Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Muharami Shabani Mkenge

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Primary Question

MHE. MUHARAMI S. MKENGE aliuliza:- Je, lini Seriikali itafanya ukarabati wa majengo ya magofu ya Bagamoyo ili yasianguke na kuleta madhara?

Supplementary Question 1

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza pamoja na ombi moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali. Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Mji Mkongwe watafanya ukarabati wa lile Jengo la Ngome Kongwe ya Bagamoyo; je, ni lini kazi hiyo itaanza rasmi kufanyika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi. Wananchi wa Kaole na Wazee wa Kaole Bagamoyo wamenituma; wanashukuru sana kwa eneo lao kuwa eneo maarufu kwa utalii wa malikale, lakini ombi lao ni kwamba pale pana msikiti wa miaka mingi, kwa hiyo, wanaomba ule msikiti uhesabike kama misikiti mingine na watalii pamoja na watu wengine watakapokuja wavue viatu ili watakapoingia mle ndani ili kutunza mila na utamaduni wa misikiti katika Mji wa Kaole Bagamoyo. (Makofi)

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali nampongeza sana Mheshimiwa Muharami, Mbunge wa Bagamoyo kwa namna ambavyo anaendelea kutunza historia hususan ya malikale. Pia nawaomba wananchi wa Bagamoyo tuendelee kushirikiana kwa pamoja, kulinda na kuendeleza hizi malikale tulizoachiwa na waasisi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la lini kazi hii itafanyika kwa mashirikiano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, niwaahidi tu wanachi wa Bagamoyo, kwa mwaka wa fedha unaokuja ambapo tayari bajeti tumeshapitishiwa, tutaanza ukarabati wa jengo hili. Kwa hili la msikiti natoa tu maelekezo hapa hapa kwamba Mkurugenzi wa Maliakale ashirikiane na viongozi walioko katika Wilaya ya Bagamoyo kuhakikisha anatoa maelekezo kwamba msikiti huu ni sawa na misikiti mingine na heshima zinazotakiwa kama msikiti watu waingie bila viatu, basi utekelezaji wake uanze mara moja, ahsante. (Makofi)