Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: - Je, ni lini Serikali itaandaa utaratibu mzuri wa matibabu kwa watu wenye ulemavu wakati ikisubiri Bima ya Afya kwa wote?

Supplementary Question 1

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishukuru Serikali kwa majibu mazuri; nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ugonjwa hautasubiri mpaka mpango huu mzuri wa bima ya afya kwa wote ukamilike, na kwa kuwa miongozo ambayo inatolewa na Serikali kiuhalisia haizingatii na watendaji; ni nini kauli ya Serikali kwa watendaji hawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ikumbukwe kwamba wakati wa Bajeti ya Wizara hii ya Afya, Mheshimiwa Waziri wakati akihitimisha hotuba ya bajeti yake alisema kwamba Serikali imeandaa utaratibu mzuri wa matibabu kwa wazee, ambapo alisema kwamba zitaandaliwa tisheti nzuri ambazo zitahamasisha utoaji wa huduma bora kwa wazee.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Serikali inaonaje mpango huu mzuri ukawajumuisha na watu wenye ulemavu?

Kwa mfano kama tisheti hizi zitaandikwa mzee kwanza, basi iwe mzee kwanza na mtu mwenye ulemavu, lakini pia kama itaandikwa kwamba tuwajali wazee basi tuwajali wazee na watu wenye ulemavu.

Name

Dr. Godwin Oloyce Mollel

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Siha

Answer

NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL). Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kusema kwamba ni kweli kama Mheshimiwa Mbunge anavyosema, kwamba ugonjwa na matatizo hayasubiri mswada kutengenezwa. Lakini kama ambavyo unajua kwamba kwa sasa kwenye hospitali zetu; na kwenye eneo hilo anachotaka kujua Mheshimiwa Mbunge ni tamko gani linatolewa. Kwa sababu kwa kweli pamoja na kuwepo na sheria na vitu, vingine inawezekana kuna maeneo ambayo haizingatiwi maelekezo ya Serikali kwa mambo ambayo kwa sasa yapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi niseme na nitoe ari kwamba, kwanza agizo, Waganga Wakuu wa Mikoa na Ma-DMO wanapokuwa wanazunguka; cha kwanza kwenye CCP zetu na kwenye supervision zao wahakikishe kwamba wamekagua na kuhakikisha kwamba hizi haki zimezingatiwa. Pia kuwaomba kupitia TAMISEMI Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala kusimamia suala hilo ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ni kuhusu suala la kuunganisha huduma za watu wenye ulemavu pamoja na huduma za wazee. Kama ambavyo tayari Mheshimiwa Waziri ameshazindua hili suala la tisheti na kuzindua huo mkakati wa kuweza kuboresha huduma za wazee kama ambavyo mmeona kwenye vyomba vya Habari; tunachukuwa wazo lake kwamba hilo suala liende kuunganishwa pamoja na suala la watu wenye ulemavu.