Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Sophia Mattayo Simba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA M. SIMBA aliuliza:- Hali ya magereza nchini ni mbaya hivyo kufanya vigumu katika utoaji wa haki za kibinadamu licha ya kwamba nchi imekuwa ikijali sana utekelezaji wa mikataba mbalimbali ya kikanda na ya kimataifa katika utoaji wa haki hizo za wafungwa. (a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha hali hiyo katika magereza nchini? (b) Je, Serikali imejenga magereza mapya mangapi katika kipindi cha miaka 20 iliyopita?

Supplementary Question 1

MHE. SOPHIA M. SIMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, na ninamshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri lakini kidogo yananitatanisha.
Mheshimiwa Spika, anazungumzia ujenzi wa magereza 11 katika kipindi cha miaka 20. Speed hii si nzuri, na pia hayo magereza pamoja na kwamba amesema hayajamalizika lakini wanayatumia, nadhani hapo pana hitilafu kubwa.
Ningependa niulize katika hayo magereza yanayojengwa ni lini anafikiri wanaweza wakaboresha ile mahabusu ya watoto iliyopo Upanga Dar es Salaam; ni mahabusu ya miaka mingi na ni ndogo na haifanani kuwa mahabusu ya watoto? Na sidhani kama zipo mahabusu nyingi kama hizo, Waziri wa Ardhi ana viwanja vingi Dar es Salaam ni vyema akaihamisha pale, ni lini watafikiria kuiondoa ile mahabusu pale?
Mheshimiwa Spika, la pili, kumejitokeza msongamano mkubwa sana kwenye mahabusu na magereza, hasa mahabusu pale wanapokamata watu wengi kwa wakati mmoja. Ningependa kujua hivi kule polisi au magereza wana utaratibu gani wanapokamata watu wengi kwa pamoja, wa kuweza kupunguza wengine kwenda maeneo mengine kwasababu pale ndipo kuna gross breach ya human rights, watu wanapumuliana, wale watuhumiwa wanashindwa hata kukaa na wanalala wakiwa wamesimama.
Mheshimiwa Spika, ningependa kujua kuna utaratibu gani kupunguza hilo tatizo kwa sababu ni la muda tu wanakamatwa kwa muda? Ahsante. (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kasi ya kuongeza idadi ya magereza ama kuboresha magereza yaliyopo, naomba tu nichukue fursa hii kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inajitahidi sana kuhakikisha kwamba magereza yetu yanaendelea kuongezeka ukubwa kwa kupanua na kujenga mabweni mapya. Na mfano mzuri wa hilo ni bajeti ya mwaka huu ambayo tumeipitisha hivi karibuni; ambapo tumetenga takribani shilingi bilioni tatu kwa ajili ya kazi hiyo ambayo itahusisha ukarabati mabweni karibu 15 katika maeneo mbalimbali nchini.
Mheshimiwa Spika, baadhi ya maeneo hayo ni kama vile Nzega, Babati, Ushora, Tarime na kadhalika. Lakini pia itahusisha kukamilisha kwa mabweni kama saba ambayo yameshaanza kujengwa ambayo yapo maeneo mbalimbali, likiwemo hilo la Chato, Mpwapwa, Biharamulo, Mkuza, Urambo na kadhalika; pamoja na kuimalisha maeneo ya huduma katika magereza yetu ambapo itahusisha ujenzi wa jiko katika Gereza la Segerea pamoja na mazingira mengine ya magereza yetu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kazi hiyo inafanyika hatua kwa hatua kadri hali ya uchumi utakavyoruhusu na tutaendelea kufanya hivyo katika bajeti ya kila mwaka.
Mheshimiwa Spika, lakini kuhusiana na lile Gereza la Watoto la Upanga ambalo Mheshimiwa Sophia Simba ameliulizia; ni kwamba kimsingi lile lipo chini ya Wizara ya Afya kwenye Idara ya Ustawi wa Jamii. Kwa hiyo, sisi tunachokifanya ni kwamba hatuna magereza ya watoto ukiachia Gereza la Vijana la Wami ambalo lipo Morogoro; linalochukua vijana wa miaka 16 mpaka 21, kimsingi watoto wanopatikana kwenye hatia katika magereza hupelekwa katika Idara ya Ustawi wa Jamii kwa ajili ya kuhudumiwa kama watoto na si wafungwa. Kwa hiyo, kimsingi jibu la swali lake lilikuwa hivyo.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili linahusu kupunguza msongamano magerezani. Kuna njia mbalimbali zimefanyika, ukiachia hizi ambazo tumezungumza za kuona jinsi gani tunapanua mabweni na kujenga magereza mapya pia kuna hatua mbalimbali ambazo zimesaidia kufanikisha kupungua kwa idadi ya wafungwa kutoka 38,000 mpaka sasa hivi takribani 34,000 tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingia madarakani.
Mheshimiwa Spika, hali hiyo ilitokana na hatua mbalimbali ikiwemo kuhakikisha kwamba tunatumia njia za parole, huduma za jamii, probation na njia nyingine ili kuona sasa wafungwa ambao wana kesi ndogo ndogo ama wana hatia ndogo za miaka michache kukaa magerezani basi watumie vifungo vya nje badala ya kurundikana magerezani na kusababisha msongamano usio ulazima. (Makofi)
WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Spika, niseme kwanza nimefurahi kukuona hapo.
Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani kwa majibu mazuri. Ni kweli kwamba mahabusu za watoto ziko chini ya wizara yangu, lakini nataka kumthibitishia mama Sophia Simba kwamba katika mwaka huu wa fedha tumetenga zaidi ya bilioni mbili kwa ajili ya kuboresha kwanza makazi ya wazee lakini pia tutaboresha hizo nyumba za kuwarekebisha tabia watoto. Tunajaribu ku-avoid neno mahabusu kwa sababu tunataka kuwarekebisha tabia, ndilo neno ambalo tunapenda kulitumia.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mama yangu Sophia hatukuwa na mpango wa kulihamisha lakini sasa kabla hatujaboresha naomba nichukue hoja yako tuone kama je, tuboreshe au tulihamishe tulipeleke sehemu nyingine. Nakushukuru sana. (Makofi)

