Answers to Primary Questions by Hon. Mwanaidi Ali Khamis (22 total)
MHE. ALI HASSAN OMAR KING Aliuliza: -
Je, Serikali imefikia hatua gani katika kufuatilia fedha za wananchi zilizopo katika Benki ambazo zimezuiliwa kuendesha shughuli zao hapa nchini?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu tangu niteuliwe kuwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kuchukua nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema kwa kuijaalia nchi yetu amani na utulivu na kutujaalia sisi sote uzima na afya njema.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais wangu, Dkt John Pombe Joseph Magufuli kwa kuniamini na kuniteua katika nafasi hii. Aidha, nitoe shukrani kwa familia yangu kwa kuendelea kunitia moyo hivyo kunipa nguvu na kuendelea kutekeleza majukumu yangu kiufanisi. Vilevile niwashukuru viongozi wangu wa CCM pamoja na UWT kuanzia ngazi ya Mkoa hadi Taifa kwa kuniamini na kunipa nafasi hii kuwa mwakilishi wao hapa Bungeni. Ahsanteni sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo mafupi, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Hassan King, Mbunge wa Jang’ombe, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka 2017 na 2018, Benki Kuu ya Tanzania ilizifutia leseni ya kufanya biashara ya kibenki benki saba kwa mujibu wa vifungu vya 11(3)(i), 41(a), 58(2)(a), na 61(1) vya Sheria ya Mabenki na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006. Benki zilizofutiwa leseni ya kufanya biashara nchini ni pamoja na: FBME Bank Limited; Mbinga Community Bank Plc, Njombe Community Bank Limited, Kagera Farmers’ Cooperative Bank Limited, Meru Community Bank Limited; Efatha Bank Limited; na Covenant Bank for Women (T) Limited.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzifutia leseni benki hizo Benki Kuu ya Tanzania iliteuwa Bodi ya Dhima ya Amana (Deposit Insurance Board) kuwa Mfilisi. Katika kutimiza wajibu wake wa msingi Bodi ya Bima ya Amana ilianza zoezi la kulipa fidia ya bima ya amana ya Sh.1,500,000 kwa waliostahili kulipwa bima ya amana na zoezi hili bado linaendelea kwa wateja ambao hawajajitokeza kuchukua fidia. Sanjari ya zoezi hili DIB inaendelea na zoezi la ufilisi wa benki hizo tajwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwishoni mwa mwezi Desemba 2020, Sh.9,440,305,975.88 zimeshalipwa kwa wateja ambao wenye amana katika Benki sita za Wananchi (Community Banks) kama zilivyotajwa hapo juu ukiiondoa Benki ya FBME. Malipo hayo ni sawa na asilimia 77.27 ya kiasi cha Sh.6,393,690,743.89 zilizotengwa kwa ajili ya kulipa fidia. Aidha, jumla ya wateja waliolipwa ni 21,675 kati ya wateja 57,076 ikiwa ni asilimia 37.98 ya wateja waliokuwa na amana zilizostahili fidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Benki ya FBME, hadi mwishoni mwa mwezi Desemba 2020, jumla ya Sh.2,428,779,092.11 zimelipwa kwa wateja wenye amana ambazo ni sawa na asilimia 52.13 ya kiasi cha Sh.4,659,011,005.76 zilichotengwa. Aidha, jumla ya wateja waliolipwa ni 3,443 kati ya wateja 6,628 ambao ni sawa na asilimia 51.95 ya wateja waliokuwa na amana zinazostahili fidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, wateja waliokuwa na amana inayozidi Sh.1,500,000/= watalipwa kiasi kilichobakia chini ya zoezi la ufilisi ambalo kwa mujibu wa sheria na taratibu za ufilisi kitakacholipwa kitategemea fedha zitakazopatikana kutokana na kuuza mali za benki husika. Zoezi hilo la kukusanya madeni na mali za benki hilo linaendelea ili kupata fedha za kuwalipa wateja wenye amana zenye thamani zaidi ya Sh.1,500,000/=. Ahsante.
