Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Dorothy George Kilave

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Temeke

Primary Question

MHE. DOROTHY G. KILAVE aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kupunguza gharama za malipo kwa Akinamama wanaojifungua kawaida na wale wa operesheni?

Supplementary Question 1

MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini nilitaka kujua ni mpango upi wa kupunguza kabisa gharama hasa za mama mjamzito anapojifungua kwa operesheni, ambapo Temeke tunalipa laki mbili kwa operesheni na Vituo vya Afya ni shilingi laki moja; je, mpango huo ukoje wa kupunguza kabisa gharama hii?

Swali la pili; je, kuna mkakakti gani wa kufanya ili sasa Serikali itoe vifaa vile ambavyo akina mama tunapokwenda kujifungua tunaambiwa tununue pamba viwembe vile na kadhalika.

Je, Serikali ina mpango mkakati gani sasa wa kuweka vile vifaa ndani ya hospitali zote ili tusiweze kununua. (Makofi)

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninampongeza kwa jinsi ambavyo anafuatilia masuala haya kwa ukaribu kwenye Jimbo lake. Niseme tu kwamba suala ni la kisera kwamba mama mjamzito na watoto chini ya miaka mitano hawatakiwi kulipishwa. Ninaomba Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa tuweze kushirikiana pamoja kusimamia hili takwa la kisera.

Mheshimiwa Naibu Spika, Dar es salaam kwa kweli nilitembea kwenye baadhi ya vituo vya afya na hospitali za Wilaya nilichogundua ni kwamba, unaweza ukakuta Kituo cha Afya kinapata wagonjwa wengi kuliko hata baadhi ya hospitali za Wilaya. Kwa hiyo, wakati mwingine mgao wanaoupata MSD unakuwa mdogo kiasi kwamba wanaishiwa mapema kulingana na idadi ya watu, hata kwa mwaka ni zaidi ya 160,000 watoto wanazaliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni nini? Kwamba mgao wanaoupata MSD ni mdogo ukilinganisha na idadi ya watu, kwa hiyo tutakwenda sisi kama MSD kufanya kuhakikisha inatolewa mgao wa dawa na vifaa kulingana na idadi ya watu na siyo kuangalia kituo, aidha ni kituo cha afya au na ku-generalize.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu mkakati ndiyo huo, kwamba tukiweza kwa Dar es Salaam ambapo unakuta kituo cha afya kinapata wagonjwa kuliko hata baadhi ya Hospitali za Wilaya sehemu nyingine, tukienda kuwapa vifaa kulingana na idadi ya wagonjwa badala ya kuangalia ni status gani hospitali inayo, maana yake hawatakuwa tena na huo upungufu na pale MSD zimenunuliwa kit za kutosha kwa ajili ya akina mama kujifungua. Hivyo hilo tatizo litaenda kuisha, nafikiri shida kwako ni idadi ya watu kwa hiyo kinachopelekwa kinakuwa kidogo sana. (Makofi)