokea ushauri huu.

Mheshimiwa Spika, niende kwenye Jeshi la Polisi wanafanya kazi nzuri, lakini sasa hizi nyumba Mheshimiwa Naibu Waziri aliwahi kunijibu hapa kwamba tukachangishane tuanze ujenzi kule kujenga nyumba za watumishi hii na yenyewe siyo sawa jamani tunachangishana kwenye maboma tunachangishana kwenye kila kitu, kwenye hili mimi niombe Serikali itusaidie. Hai hatuna nyumba tuna watumishi 150 hakuna nyumba mpaka ya mkuu wa kituo wanapata taabu sana kwenye kutekeleza majukumu yao.

Mheshimiwa Spika, pia kwa ujumla kuhusu stahiki za watumishi hawa kwa maana ya Majeshi yote, tuangalie namna ya kuwafanya wawe na mazingira bora Polisi na yeye ni mtu. Mimi naangaliaga mara nyingi sana ukipita barabarani wale ma-traffic wanasimama juani muda mrefu sana lakini wanaenda kujishikiza kwenye magari yao hebu tutafuteni utaratibu, hata kama ni kutengeneza mobile vinyumba ambavyo wanaweza kupeana wakati wanabadilishana shift, mmoja akapumue pale nao watu. Wadada wa watu wanaingia kule Jeshini wakiwa weupe wanatoka weusi kwa sababu ya jua, mimi naomba na wenyewe tuwatazame. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho niombe kwa umahsusi wake…

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa ahsante sana.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)