MHE. ABUBAKAR D. ASENGA Aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaongeza uwekezaji wa Kiwanda cha Sukari Kilombero ili kunusuru miwa ambayo haijavunwa kwa zaidi ya mwaka mmoja sasa?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abubakari Damian Asenga, Mbunge wa Kilombero, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inaona kuna umuhimu wa kuongeza uzalishaji wa sukari nchini ili kukabiliana na changamoto ya uhaba wa sukari ambao umekuwa ukijitokeza mara kwa mara. Kwa msingi huo, hoja ya kuongeza uwekezaji katika Kiwanda cha Sukari cha Kilombero ni ya msingi sana.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Ofisi ya Msajili wa Hazina imekuwa ikisimamia utendaji kazi wa Kiwanda hiki cha Sukari cha Kilombero kwa ukaribu kama inavyosimamia kampuni nyingine ambazo Serikali ina hisa chache kwa mujibu wa Sheria ya Msajili wa Hazina, Sura 370. Serikali pamoja na Mbia Mwenza (Kilombero Holding Limited) imekuwa kwenye majadiliano ya kina kuhusu kuongeza uzalishaji wa kiwanda hiki kwa kufanya upanuzi wa kiwanda ambapo imekubaliana kupitia gharama za upanuzi wa kiwanda, kufanya upembuzi yakinifu na namna ya ugharamiaji wa mradi. Mara baada ya zoezi hili kukamilika uwekezaji katika kiwanda hiki utafanyika haraka iwezekanavyo. (Makofi)
MHE. DAIMU I. MPAKATE Aliuliza:-
Jimbo la Tunduru Kusini limepakana na nchi ya Msumbiji kwa upande wa Kusini.
Je, ni lini Serikali itafungua Ofisi za Mamlaka ya Mapato (TRA) Lukumbule?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kuwapongeza wananchi wa Jimbo la Tunduru Kusini kwa kutambua umuhimu wa kulipa kodi na hivyo kuhitaji huduma za kikodi zisogezwe karibu yao. Ni dhamira ya Serikali kutumia fursa kama hii kusogeza karibu huduma za kikodi kwa wananchi ili kurahisisha ulipaji na ukusanyaji wa kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) inao utaratibu wa kupitia na kufanya tathmini ya sehemu zote ambazo zinaweza kujengwa ofisi kwa ajili ya kurahisisha ukusanyaji wa kodi.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu huu unazingatia uwiano wa gharama za ukusanyaji wa mapato na kiwango cha kodi kinachotarajiwa kukusanywa pindi ofisi hizo zitakapofunguliwa kutokana na shughuli mbalimbali za kiuchumi katika eneo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na mwenendo wa kukua kwa biashara kati ya Tanzania na Msumbiji, TRA inapenda kuwahakikishia wananchi wa Jimbo la Tunduru Kusini kuwa imelichukua suala hili na italifanyia kazi kwa kutuma timu ya wataalam ili kufanya tathmini ya kina na endapo kiwango cha kodi kinachotarajiwa kukusanywa kitakuwa kikubwa ikilinganishwa na gharama za ukusanyaji wa mapato, ujenzi wa ofisi katika eneo hilo utaanza haraka iwezekanavyo.
