Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Michael Mwita Kembaki

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Mjini

Primary Question

MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y. MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: - Je, ni lini Serikali itaanza kuharakisha utoaji wa matokeo ya tafiti za ndani za tiba asilia za kutibu maradhi mbalimbali kama inavyofanya kwenye tafiti za nje ya nchi kwa kuziundia Tume ya Jopo la Wachunguzi mapema?

Supplementary Question 1

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nimshukuru na nimpongeze Waziri kwa majibu yake mazuri ambayo yametolewa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asilimia 45 ya Watanzania wanatumia tiba asili. Tunashuhudia waganga wa tiba asili wakiwapa watumiaji kwa vifungashio ambavyo siyo salama. Vilevile tunaona wanatumia vikombe kupima dawa na mengine ambayo sijayataja. Ningependa kujua, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba dawa wananchi wanazotumia ni salama na vilevile zinasajiliwa kwa ajili ya matumizi sahihi ya wananchi? (Makofi)

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nijibu swali la Mheshimiwa Kembaki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, alichojaribu kusema ni kwamba asilimia 45 ya Watanzania wanatumia hizi dawa za asili ambayo ni kweli. Pia anajaribu kuonesha kwamba wakati mwingine zinafungwa kwenye vifungashio ambavyo siyo salama. Anataka kujua tunafanyaje ili kuhakikisha sasa hizi dawa zinaweza kuwafikia Watanzania zikiwa salama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tuna taasisi yetu ya Mkemia Mkuu wa Serikali ambayo kazi yake moja kwa moja ni kwa ajili ya kupima usalama wa dawa hizo; lakini kuwapa maelekezo ni namna gani wanaweza wakazipaki na kufikisha kwa wananchi zikiwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakiri ukweli kwamba kwa kipindi hiki cha corona kumekuwa na dawa mbalimbali na mambo mengi ambayo yanaleta shida. Hata hivyo, Rais wetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kama nilivyosema nyuma hapa, alishatoa shilingi bilioni 1.2; na leo nimetoka ofisini, imeenda tena shilingi bilioni 1.2, kwa maana ya shilingi bilioni 2.4 kwenye eneo hili la tiba asili kwa ajili ya kwenda kujenga uwezo kwa hawa watu wetu wazalishaji wa tiba ya asili, lakini kujengea taasisi zetu uwezo wa kuangalia hizo tiba asili zinazotolewa.

Je, zina hivyo vitu ambavyo vinaweza kutibu ugonjwa wenyewe unaosemekana? Pia itaenda kununua mashine za kupima na mambo mengine ya kusaidia utafiti na kupima usalama wa dawa hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali imejiwekeza kwenye hilo. Majibu mengine kutokana na hii shilingi bilioni 1.2 ambayo imetoka leo, nayo tutawaletea majibu yake kwa sababu tunaenda kuangalia dawa nyingine 56 ambazo zilikuwa zinatumika wakati huu wa corona. Ahsante sana. (Makofi)

Name

Humphrey Herson Polepole

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Primary Question

MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y. MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: - Je, ni lini Serikali itaanza kuharakisha utoaji wa matokeo ya tafiti za ndani za tiba asilia za kutibu maradhi mbalimbali kama inavyofanya kwenye tafiti za nje ya nchi kwa kuziundia Tume ya Jopo la Wachunguzi mapema?

Supplementary Question 2

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nchi za Uingereza, Denmark, Sweden na Norway zimeamua kuachana kabisa na masharti kichefuchefu dhidi ya ugonjwa wa Corona; na kuamua kuishi na ugonjwa wa Corona kama magonjwa mengine. Nini kauli ya Serikali kuhusu mwelekeo huu mpya Kimataifa? Ahsante. (Makofi)

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli ya Serikali, ninachokiona ni kwamba Sweden na nchi zilizotajwa zimeamua kusimama kwenye msimamo wa Tanzania toka mwanzo. Kauli ya Tanzania ni moja tu kwamba sisi kama Tanzania tutaendelea kuhakikisha tunakuwa makini katika kufuata zile taratibu zote ambazo WHO wamezielekeza. Pia tutaendelea kufuata zile taratibu ambazo ni local, zinazotokana na watu wetu na nchi yetu ambazo tulishazifuata toka mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo tutaendelea kulinda mipaka yetu na kuwapima watu wanaoingia na wanaotoka kuhakikisha watu wetu ndani ni salama. Pia tuwahakikishie usalama wenzetu waliopo huko duniani wakija kwetu, nasi tukienda kwao ili tuweze kuitengeneza dunia salama kwa kufanya kazi kwa pamoja. Kwa sababu tukiwa wote salama, wote tutakuwa salama; mmoja asipokuwa salama, wote hatutakuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, lakini niseme, dunia siku moja itafika mahali ikubali mwelekeo wa Tanzania toka mwanzo ulikuwa ni sahihi. Ahsante sana. (Makofi)

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y. MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: - Je, ni lini Serikali itaanza kuharakisha utoaji wa matokeo ya tafiti za ndani za tiba asilia za kutibu maradhi mbalimbali kama inavyofanya kwenye tafiti za nje ya nchi kwa kuziundia Tume ya Jopo la Wachunguzi mapema?

Supplementary Question 3

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Madawa ya asilia ni kweli kama Watanzania tulikuwa tunayatumia siku za nyuma mpaka sasa. Ila kwa sasa kumekuwa na matangazo mengi sana kwenye vyombo vya habari, wakielezea kwamba wanatibu magonjwa sugu ya figo na magonjwa mengineyo ambayo ni hatarishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina kauli gani ya kukataza matangazo hayo kwa kuwa hayana tafiti sahihi kwa wananchi na wamepoteza fedha nyingi sana kwa kununua dawa hizo na zisitibu chochote? Tunaomba kauli ya Serikali kwa watu kama hao. (Makofi)

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nampongeza kwa swali lake zuri, kweli kwamba kumekuwa na matangazo hayo. Ila ukisikia Serikali na Taasisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali na TMDA tena inapunguziwa kazi; na hata Wizara ya Afya kwa kutumia wadau wengine, kwa kweli lengo ni moja kusaidia hawa watu ambao ni wabunifu wetu wanaohangaika huku na huku kutafuta ufumbuzi wa matatizo mbalimbali hawakatishwi tamaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuhakikisha tunawadhibiti ili wasiweze kufanya kitu ambacho kinaweza kikapelekea madhara kwa watu; na ndiyo maana leo kwenye Wizara ya Afya kuna Kurugenzi ya Tiba Asili. Moja ya kazi yake, pamoja na ku-facilitate waweze kuzalisha hiki wanachokifiki, lakini ni kuwa-control kuhakikisha wanachokifanya mwisho wa siku hakiwi holela. Tutakwenda kuongeza nguvu hapo kama Mheshimiwa Mbunge alivyoshauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge ukienda Wilaya ya Meru, najua kuna watu wasiokuwa na uelewa walivuruga. Kuna Hospitali ilikuwa inaitwa MOMELA ilikuwa unapimwa vipimo vingine vyote vya kidaktari; unapimwa Ultra-Sound, unapimwa damu kama kawaida, lakini ukifika duka la dawa, unapata dawa za tiba za asili. Tunataka tufike hapo, kwamba ifike mahali tuna dawa ambazo tunajua zinatibu ugonjwa, tuna dawa za kisasa na tiba asili. Vilevile uweze kufuata taratibu zote za kuhakikisha usalama. Huko ndiko tunakoelekea.

Mheshiiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunachukua wazo lako na tunaongeza nguvu kwenye eneo hilo. (Makofi)