Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Conchesta Leonce Rwamlaza

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA Aliuliza:- Je, ni lini Serikali itawalipa fidia Wananchi wenye Viwanja eneo la Miganga West na East, Kata ya Mkonze katika Manispaa ya Jiji la Dodoma kwa kuwa uthamini ulishafanywa na baadhi ya Wananchi bado hawajalipwa?

Supplementary Question 1

MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kitu cha kwanza, majibu niliyopewa ni tofauti kabisa na majibu ambayo nimesomewa na Waziri, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sheria inasema, wakithamini wanapaswa walipe wale wathaminiwa ndani ya miezi sita; na kwa kuwa watu wengine wameshalipwa: Je, wale ambao hawajalipwa, kuna nyongeza yoyote ambayo itawekwa kwa ajili ya fidia kwa sababu Serikali imechelewa kulipa na hawajaweza kuendeleza maeneo yao? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili: mwananchi yeyote anapochukua kiwanja cha Serikali ambacho kimepimwa anakuwa amejihakikishia makazi yake kwa sababu atajiandaa katika maisha yake; kuchukua viwanja vyao, ukachelewa kulipa ni kuwadumaza: Pamoja na majibu aliyotoa, wale watu waliobaki watalipwa lini kwa commitment ya Serikali? (Makofi)

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Conchesta kama alivyouliza. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Dugange kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza ana hofu ya kujua kwamba wale ambao hawajalipwa, watalipwaje pesa zao? Je, kutakuwa na nyongeza? Sheria iko wazi na tuliipitisha hapa 2019 tukafanya marekebisho kwamba inapofika miezi sita kama hajalipwa, tunaanza ku-calculate interest kwa bei ya soko iliyopo wakati huo. Hii inakwenda ndani ya miaka miwili, ikifika miaka miwili hawajalipwa maana yake lile zoezi inabidi lianze tena uthamini upya. Sheria tuliipitisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe hofu tu kwamba watu hawa watalipwa kwa bei ya soko wakiwa wamewekewa na riba yao katika pesa walizochukua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anauliza, ni lini pengine wataacha kuchukua maeneo ya watu halafu wanakuwa hawana uhakika wa malipo yao? Naomba niseme tu kwamba katika maeneo ambayo Serikali inakuwa na interest nayo, lazima itaongea na washirika waliopo pale, wenye ardhi zao, kuwaambia dhamira na nia njema ya Serikali; na kabla ya kutwaa kunakuwa na makubaliano ambayo ni lini maeneo haya yatatwaliwa na kwa kazi ipi? Inapokuwa na public interest, huwa haina majadiliano zaidi ya kukaa nao na kukubaliana nini kifanyike?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa hili ambalo tayari tunaona ni miradi mikubwa ya Kiserikali ambayo inapita, hatutakuwa na mjadala mwingine isipokuwa ni kuzungumza nao. Tayari Tume ya Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi katika maeneo yote inayopita miradi mikubwa, wameshaandaa mpango wa matumizi ya ardhi. Kwa hiyo, wale watakaobaki pale, watapimiwa maeneo yao, wale watakaotakiwa kuondoka kwa ajili ya kupisha pengine labda ni zile stations zinazojengwa, basi watapewa fidia yao kwa mujibu wa soko la wakati huo. (Makofi)