MHE. STELLA S. FIYAO Aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuondoa kodi kandamizi kwa wafanyabiashara na kuweka kodi rafiki ili kuwasaidia kufanya biashara kwa uhuru na kulipa kodi kwa wakati na kuondokana na sintofahamu ya wafanyabiashara kukimbilia kufanya biashara nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Simon Fiyao, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kulijulisha Bunge lako tukufu kuwa Serikali ya Awamu ya Tano haitozi kodi kandamizi. Aidha, Serikali imeendelea kuweka mazingira mazuri ya biashara ikiwa ni pamoja na kuongeza vivutio na fursa mbalimbali za uwekezaji kwa wazawa na wawekezaji kutoka nje. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kupitia na kuimarisha mifumo ya kisera, kisheria na kitaasisi kwa kutekeleza Mpango wa Kuboresha Mfumo wa Ufanyaji wa Biashara nchini (Blueprint for Regulatory Reforms to Improve the Business Environment) wenye lengo la kurahisisha mazingira ya kufanya biashara ambapo kupitia Sheria ya Fedha ya mwaka 2019/2020 ilifuta tozo na ada zisizo rafiki 54 zilizokuwa zinatozwa na wakala, taasisi na mamlaka mbalimbali za Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali imekuwa ikifanya maboresho mbalimbali kwenye viwango vya kodi kupitia Sheria ya Fedha (Finance Act) kila mwaka kwa lengo la kuongeza wigo wa ukusanyaji kodi na mapato mengine ya Serikali, kuchochea ukuaji wa biashara ndogo na za kati pamoja na kuhamasisha uzalishaji viwandani na kulinda viwanda vya ndani dhidi ya ushindani kutoka nje.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA Aliuliza:-
Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya michezo ya kubahatisha maarufu kama bonanza kulipiwa kodi ya shilingi laki moja tu kwa mwezi na kutolipa Service Levy kwa Halmashauri?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Musukuma Joseph Kasheku, Mbunge wa Geita, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, michezo ya kubahatisha hapa nchini inasimamiwa na Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania kupitia Sheria ya Michezo ya Kubahatisha, Sura Namba 41 ya mwaka 2003. Sheria hii inatambua kuainisha michezo mbalimbali ya kubahatisha ikiwemo michezo ya slot machines na imeainisha kodi na tozo iliyopaswa kulipwa kwa kuzingatia aina ya mchezo husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, biashara ya michezo ya slot machine, maarufu kwa jina la bonanza, inalipiwa service levy ya asilimia 0.03 ya mapato ya mwaka yanayotokana na michezo hiyo. Tozo hiyo hukusanywa na mamlaka ya Serikali za mitaa. Hivyo basi michezo ya slot machine inalipiwa service levy kwa mujibu wa sheria iliyopo.
MHE. JERRY W. SILAA Aliuliza: -
Je, Serikali haioni haja ya sasa ya kurejesha mfumo wa TANePS Hazina ili ukatekelezwe na kusimamiwa pamoja na GePG katika kuongeza ufanisi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerry William Silaa, Mbunge wa Ukonga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo wa TANePS umetayarishwa na kukidhi matakwa ya sheria ya ununuzi wa umma Sura Na. 410 ambayo imeweka misingi na taratibu za ununuzi wa umma inayohimiza uwazi, usawa na haki katika michakato ya ununuzi ili kuipatia Serikali thamani halisi ya fedha zinazotumika katika ununuzi wa bidhaa na huduma mbalimbali. Aidha, kifungu Na. 9(1) cha Sheria kimeipa nguvu mamlaka ya udhibiti wa ununuzi wa umma kuanzisha na kusimamia mifumo na taratibu zote zinazohusu masuala ya ununuzi wa umma ikiwa ni pamoja na mfumo wa TANePS.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa mfumo wa TANePS tayari umeunganishwa na mifumo ya GPG na taratibu zinaendelea ili kuunganisha na mifumo mingine ya Serikali ikiwemo mifumo ya MUSE na kadhalika.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Ununuzi wa Umma Sura Na. 410 pamoja na Kanuni zake, Serikali inaendelea kuboresha utendaji na mfumo TANePS ili kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa shughuli za ununuzi, hivyo basi haioni haja ya kuhamishia mfumo huo Hazina kwa sasa. Ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO Aliuliza: -
Je, ni lini Serikali itatoa amana na hisa za wateja waliokuwa wamewekeza katika Benki ya Wananchi Meru ambayo ilifungiwa kutoa huduma za kibenki Mwaka 2018?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, mnamo tarehe 4 Januari, 2018 Benki Kuu ya Tanzania iliifutia leseni Benki ya Wananchi wa Meru kutofanya biashara za kibenki kwa mujibu wa vifungu Na. 11(3)(1), 41(a), 58(2) na 61(1) ya Sheria ya mabenki na taasisi ya fedha ya mwaka 2006.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kufuatia leseni benki hizo Benki Kuu ya Tanzania iliiteua Bodi ya Bima ya Amana kwa ufilisi. Katika kutimiza wajibu wake wa msingi kisheria, Bodi ya Bima ya Amana ilianza zoezi la kulipia fidia ya kulipia fidia ya bima ya amana hadi shilingi 1,500,000 kwa wateja waliostahili kulipwa bima ya amana, na zoezi hilo bado linaendelea kwa wateja ambao hawajajitokeza kuchukua fidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia mwisho wa mwezi wa Februari, 2021 jumla ya shilingi bilioni 1.47 zimeshilipwa kwa wateja waliokuwa na amana katika benki hiyo. Malipo hayo ambayo ni sawa na asilimia 78.70 ya kiasi cha shilingi bilioni 1.86 zilizotengwa kwa ajili kulipia fidia. Aidha, jumla ya wateja waliolipwa 4,679 kati ya wateja 13,138, ikiwa ni asilimia 35.61 ya wateja waliokuwa na amana zinazostahili fidia.
