Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Jacqueline Kandidus Ngonyani (Msongozi)

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga vituo vya afya katika Kata za Tinginya, Muhimba, Kalulu, Mindu, Nalasi Magharibi na Nalasi Mashariki Wilayani Tunduru?

Supplementary Question 1

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja la nyongeza, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Tunduru, na kwa Kata hizi zilizotajwa; Tinginya, Malumba, Kalulu, Mindu, Narasi Mashariki na Narasi Magharibi, ni kata ambazo hazina vituo vya afya. Lakini pia zinazungukwa na Selous Game Reserve. Wakati mwingine unakuta wale akinamama wanaokwenda kujifungua, haja ya kujifungua inawapata wakati wa usiku ambapo sasa kutoka maeneo waliyopo mpaka kufika kwenye hospitali ya wilaya pana zaidi ya takribani kilometa 80 mpaka 100 na wakati mwingine sasa wamekuwa wakipata majanga ya kuvamiwa na tembo, wanyama wakali kama simba na chui.

SPIKA: Swali.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ni lini sasa Serikali itaona umuhimu wa wananchi hawa kujengewa vituo vya afya ili waweze kuondokana na adha hiyo?

(b) Mheshimiwa Spika, maeneo hayo yote niliyoyataja yana zahanati tu, na zahanati zao wakati mwingine unakuta hazina watumishi wa kutosha. Zahanati moja ina mtumishi mmoja na kwamba akiumwa huyo mtumishi ni wiki nzima hakuna huduma ya afya. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba zahanati hizo zinapelekewa wahudumu wa afya ili waweze kupata huduma inayostahili? Ahsante.

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ameuliza kwamba lini Serikali itaona umuhimu wa kujenga vituo vya afya katika maeneo hayo. Na nilishalijibu katika jibu langu la msingi kwamba kwa kadri ya upatikanaji wa fedha Serikali tutaendelea kujenga katika maeneo husika, na nimhakikishie kabisa kwamba Serikali inazingatia umuhimu wa maeneo hayo ambayo wananchi wanatokea. Kwasababu kama alivyoeleza hapo awali kwamba kuna changamoto nyingi. Kwa hiyo, nimhakikishie tu kwamba tutayaingiza katika mpango na fedha itakavyopatikana ataona matokeo yake.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ameeleza kwamba katika maeneo hayo watumishi/wahudumu wa afya hawapo wa kutosha. Na sisi kama Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya tuna huo mpango, kwa kadri tunavyokuwa tunaajiri kutokana na vibali ambavyo tunapatiwa tutaendelea kuwatenga. Kwa hiyo, hata maeneo hayo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutaendelea kupeleka kulingana na vibali vya ajira ambavyo serikali itakuwa inatupatia. Ahsante.

Name

Dr. John Danielson Pallangyo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Arumeru-Mashariki

Primary Question

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga vituo vya afya katika Kata za Tinginya, Muhimba, Kalulu, Mindu, Nalasi Magharibi na Nalasi Mashariki Wilayani Tunduru?

Supplementary Question 2

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Changamoto zilizoko Tunduru zinafanana sana na changamoto zilizoko kule Arumeru Mashariki, hususan Kata za Maruvango, Kikatiti, Malula na Majengo. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga vituo vya afya kwenye hizo kata ambazo nimezitaja?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nilijibu katika swali la msingi kwamba kwa kadri Serikali tutakavyokuwa tunapata fedha ya kutosha na bajeti yetu tutakavyokuwa tunaitenga, tutaendelea kujenga. Kwa hiyo, hata maeneo ya Arumeru Mashariki nayafahamu na ninajua umbali wake. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kadri fedha itakavyopatikana basi tutazingatia na maeneo husika. Ahsante.