Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mariamu Nassoro Kisangi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Wilaya mpya ya Ukonga katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilala?

Supplementary Question 1

MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa mchakato wa kuanzisha Wilaya ya Ukonga ulifanywa mwaka 2015 sambamba na uazishwaji wa Wilaya ya Kigamboni na Ubungo katika halmashauri mbili ambazo wakati huo Mkoa wa Dar es Salaam ulikuwa na Halmshauri ya Temeke, Ilala na Kinondoni. Kwa hiyo, Wilaya zote za Mkoa wa Dar es Salaam zilifanya mchakato wa kutaka kuongeza halmashauri ikiwemo Halmashauri ya Wilaya Ukonga. Je, Serikali haioni haja sasa ya kurudia kwenye kumbukumbu zake kuangalia jambo hilo ili lifanyiwe utaratibu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwanza, niipongeze Serikali kwa kuanzisha Jiji la Dar es Salaam lakini kwa kuwa Ofisi za Halmashauri ya Jiji ziko katika Mtaa wa Morogoro Road na Drive In kwa kifupi mjini Posta na kwa mkazi wa Chanika, Msongora, Mzinga, Kitunda, Zingiziwa, wana changamoto kubwa ya kufika kwenye Halmashauri hizo za Wilaya ili kuweza kupata huduma za kijamii. Je, Serikali haioni haja ya kusisitiza jambo hili la kupata Wilaya mpya ya Ukonga? (Makofi)

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza Mheshimiwa Mbunge anasema mchakato ulifanyika mwaka 2015, wakati wa mchakato ule Halmashauri za Ubungo na Kinondoni ndizo zilizokuwa na sifa za kupata Halmashauri za Wilaya na anasema twende tuka-review mchakato wa mwaka 2015. Nafikiri jibu la Serikali ni la msingi, kama kuna maombi mapya ni lazima muanze upya mchakato na kila kipindi kinapopita kinakuwa na sababu zake. Kwa hiyo, maombi yote ya nyuma kwa sasa hivi tunasema ni maombi ambayo hayatambuliki kwa sababu zoezi lile lilifanyika kwa wakati mmoja na halmashauri ambazo zilikidhi vigezo zilipewa hiyo hadhi za kuwa wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ushauri wangu utabaki palepale kwamba kama kuna nia hiyo anzeni upya watu wa Ukonga mfuate taratibu zote za kisheria, mlete maombi na sisi tutayapeleka kwa Mheshimiwa Rais. Rais ndiye atakayekuwa na maamuzi ya mwisho ya kuanzishwa either kwa Wilaya ya Ukonga ama kusitisha kwa kadri atakavyoona inafaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili amerudia jambo lilelile kwa sababu Makao Makuu ya Ofisi za Jiji yapo mjini sana na anaona kwamba kuna haja ya kuwa na wilaya mpya ili kusogeza huduma. Kikubwa ni kwamba Serikali tutaendelea kupeleka huduma kwa wananchi, lakini hayo maombi yenu kama yatakidhi basi Serikali itaendelea kuangalia. Hilo nafikiri ndiyo jibu sahihi kwa wakati huu. Ahsante.

Name

Deo Kasenyenda Sanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Makambako

Primary Question

MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza: - Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha Wilaya mpya ya Ukonga katika Halmashauri ya Wilaya ya Ilala?

Supplementary Question 2

MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa Makambako kuhusiana na masuala ya Polisi na TANESCO ni wilaya na taasisi zingine ni wilaya. Serikali haioni sasa ni muhimuMakambako tupewe wilaya kwenye Halmashauri ya Mji wa Makambako kwa sababu taasisi zingine zote zipo kiwilaya kasoro halmashauri kutamka kwamba ni Halmashauri ya Wilaya ya Makambako?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Sanga, kama ifuatavyo:
-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameeleza kwamba Halmashauri ya Mji wa Makambako ambapo yeye ndiye Mbunge wa eneo hilo kwamba kipolisi ni wilaya. Nieleze tu kuna wilaya za kipolisi na wilaya za kiutawala ambapo sisi Ofisi ya Rais - TAMISEMI tunasimamia. Ndiyo maana unajikuta kuna maeneo mengine ni Mikoa ya Kipolisi, kwa mfano Ilala ni Mkoa, lakini ni wilaya, kulikuwa na Kinondoni wakati fulani zilikuwa Wilaya za Jiji la Dar es Salaam wakati ule lakini bado zilikuwa zinatambulika kama ni Mikoa ya Kipolisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, huwezi kuniambia tu kwa sababu Kinondoni ni Mkoa wa Kipolisi basi tutamke leo kutakuwa na Mkoa wa Kinondoni. Niseme tu hizo ni taratibu za kiutendaji za kiserikali endapo wao wanaona wanahitaji kuwa na halmashauri basi wafuate taratibu kama ambavyo tumejibu katika swali la msingi. Ahsante.