Mheshimiwa Naibu Spika, wateja waliokuwa na amana inayozidi shilingi 1,500,000 watalipwa kiasi kilichobaki chini zoezi la ufilisi, ambapo kwa mujibu sheria na taratibu za ufilisi kiasi kitakacholipwa kitategemea fedha zitakazopatika kutokana na kuuza mali za benki husika. Zoezi hili la kukusanya madeni na mali za Benki ya Wananchi Meru ili kupata fedha ya kuwapatia wateja wenye amana zenye thamani ya shilingi 1,500,000 pamoja na wanahisa wa benki hii bado linaendelea. Ahsante.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO aliuliza:-
Je, Serikali inatumia njia gani kuwawezesha wanawake wajasiriamali kupata mafunzo ya ujasiriamali, uandaaji wa maandiko ya miradi na kuwaunganisha na taasisi za kifedha ili wapate mikopo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Husna Juma Sekiboko, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, uwezeshaji wanawake kiuchumi ni suala muhimu katika kufikia usawa wa kijinsia na kupunguza umaskini wa kipato katika jamii. Serikali imeweka kipaumbele katika kuwawezesha wanawake kiuchumi kama mkakati wa kufikia usawa wa kijinsia katika nyanja zote.
Mheshimiwa Spika, Serikali katika kuwezesha wanawake kiuchumi na kuwaunganisha na taasisi za mikopo inaratibu makongamano ya kiuchumi ya wanawake wajasiriamali ambapo kwa kipindi cha kuanzia mwaka 2019/ 2020 hadi sasa Serikali imewezesha makongamano matano (moja katika kila mkoa) katika mikoa mitano (5) ya Arusha, Dodoma, Singida, Ruvuma na Mbeya kati ya makongamano 26 ya mikoa iliyopangwa.
Mheshimiwa Spika, katika makongamano haya elimu ya matumizi ya teknolojia rahisi na sahihi katika uzalishaji, kuanzisha na kujiunga na vikundi vya kiuchumi pamoja na umuhimu wa kuzingatia viwango vya ubora wa bidhaa zinazozalishwa ili kukidhi matakwa ya kisheria na masoko inatolewa. Aidha, makongamano haya yamewafikia takribani jumla ya wanawake 2,768 kati ya 1,500 waliolengwa.
Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushirikiana na SIDO, TBS, TMDA, BRELA na Halmashauri imeendelea kuwajengea uwezo wanawake wajasiriamali hapa nchini katika stadi mbalimbali za ujasiriamali ikiwa ni pamoja na namna ya uboreshaji wa huduma na bidhaa zinazozalishwa na wanawake na uandaaji wa maandiko ya miradi. Katika kipindi cha mwaka 2019/2020 jumla wanawake 3,424 walifikiwa kati ya 5,000 waliolengwa.
