Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RITTA E. KABATI aliuliza:- (a) Je, ni lini askari wa Iringa watajengewa nyumba? (b) Je, ni kiasi gani cha fedha wanachodai askari wa Mkoa wa Iringa posho na stahiki zao zingine?

Supplementary Question 1

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nina maswali tu madogo mawili ya nyongeza.
Pamoja na askari wa Iringa kuishi kwenye mazingira magumu sana, lakini zaidi ya nusu ya askari wanaishi nje ya makambi yao yaani uraiani. Pia katika Mkoa huo wa Iringa, Wilaya ya Kilolo Serikali haijaweza hata kujenga jengo lolote la ofisi wala makazi ya askari na katika majibu yake Serikali imesema kwamba itakuwa inajenga kadri itakavyokuwa inapata fedha.
Je, Serikali ipo tayari sasa kutoa kipaumbele kwa Mkoa wetu wa Iringa ili askari wetu waweze kuishi kwenye mazingira bora yajengwe mapema sana? (Makofi)
Swali la pili, kwa kuwa askari wa Mkoa wa Iringa wanadai posho na stahiki zao kiasi kikubwa sana cha pesa na Serikali imesema kwamba bado wanafanya uhakiki. Je, ni lini sasa uhakiki utakamilika ili askari wetu wa Mkoa wa Iringa waweze kupata stahiki zao na posho kwa sababu familia zoa zimekuwa zikiishi kwa shida sana na hasa watoto na wake za askari? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, wakati tunakamilisha mchakato wa ujenzi wa nyumba za askari ule ambao nimekuwa nikiuzungumza hapa Bungeni kila siku ambao pia utahusisha na Mkoa wa Iringa tunajipanga kutumia rasilimali za ndani pamoja na rasilimali zilizopo katika maeneo husika pamoja na rasilimali watu ili kupunguza tatizo au changamoto za makazi kwa askari wetu na vituo vya polisi.
Mheshimiwa Spika, nataka nichukue fursa hii kwanza kabisa na kwa dhati nimpongeze Mheshimiwa Ritta Kabati kwa jitihada zake kubwa sana ikiwemo ujenzi wa Kituo cha Polisi Iringa, ambapo sasa hivi nguvu zake anazielekeza maeneo ya Kilolo, lakini kwa kutambua kwamba Mheshimiwa Mbunge amefanya kazi kubwa sana pale Iringa ya ujenzi wa kituo nataka nimhakikishie kwamba tutakuwa pamoja na yeye tutashirikiana naye ili tuweze kuona kwa haraka sana tutatumia mpango huu wa matumizi ya rasilimali katika eneo husika ili kupunguza changamoto ya makazi pamoja na vituo vya polisi.
Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge baada ya kikao hiki cha Bunge tukae kwa pamoja tushauriane tuone iko vipi kwa haraka sana mpango huu ambao tumeubuni hivi karibuni tunaanza kutekekeleza kwa Kilolo.
Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusiana na lini ukaguzi utamalizika. Naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya kila linalowezekana kuhakikisha kwamba tunakamilisha ukaguzi haraka iwezekanavyo ili malipo haya yaweze kulipwa.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu na nimpongeze sana niongezee tu kwa kumpa assurance Mheshimiwa Mbunge ambaye jambo hili amekuwa akilifuatilia kwa umakini sana la maisha ya polisi na vitendea kazi vyao kwamba tarehe 9 Septemba, 2016 wale wenzetu ambao tulikuwa tunaongea nao kuhusu mkataba wa ujenzi wa nyumba za askari kiongozi wao mkubwa atakuja na atakutana na IGP pamoja na Katibu Mkuu wa Wizara na baada ya hapo tutabakiza mawasiliano ya ndani ya Serikali kwa ajili ya kwenda kwenye utekelezaji wa jambo hilo.
Mheshimiwa Spika, la pili Wizara tumeamua kwenda na jambo hili sambamba kwamba jitihada zitakazofanyika za kibajeti tuzioanishe na jitihada za rasilimali tulizonazo ndani ya taasisi zetu hizi na nimeelekeza mikoa yote wafanye tathmini ya kila mkoa tuna wafungwa wangapi wanaoweza kufanya kazi za kufyatua tofali na wafanye tathmini ya vitendea kazi vinavyoweza kutumika kufyatulia tofali hizo na aina ya tofali ambazo zinatakiwa, lakini pia na kutumia bajeti kidogo zilizopo kwa ajili ya vitendea kazi vingine ambavyo vitatakiwa kama cement ama nondo kwa ajili ya kuanza miradi hiyo katika maeneo ambayo kazi hiyo si kubwa sana kwa ajili ya kupunguza tatizo hili sambamba na jitihada za kibajeti ambazo tunazifanya.
Kwa hiyo, Serikali inatambua ukubwa wa tatizo hili na inaweka uzito unaostahili na Mheshimiwa Rais tayari alishatuelekeza wasaidizi wake na sisi tunatembea kwenye nyayo zake kuhakikisha tunamaliza tatizo hilo la manung‟uniko ya askari.
Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo kwenye upande wa madai yao nimeelekeza kila ambaye anatunza kumbukumbu za askari waweze kuhakikisha kwamba wanaorodhesha vizuri kuwarahisishia wale wanaokagua, wanaofanya ukaguzi ili madai hayo ya askari yasikae muda mrefu sawasawa na maeneo mengine ambayo yana uficho ama yana tatizo la kuweza kufanya ukaguzi kwa sababu askari anapokuwa kazini huku anadai inampunguzia morali ya kazi na inampunguzia uwezo wake wa kufanya kazi.