Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Agnesta Lambert Kaiza

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AGNESTA L. KAIZA aliuliza: - Je, Serikali haioni umuhimu wa kukutana na Wafanyabiashara na kutafuta namna bora ya kuwa na utaratibu wa ukadiriaji kodi wenye usawa na unaozingatia mabadiliko ya biashara ili kulinda mitaji ya wafanyabiashara wa ndani?

Supplementary Question 1

MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Wafanyabiashara wengi wenye mitaji midogo hawana elimu ya kutosha kuhusiana na suala zima la kufanya makadirio yao wenyewe ya kulipa kodi. Jambo hili limepelekea wafanyabiashara hawa mara nyingi kuajiri wataalam wa kuja kuwasaidia jambo ambalo hupelekea wao kutozwa fedha nyingi kuanzia shilingi laki tano, milioni moja na kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili limekuwa ni changamoto sana kwa wafanyabiashara na mwisho wa siku wafanyabiashara wengi wameshindwa kuendelea na biashara kwa maana wamekata tamaa kwa kuwa mwisho wa siku wanajikuta hawapati chochote, kila wanachokifanya kinaishia katika kulipa wataalam.

Je, Serikali ina mpango gani madhubuti wa kutoa elimu sahihi kwa wafanyabiashara hawa hususan wafanyabiashara wa vijijini ambao kimsingi elimu kwao haipo kabisa? Naomba majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wafanyabiashara hawa wenye mitaji midogo walikuwa wamewekewa utaratibu maalum wa makadirio ya shilingi 20,000/= kwa mwaka, lakini mpaka sasa ninapoongea utaratibu huu upo kimya kabisa, ni kama haupo: Je, Serikali ina kauli gani kuhusiana na utaratibu huu ambao upo kimya kwa wafanyabiashara hawa ikiwa ni sambamba na kwa wafanyabiashara wenye maduka siyo tu kwa machinga. Ahsante sana. (Makofi)

Name

Hamad Hassan Chande

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kojani

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza naomba nimpongeze sana ndugu yangu Mheshimiwa Agnesta kwa namna anavyotetea Wafanyabiashara wadogo nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la taaluma, Serikali kupitia Mamlaka ya Mapato Tanzania imekuwa na utaratibu wa kutoa elimu kwa wafanyabiashara wadogo wadogo na hata wakubwa kupitia runinga, redio, na matamasha. Inawezekana baadhi ya vijiji elimu hiyo haijawafikia. Tutachukua ushauri huu kushuka chini vijijini kabisa kwa ajili ya kupeleka elimu ya kulipa kodi hasa kwa hiari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili; kuhusu utaratibu wa wafanyabiashara wadogo kulipa ada ya shilingi 20,000/= kwa mwaka bado upo na unaendelea kwa wale wafanyabiashara wadogo wadogo kupitia vitambulisho vya Machinga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)