MHE. BAKARI HAMAD BAKARI - K.n.y. MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani mahsusi wa kuwapatia Bima ya Afya wanafunzi wa elimu ya juu na wanaosubiri kupata ajira?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. MWANAIDI ALI KHAMISI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Latifa Khamis Juwakali Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za bima ya afya kwa kuongeza kitita cha huduma na upatikanaji wa huduma kwa wanachama kupitia Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya kwa kutekeleza mikakati mbalimbali yenye lengo la kuwawezesha wananchi wengi kujiunga katika mfumo wa bima ya afya na hivyo kuwa na uhakika wa kumudu gharama za matibabu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati inayotekelezwa ni pamoja na utekelezaji wa bima ya afya kwa wanafunzi wa elimu ya juu ambao hujiunga kwa kuchangia na kunufaika na huduma za bima ya afya kwa mwaka mzima. Vilevile kwa wale wanaosubiri kupata ajira, Mfuko wa Maendeleo wa Bima ya Afya una utaratibu wa umeandaa utaratibu wa vifurushi ambavyo vimezingatia uhitaji wa aina ya huduma, umri na ukubwa wa familia kwa kuwapatia wanachama wigo na kuchagua aina ya kifurushi kwa kulinganisha na mahitaji yake.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa kutambua umuhimu wa kila mwananchi kuwa na Bima ya Afya, Serikali inakamilisha rasimu ya muswada wa kutunga Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote ambao utawasilishwa Bungeni mwezi Juni, 2021. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA aliuliza:-
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwakomboa wanawake wanaobebeshwa mzigo mkubwa wa kugharamia matunzo ya watoto bila msaada wa baba?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. MWANAIDI ALI KHAMISI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto naomba kujibu maswali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Viti Maalum kama ifuatavyo:
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kulithibitishia Bunge lako tukufu kuwa Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa wanaotoa wanawake tangu enzi za kupigania uhuru na maendeleo ya nchi kwa ujumla hadi kufikia hapa tulipo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuwakomboa wanawake hawa wanaobebeshwa mimba na kuachwa bila matunzo, Serikali imeandaa Sheria ya Mtoto Namba 21 ya mwaka 2009 ambayo pamoja na masuala mengine inatoa maelezo kuhusu matunzo kwa mtoto kutoka kwa wazazi wote wawili. Sheria hii kupitia kifungu cha 7(1), kifungu cha 8(1)(a) mpaka (g), kifungu cha 8(2) na kifungu cha 9(3)(a) na (b) imetoa maelezo kwa wazazi kuhakikisha kuwa watoto wanapata mafunzo yote ya stahiki ili kuhakikishiwa kuwa haki sawa na ustawi wake vinatimizwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii pia kupitia kifungu cha 44 (a) mpaka (e) na kifungu cha 45(1) pia imetoa maelezo endapo wazazi wa mtoto kama hawaishi pamoja na kama mtoto atakuwa anaishi na mzazi wake wa kike yaani mama, basi mzazi wa kiume atawajibika katika kugharamia malezi ya mtoto kulingana na kipato alichonacho na mazingira anayoishi mtoto husika. Aidha, sheria hii pamoja na kanuni zake imekuwa ni msaada mkubwa katika kuhakikisha kuwa mzigo wa kugharamia malezi ya watoto unawagusa wazazi wa pande zote mbili yaani baba na mama wa mtoto.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe rai kwa wananchi wote kuwa jukumu la kutunza familia ni la lazima watu wote wawili na asitokee mmojawapo kutegea kwa kutotoa matumizi. Nashukuru. (Makofi)
MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza:-
Je, Serikali ina mikakati gani dhidi ya vitendo vya Ukatili vinavyofanywa kwa wanawake na watoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. MWANAIDI ALI KHAMISI) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Swai, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uwepo wa tatizo la ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake na watoto na kuendelea kuchukua hatua mbalimbali za kutokomeza ukatili huo. Moja ya hatua hizo ni pamoja na kuandaa na kusimamia utekelezaji wa Mpango kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto wa mwaka 2017/2018 hadi 2021/2022. Mpango huu wa miaka mitano unalenga kupunguza kiwango cha ukatili dhidi ya wanawake na watoto katika jamii yetu kwa asilimia 50 ifikapo mwaka 2022.
Mheshimiwa Spika, jitihada nyingine ni pamoja na kuanzishwa kwa Kamati 16,343 za Ulinzi na usalama wa wanawake na watoto kwenye ngazi za Mamlaka za Serikali za Mitaa ambazo zina jukumu la kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto. Pia kuanzishwa kwa madawati 420 ya Jinsia na watoto katika vituo mbalimbali vya Polisi nchini ambayo huwezesha wahanga wa ukatili kuripoti aina mbalimbali ya ukatili wa kijinsia.
