Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Khalifa Mohammed Issa

Sex

Male

Party

ACT

Constituent

Mtambwe

Primary Question

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA aliuliza:- Je, ni lini Serikali italeta Bungeni Muswada wa Mabadiliko ya Sheria ya Mkopo wa Elimu ya Juu ili kuwapunguzia mzigo mkubwa wa malipo wanufaika wa mkopo huo?

Supplementary Question 1

MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuondoa tozo ile lakini pia mpango ambao Wizara ya Elimu inaupanga kuondoa tozo ya asilimia 10 kwa wanufaika baada ya grace period. Hata hivyo nina maswali mawili madogo ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali inakata asilimia 15 ya gross salary ya mnufaika baada ya kuajiriwa, je, haioni asilimia 15 ni kubwa haiwezi kuipunguza mpaka kufikia angalau single digit; asilimia 5, 6 mpaka 9? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa kuwa mfuko huu unanufaisha wale degree holders haioni sasa wakati umefika kushuka chini katika vyuo vya kati kama vile VETA, FDCs na kadhalika?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba sasa kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khalifa, Mbunge wa Mtambwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli wanufaika hawa huwa wanakatwa asilimia 15 kutoka kwenye mshahara wao ghafi kwa ajili ya kurejesha mikopo hii. Lengo la kukata asilimia 15 ni ili kuweza kurejesha fedha zile kwa haraka na kwa muda mfupi. Hata hivyo, tupokee mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge ya kuangalia namna gani tunaweza kupunguza eneo hilo. Kwa vile tarehe 4 na 5 ya mwezi huu tuliwasilisha bajeti yetu hapa na miongoni mwa mijadala iliyotokea ni kuhusiana na hii Bodi ya Mikopo na kwa vile tutakuwa na mjadala mpana wa kitaifa, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge tunakwenda kulijadili na hili tuweze kuangalia namna gani tunaweza tukalizingatia.

Mheshimiwa Spika, swali la pili anauliza mikopo hii imewalenga sana wale wanaochukua elimu ya juu kwa maana ya degree, ni namna gani tunaweza tukafikia zile kada za vyuo vya kati. Kwa vile tutakuwa na mjadala mpana wa kitaifa juu ya mwelekeo ya elimu katika Taifa letu basi na hili nalo tutakwenda kulijadili kwa kina na ninyi Waheshimiwa Wabunge mtakuwa ni sehemu ya mjadala huo, tunaamini tutapata mawazo endelevu kuona ni namna gani tunaweza nalo hili tukaliingiza kwenye mpango.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.