Name

Esther Nicholus Matiko

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA M. SIMBA aliuliza:- Hali ya magereza nchini ni mbaya hivyo kufanya vigumu katika utoaji wa haki za kibinadamu licha ya kwamba nchi imekuwa ikijali sana utekelezaji wa mikataba mbalimbali ya kikanda na ya kimataifa katika utoaji wa haki hizo za wafungwa. (a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha hali hiyo katika magereza nchini? (b) Je, Serikali imejenga magereza mapya mangapi katika kipindi cha miaka 20 iliyopita?

Supplementary Question 2

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, napenda kuuliza swali la nyongeza.
Kwa kuwa magereza mengi nchini ni kweli miundombinu ni michakavu sana; na kwa kuwa asilimia zaidi ya 75 mahabusu waliopo magereza ni wale ambao wana kesi za kudhaminika lakini wananyimwa dhamana. Swali langu linakuja kwamba Gereza la Tarime linachukua mahabusu na wafungwa kutoka Wilaya ya Rorya na unakuta ina msongamano mkubwa kutoka 209 mpaka 560 mpaka 600.
Mheshimiwa Spika, ningependa kujua sasa Serikali ni lini itajenga gereza Rorya, kwa sababu ile ni Wilaya inajitegemea, ili kupunguza msongamano wa mahabusu na wafungwa Tarime ambayo inaweza ikapelekea magonjwa mbalimbali na ukizingatia miundombinu ni mibovu sana? Lakini pia kwa haki za kibinadamu wanatoka kule Rorya kufuatilia kesi Tarime, kuja kuona mahabusu Tarime, kuja kuona wafungwa Tarime. Ni lini sasa mtajenga Gereza la Rorya kupunguza msongamano katika Gereza la Tarime? Ahsante. (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli tunakiri kwamba kuna msongamano wa wafungwa katika Gereza la Rorya na kuna umuhimu mkubwa wa kujenga Gereza pale. Lakini changamoto ya upungufu wa magereza katika Wilaya zetu mbalimbali nchini halipo Rorya tu; kwenye maeneo mengi ya Wilaya nchini bado magereza yamekuwa ni upungufu.
Kwa hiyo tutajaribu kuhakikisha kwamba tunapunguza msongamano huo kwa kujenga magereza katika Wilaya ambazo zina upungufu katika nchi nzima, na utekelezaji wa mpango huo utategemea upatikanaji wa rasilimali fedha, kwani mpaka sasa hivi kati ya Wilaya 92 ni Wilaya 43 nchini ndio ambazo zina magereza.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kimsingi tunalifahamu hili tatizo, niombe tu Mheshimiwa Mbunge awe na subira pale ambapo hali itakapo ruhusu tutashughulikia pamoja na hizo Wilaya nyingine 43 ambazo nimezizungumza zenye mapungufu hayo. (Makofi)