Mheshimiwa Spika, Serikali pia imewezesha kutungwa kwa Sheria za Msaada wa Kisheria Na.1 ya mwaka 2017. Sheria hii inatoa fursa kwa wanawake waliofanyiwa unyanyasaji au kudhulumiwa kupata haki zao kupitia vyombo vya usimamizi wa sheria.
Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuhakikisha utekelezaji wenye ufanisi wa Mpango kazi wa Taifa wa kutokomeza ukatili, sheria zilizopo pamoja na kuimarisha Kamati za Ulinzi wa Wanawake na Watoto. Ahsante.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO aliuliza: -
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuhamisha Dawati la Kijinsia kutoka Jeshi la Polisi na kwenda kwenye Vituo vya kutolea Huduma za Afya?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Husna Sekiboko, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendeshwa kwa mujibu wa Sheria mbalimbali za Nchi. Jeshi la Polisi limepewa mamlaka kwa mujibu wa Sheria ya Jeshi la Polisi na Polisi Wasaidizi, Fungu Na. 5, Kifungu kidogo cha (322) ya mwaka 1965 na kuboreshwa mwaka 2002 ya kulinda raia na mali zake na kupeleleza makosa mbalimbali. Hivyo, Dawati hilo ni vyema likaendelea kukaa lilipo sasa badala ya kwenye vituo vya kutolea huduma ya afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuhakikisha kuwa waathirika wa vitendo vya ukatili wa kijinsia wanapatiwa huduma rafiki na za haraka, Dawati hili hushirikiana na Vituo vya Mkono kwa Mkono ambavyo viko kwenye Vituo vya Afya vikiwa na Wataalam wa Afya, Maafisa wa Jeshi la Polisi, Ustawi wa Jamii na Wanasheria kwa ajili ya utoaji wa huduma stahiki.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza: -
Je, ni kwa kiasi gani Serikali imewezesha Maafisa Maendeleo ya Jamii ambao wamepewa jukumu kubwa la kuanzisha na kusimamia shughuli za vikundi vya Maendeleo kwenye Halmashauri ili waweze kutimiza majukumu yao ipasavyo?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. MWANAIDI ALI KHAMISI) alijibu: -
Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, Serikali inawezesha Maafisa Maendeleo ya Jamii kupata vitendeakazi kadri Bajeti inavyoruhusu, ambapo hadi sasa imewapatia pikipiki 29 Maafisa wa Maendeleo ya Jamii wa Halmashauri ya Wilaya ya Chamwino Mkoani Dodoma na Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika Mkoani Katavi.
Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI imetoa kanuni za utoaji na usimamizi wa mikopo kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu, marekebisho haya ya mwaka 2021. Kupitia kanuni hii, Maafisa hawa hutengewa fedha kutoka kwenye marejesho kwa ajili ya ufuatiliaji wa mikopo hiyo.
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. BAHATI K. NDINGO aliuliza: -
Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa Vituo Vya Wazee nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -
Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu. Pia namshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum. Napenda kumhakikishia Mheshimiwa Rais kuwa nitafanya kazi kwa uwezo wangu wote na kwa kudra za Mwenyezi Mungu, nitatekeleza majukumu yangu ipasavyo katika kuleta maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bahati Keneth Ndingo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, katika kuboresha utoaji wa huduma, Serikali imeendelea kuboresha majengo na miundombinu ya makazi ya wazee kwa awamu ambapo kwa kipindi cha mwaka wa fedha 2019/2020 na mwaka wa fedha 2020/2021 ukarabati umefanyika katika makazi saba ya wazee ikiwemo; Nunge (Dar es Salaam), Kolandoto (Shinyanga), Njoro (Kilimanjaro), Magugu (Manyara), Kiilima (Kagera), Fungafunga (Morogoro) na Sukamahela (Singida). Aidha, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa Makazi ya Wazee Wasiojiweza nchini kwa kadri ya upatikanaji wa rasilimali fedha zitapopatikana. Ahsante. (Makofi)
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza: -
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwasaidia watoto wa mitaani ambapo kwa siku za hivi karibuni kumekuwa na ongezeko kubwa?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA,WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: alijibu: -
Mheshimiwa Spika; kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum napenda kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwepo na ongezeko la watoto wa mitaani hivi karibuni. Hii inatokana na sababu mbalimbali za kifamilia.
