Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Najma Murtaza Giga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA aliuliza: - Je, nini Sababu ya kukosekana uwiano wa jinsia ya kike kwenye nafasi za uteuzi na ajira nchini?

Supplementary Question 1

MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, na nimpongeze sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu wa kulipa kipaumbele suala la jinsia katika ajira katika kipindi chake.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwamba, kwa mujibu wa Ibara ya 22 na 23 ya katibu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haki ya usawa wa ajira na ujira ni ya raia wote wa nchi yetu kwa shughuli yoyote inayosimamiwa na mamlaka yetu ya nchi.

Sasa, je, Mheshimiwa Waziri kwa nini hamuoni jambo la busara kwenda kumshauri Mheshimiwa Rais ili sasa Serikali ije ilete sheria ili hizo kanuni zenu na miongozo iingie humo iwe sheria, ili yoyote yule ambaye atakiuka sheria hiyo aweze kuadhibiwa?

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA. Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wote humu ni mashahidi, Mheshimiwa Rais wetu wa awamu ya sita Mama yetu Samia Suluhu Hassan ameonesha nia ya dhati ya kuweza kuleta uwiano sawa katika nafasi za uteuzi. Lakini vilevile sisi kama Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kama nilivyosema awali kwenye majibu yangu ya msingi, tumeanza kuweka miongozo, tunaandaa namna ya kuweza kupata usawa katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano, miongozo ya Sekretarieti ya Ajira inasema wazi pale endapo candidate wawili watagongana maksi na mmoja ni mwanamke, basi atachuliwa yule mwanamke katika kuingia katika ajira ya Utumishi wa Umma. Miongozo hii ipo na tutaendelea kuisimamia na kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini niwatoe mashaka, Mheshimiwa Rais ameweza kutafuta fedha kutoka European Union, Serikali ya Finland na Serikali yetu ya Tanzania vilevile imewekeza fedha katika Chuo kile cha Uongozi Institute; ambapo sasa tunaenda kutoa mafunzo ya uongozi kwa wanawake zaidi ya 500. Na hivi ninavyozungumza tayari kuna wanawake 50 ambao wapo katika mafunzo ya uongozi kwenye Taasisi yetu ya Uongozi Institute. Watakapo maliza wao wanakuja tena wanawake mia 100 katika mwaka huu wa fedha kwa ajili ya kuweza kupata mafunzo ya uongozi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imejipanga vyema katika kuhakikisha wanawake wanapata fursa sawa katika uteuzi na ajira nchini. Naomba kuwasilisha.