Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Primary Question

MHE. JAPHET N. HASUNGA aliuliza: - Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kutoka Iyula – Ipyana hadi Idunda – Vwawa?

Supplementary Question 1

MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nashukuru sana kwa Serikali kutoa hizo fedha ambazo zimetumika katika hilo eneo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kipande cha Idunda – Soga kuelekea katika eneo la Mbeya Vijijini, Serikali imelima tu lakini haikuweza kuweka changarawe na kujenga kidaraja kidogo katika lile eneo. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inakamilisha hilo eneo ili liwe linapitika wakati wote wa mwaka?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa ili wananchi wa Idunda, Ipyana waweze kusafiri hadi Iyula hadi kuelekea Makao Makuu ya Jimbo la Vwawa ni lazima kipande cha Iyula – Hatete – Mbewe kikamilike ambacho mpaka sasa hivi bado hakijakamilika.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inakamilisha kipande hicho ili kuwasaidia wananchi hao waweze kusafiri kiurahisi? (Makofi)

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali lake la kwanza la kipande cha Idunda – Soga ili kiweze kujengwa kuwa changarawe na kuna daraja ambalo Mheshimiwa Hasunga amelitaja lina changamoto. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 TARURA katika Wilaya ya Songwe, Halmashauri ya Songwe DC ilikuwa imetengewa shilingi milioni 650 tu, lakini katika mwaka wa fedha 2021/2022 na huu tunaokwenda wametengewa zaidi ya shilingi bilioni 2.8 kwa ajili ya utekelezaji wa barabara. Hivyo basi, nichukue nafasi hii kumuelekeza Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Songwe kuhakikisha wanafika kwenye barabara hii na kuona changamoto ambayo ipo ili waweze kutengeneza daraja hili ambalo amelitaja Mheshimiwa Hasunga la kuunganisha wananchi kati ya Songwe na Mbeya.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la wananchi wa Igana kupita barabara ya Iyula - Katete na Mbewe. Nirejee tena yale maelekezo ambayo nilikuwa nimeyatoa kwenye swali lake la kwanza, Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Songwe anapotembelea barabara hii ya Idunda – Soga ahakikishe anaangalia nini kimekwamisha barabara hii ambayo nimetoka kuitaja hivi sasa na kuweka mikakati ya kuweka changarawe na kuimalizia.