Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Agnesta Lambert Kaiza

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AGNESTA L. KAIZA aliuliza: - Je, Serikali ipo tayari kuruhusu uraia pacha kwa Watanzania wenye uraia wa nchi nyingine?

Supplementary Question 1

MHE. AGNESTA. LAMBERT KAIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa sheria zetu siyo amri ya Mungu na kwa kuwa ndani ya Bunge hili tumekwisha rekebisha sheria mbalimbali. Je, Serikali inapata kigugumizi gani kuleta Muswada wa Marekebisho ya Sheria hii ya Uraia Pacha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa Katiba yetu ya nchi inakataza ubaguzi wa aina yoyote ile. Je, Serikali haioni kuwa kama raia wake ambao wamepata urai nchi nyingine kwamba huu nao ni ubaguzi kwao? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili kwa pamoja ya nyongeza ya Mheshimiwa Agnesta Lambert, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli sheria siyo msahafu na sheria hizi zinatungwa kwa maslahi ya watu, lakini pia zinatungwa kwa matakwa ya watu. Bado Serikali haijajiridhisha kwamba uraia pacha ni takwa la wananchi walio wengi na ndiyo maana hata ukiangalia katika mchakato wa Katiba uliyokwama ambao ulihusisha maoni ya wananchi mbalimbali Serikali ilipendekeza hadhi maalum na siyo uraia pacha. Kwa sababu halikuwa takwa la wananchi waliyo wengi lakini ikitokezea haja hiyo Serikali italiangalia.

Mheshimiwa Spika, sheria hii na hili haina maana kwamba Serikali ina ubaguzi na ndiyo maana tupo katika hatua za mwisho mwisho kuanzisha utaratibu wa kuwa na hadhi maalum kwa ndugu zetu hawa ambao wananchi nje ambao utaweza kuwapa fursa mbalimbali, wataweza kupata fursa nyingi ambazo wenyewe wamependekeza kulingana na maoni waliyotoa. Kuna fursa kama kumi ambazo utaratibu huu utakapokamilika zitaweza kutolewa kwa ndugu zetu hawa Watanzania waliochukua uraia wa nchi nyingine.

Name

Michael Constantino Mwakamo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Primary Question

MHE. AGNESTA L. KAIZA aliuliza: - Je, Serikali ipo tayari kuruhusu uraia pacha kwa Watanzania wenye uraia wa nchi nyingine?

Supplementary Question 2

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa diplomasia ya kiuchumi inafanya watanzania wengi kwenda nchi mbalimbali duniani kutafuta mazingira ya kiuchumi na ili wasibaguliwe kule na wanataka kufaidika na huduma hiyo…

SPIKA: Mheshimiwa swali lako.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kufanya marekebisho ya sheria hizo ili Watanzania hao waweze kufaidika na uchumi wa dunia? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika majibu yangu ya swali la msingi la Mheshimiwa Agnesta, kwamba Serikali imeona juu ya umuhimu wa waliokuwa watanzania hawa waliochukua uraia wa nchi nyingine kuweza kufaidika na fursa mbalimbali hapa nchini. Lakini siyo tu kwa wao kufaidika, hata kutoa michango yao katika uchumi wa nchi yetu na maendeleo ya nchi hii.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nimeeleza kwamba katika kuliona hilo tupo katika hatua za kuweza kuruhusu utaratibu wa hadhi maalum kwa raia hawa ambao wataweza kufaidika na mambo mbalimbali na wataweza kuchangia vilevile katika maendeleo ya nchi yetu. Miongoni mwa fursa hizo ni fursa tatu tu ambazo zitahitaji baadae marekebisho ya sheria na wakati huo utakapofika tutazileta, lakini fursa zingine zote hazihitaji mabadiliko ya kisheria na zitaweza kuruhusika kwa pale ambapo utaratibu huu utakapokuwa umekamilika.