Mheshimiwa Spika, katika kupunguza watoto wa mitaani Serikali inafanya mikakati ifuatayo: -
Kuimarisha Kamati za Ulinzi na Usalama wa Wanawake na Watoto katika ngazi za jamii ambapo hadi sasa kuna jumla ya Kamati 18,186 katika ngazi za taifa, vile vile kutoa elimu kwa wazazi au walezi kuhusu malezi chanya ya watoto kupitia Ajenda ya Taifa ya uwajibikaji wa Wazazi katika malezi ya watoto kwenye familia. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na wadau imekuwa ikifanya zoezi la kuwatambua na kuwaondoa watoto wanaoishi na kufanya kazi mtaani kwa kuwarudisha katika familia zao.
Mheshimiwa Spika, baadhi ya watoto ambao familia zao hazipatikani Serikali imekuwa ikiwapeleka katika makao ya watoto yanayomilikiwa na Serikali na yale yanayomilikiwa na taasisi binafsi, ambako wanapata huduma zote za msingi ikiwa ni pamoja na kuwaandalia mazingira ya kujitegemea kutokana na uwezeshaji wa elimu ya ufundi na mitaji ya kuanzia maisha.
Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa viongozi na jamii kwa jumla kutimiza wajibu wao katika kuimarisha malezi chanya ya watoto katika familia.
MHE. PRISCUS J. TARIMO aliuliza: -
Je, nini mpango wa Serikali kuwasikiliza na kufanyia kazi hoja za wamachinga, hasa baada ya zoezi la kuwapanga?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, Serikali inafanyia kazi hoja za wamachinga, hasa baada ya zoezi la kuwapanga kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ambapo Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya hukukutana nao mara kwa mara kwenye vikao na kujadiliana nao kupitia viongozi wao kwa lengo la kushughulikia hoja na kero zao.
Mheshimiwa Spika, katika ngazi ya Taifa, Serikali inasikiliza hoja zao kupitia viongozi wa Shirikisho la Umoja wa Machinga (SHIUMA) Taifa. Kutokana na vikao vinavyofanyika, Serikali imeweza kuwajengea uwezo katika masuala ya uongozi na utatuzi wa changamoto zao. Pia watendaji wa kata sehemu mbalimbali nchini ikiwemo kwenye masoko wamekuwa na mchango mkubwa katika kuwasikiliza na kufanyia kazi hoja na kero zao kwa kadri zinavyojitokeza. Ahsante.
MHE. NUSRAT S. HANJE aliuliza: -
Je? Serikali ina mkakati gani wa kuzuia ukatali wa kijinsia na utumikishwaji wa watoto katika makambi yanayotarajiwa kujengwa ili kuwezesha ujenzi wa Bomba la Mafuta Hoima Tanga?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Shaaban Hanje, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha vitendo vya ukatili wa kijinsia na utumikishaji wa watoto vinakomeshwa katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo mradi wa bomba la mafuta Hoima Tanga, kupitia MTAKUWWA Wizara yangu imejipanga kuimarisha na kuzijengea uwezo Kamati za Ulinzi na Usalama kwa watoto kwa vile Serikali itaendelea kutumia vyombo vya dola kuhakikisha wale wote wanaotumikisha watoto na kufanya vitendo vya ukatili wanachukuliwa hatua za kisheria. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA K.n.y. MHE. HUSNA J. SEKIBOKO aliuliza: -
Je, kuna athari gani za kijamii kwa watumishi wenza kuishi mbali na watoto wao?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Husna Juma Sekiboko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, familia ni taasisi muhimu sana katika kuleta ustawi kwa jamii na Taifa kwa ujumla. Ni kweli kuwa yapo madhara ya kijamii kwa watumishi wenza kuishi mbali na watoto wao madhara hayo ni kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, kuongezeka kwa vitendo vya ukatili kwa watoto majumbani; kukosa malezi chanya inayopelekea watoto kuathirika kisaikolojia; watoto kutokupata lishe bora inayopelekea udumavu na mmomonyoko wa maadili na kuvunjika kwa ndoa kunakosababisha watoto wa mtaani. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza: -
