Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SUBIRA K. MGALU aliuliza: - Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya uendeshaji wa Mabaraza ya Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi?

Supplementary Question 1

MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza naishukuru Serikali kwa majibu mazuri ambayo imeonesha kwa mara ya kwanza Serikali yetu imetenga pesa kwa ajili ya kuwezesha majukwaa haya.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mkoa wa Pwani unaongoza nchi nzima wa kusajili majukwaa 1,723 na kuyasajili 945 ambayo yamepelekea kuanzisha kampuni ya Go Mama Public Company Limited. Je, Serikali ipo tayari kutumia Milioni 200 zinazotengwa mwaka huu wa Fedha kwa ajili ya kuwezesha Mkoa wa Pwani kwa kuwa umeonesha dira umeanzisha kampuni ambayo inayo matarajio ya kujenga kiwanda cha vifungashio?

Swali la pili, kwa kuwa Serikali ina Mifuko mingi ya Uwezeshaji zaidi ya 72 ambayo ipo katika Wizara tofauti tofauti. Je, Serikali haioni ipo haja ya Mifuko hii kuwa chini ya chombo kimoja ili iwe fursa kwa majukwaa haya ya uwezeshaji badala ya majukwaa haya kutegemea asilimia 10 ya mikopo ya mapato ya ndani ya Halmashauri. Ahsante sana.

Name

Exaud Silaoneka Kigahe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nashukuru na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Subira Khamis Mgalu, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Subira kwa kazi kubwa anayoifanya katika Mkoa wa Pwani kama ambavyo wamesema wameanzisha hiyo kampuni ya Go Mama ambayo wanasema ina nia ya kuanzisha kiwanda cha vifungashio ambayo italeta pato kubwa sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema Serikali imeendelea na itaendelea kusaidia na kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia fursa mbalimbali ikiwemo Mifuko hii ya kuwezesha wananchi kiuchumi. Kwa hiyo, kwa kazi hiyo wanayoifanya naamini tutaangalia katika bajeti hii ili tuone namna gani mahsusi kusaidia kampuni hii ambayo inaenda kusaidia kujenga viwanda katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili tayari Serikali tumeshaanza utaratibu wa kuunganisha Mifuko hii ambayo mingi ipo ndani ya Serikali katika Wizara mbalimbali, pia mingine kutoka sekta binafsi, kwa hiyo tunaifanyia kazi, naamini katika mwaka wa fedha ujao tutafanya hivyo ili kuhakikisha Mifuko hii inakuwa na tija kwa ajili ya kuwasaidia wanawake kiuchumi. Nashukuru. (Makofi)