Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rehema Juma Migilla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Primary Question

MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza: - Je, kuna mpango gani wa kuwapatia warithi wa mstaafu asilimia 67 ya michango yake pindi anapofariki?

Supplementary Question 1

MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu hayo, nina maswali madogo mawili ya nyongeza. Kulingana na majibu ya Serikali, inaonesha kwamba mafao yanayolipwa hayazingatii asilimia ya michango isipokuwa wastaafu na wategemezi hulipwa kulingana na michango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza, je, kwa mujibu wa sheria ambayo imepitishwa hivi karibuni mwaka 2022, inasema mstaafu atalipwa asilimia 33 katika mafao yake kama pensheni yake ya mkupuo; kama analipwa asilimia 33 ina maana kwenye asilimia 100 inabaki asilimia 67 kwa ajili ya pensheni limbikizi; sasa kwa mujibu wa majibu haya, kwanini hawa wastaafu pindi anapofariki, ile asilimia 67 iliyobakia kama pensheni limbikizi wasilipwe wategemezi wake au warithi wake pindi ambapo tunajua kabisa kwamba huyu mtumishi kipindi chote cha utumishi wake ame- contribute kwenye mfuko fully? Kwanini wasilipwe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; tunaona kwamba sasa hivi kuna mfumuko wa bei, maisha yamepanda sana, lakini wastaafu waliostaafu kuanzia miaka ya 2000 na kurudi nyuma pensheni yao ni ndogo sana; ile monthly pension, Serikali haioni sababu au umuhimu wa kuongeza pensheni kwa hawa watu ambao pensheni yao haikui? Ahsante. (Makofi)

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kumjibu dada yangu, Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, maswali yake mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi, ni kwamba malipo ya mafao yanazingatia kanuni. Mstaafu anapostaafu, kama alivyoeleza, analipwa mafao ya mkupuo na kunakuwa na wastani wa umri wa kuishi. Sasa kwenye majibu ya msingi kama nilivyoeleza, anapofariki haijilishi kama alishavuka ule wastani wa umri wa kuishi au hajavuka, lakini analipwa ile miaka mitatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kiasi ambacho anakisema cha asilimia 67 kinawekwa kama makisio, lakini mstaafu analipwa kwa kadri anavyoendelea kuishi, anaendelea kupata pensheni ya mwezi. Kwa hiyo, sasa hivi tunalipa kwa miaka mitatu anapofariki bila kujali kama alikuwa ameshazidi ule umri wa wastani wa kuishi baada ya kustaafu.

Mhelshimiwa Mwenyekiti, swali la pili la Mheshimiwa Migilla kwa kweli ni la msingi la kuhusu Serikali kuangalia uwezekano wa kuongeza mafao kwa wastaafu. Utaratibu wa mifuko ni kwamba inafanya tathmini (actuarial evaluation) na kulingana na ile tathmini ndivyo ambavyo inaweza ikaangalia uhimilivu na uendelevu kuwaongeza wastaafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepanga kufanya tathmini ya mifuko katika mwaka fedha 2022/2023 na baada ya tathmini hiyo ndiyo tutaona uwezekano wa kuongeza kulingana na uwezo wa mifuko yetu.