Je, ni kwa nini Serikali isianzishe madawati ya kijinsia katika ngazi za Kata na Vijiji kutokana na ongezeko la vitendo vya ukatili?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamaii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalumu naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholus Matiko Mbunge wa viti maalumu kama ifuatvyo: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kudhibiti vitendo vya ukatili wa kijinsia katika jamii ambapo imeratibu uanzishwaji wa madawati 420 ya Jinsia katika vituo vya Jeshi la Polisi, na 153 vya Jeshi la Magereza. Aidha, madawati ya ulinzi wa watoto yameanzishwa katika shule za msingi na sekondari. Vile vile, madawati ya jinsia yanaanzishwa kwenye vyuo vyote nchini pamoja na maeneo ya umma kama kwenye masoko. Kwa upande mwingine, kKamati za Ulinzi wa Wanawake na Watoto zimeanzishwa katika ngazi ya mtaa/vijiji hadi Taifa kwa asilimia 88. Madawati haya yanachangia kwa kiasi kikubwa katika kushughulikia masuala ya ukatili wa kijinsia katika jamii. Ahsante
MHE. BENARDETA K. MUSHASHU aliuliza: -
Je, Serikali ina mkakati gani wa kukomesha ukatili wa kijinsia nchini?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamiii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bernadeta Kasabago Mushashu, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili wa Kijinsia unaozingatia kuimarisha uchumi wa kaya, kutokomeza mila na desturi zinachochea ukatili, kuimarisha malezi na makuzi na kusimamia sheria na kuwezesha huduma kwa waathirika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati za Ulinzi wa Wanawake na Watoto zimeundwa kuanzia ngazi ya Taifa hadi Kijiji. Zinafanya kazi zake katika Halmashauri kuhusu kutokomeza ukatili. Vituo vya Jeshi la Polisi, Magereza na Madawati ya Jinsia, Vyuo na Sehemu za Umma wanaunda madawati ya jinsia, Shule za Msingi na Sekondari zinaunda Madawati ya Ulinzi wa Watoto. Vilevile, Kampeni za kupinga ukatili zinaendelea sambamba na hatua za kuboresha sheria mbalimbali, ahsante.
MHE. TAMIMA HAJI ABASS aliuliza: -
Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kutoa elimu kwa jamii dhidi ya udhalilishaji na ukatili wa watoto?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -
Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tamima Haji Abass, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, kupitia mpango kazi wa Taifa wa kutokomeza ukatili kwa wanawake na Watoto, Serikali imeunda Kamati za Ulinzi wa Watoto na kuandaa vijarida na vitini vya kutoa elimu katika jamii kuhusu madhara ya ukatili, vyombo mbalimbali vya habari vinatoa vipindi vya kitaalamu kuhusu haki na ulinzi wa mtoto pia elimu ya athari za ukatili; walimu wa malezi na unasihi wamepata mafunzo ya kutoa elimu ya ulinzi wa watoto kwa walimu wenzao na wanafunzi; pia kupitia viongozi wa kijamii walio sehemu ya kamati ya jamii kwa kushirikiana na maafisa maendeleo, ustawi na elimu wanatumika katika kubadili mitazamo na fikra hasi za jamii, ahsante.
MHE. ESTHER E. MALLEKO aliuliza: -
Je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza wataalam wa saikolojia kwenye jamii ili kutoa huduma za ushauri wa afya ya akili na namna ya kuondokana na msongo?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu: -
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaona umuhimu na inathamini huduma ya msaada wa kisaikolojia na kijamii ambayo inatolewa na wataalam wa saikolojia kwa lengo la kukidhi mahitaji ya mtu kimwili, kihisia, kijamii, kiroho na kiakili katika mazingira anayoishi. Ahsante.