Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

George Natany Malima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Primary Question

MHE. GEORGE N. MALIMA Aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la muda mrefu la uhaba wa maji kwa wananchi wa Mji wa Mpwapwa?

Supplementary Question 1

MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa tatizo la maji katika Mji wa Mpwapwa limekuwa la muda mrefu. Na kwa kuwa, Serikali imekiri kwamba, ni kweli limekuwa la muda mrefu na kwamba, wana mpango wa kuchimba visima viwili katika eneo la Kikombo ili kuongeza upatikanaji wa maji katika mji ule.

Je, ni lini uchimbaji huu wa visima hivi viwili utakamilika ili watu wa Mpwapwa nao wapate unafuu wa shida ya maji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; mwezi Januari timu kutoka Wizara ya Maji ilikuja kutembelea katika Jimbo langu, tulikagua miradi miwili ya maji mmoja katika Kijiji cha Vingh’awe na mmoja katika Kijiji cha Manhangu; na mradi ule wa Vingh’awe ulitengenezwa siku nyingi, lakini historia iliyopo ni kwamba ulipochimbwa miundombinu ilijengwa chini ya kiwango; ulifanya kazi siku tatu tu mabomba yalipasuka, lakini tenki ambalo lilijengwa below standard pia nalo lilibuja lote halafu ule mradi ulikufa, lakini mradi wa Manhangu pia una story inayofanana.

Je, Serikali inasemaje kuhusu hili, maana walikuja kukagua na wakaahidi kwamba wataifanyia matengenezo ili ifanye kazi. Je, ni lini watakuja kurekebisha hiyo miradi miwili?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika,ahsante, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa George Malima, Mbunge wa Mpwapwa kama ifuatavyo:-

Swali lake la kwanza ni lini mradi ule unakwenda pesa zitapelekwa ili mradi uendelee kutekelezwa. Jibu lake kwa sababu mradi uko ndani ya mwaka wa fedha huu 2020/2021 Mheshimiwa Mbunge nakuhakikishia kabla ya mwaka huu wa fedha kuisha kwa maana ya mwezi Juni hii fedha itakuwa imefika na tutasimamia utekelezaji wake kwa karibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ameongelea kuwa mwezi Januari kuna timu kutoka Wizarani ilikwenda na ni kweli. Miradi hii anayoiongelea ya Vingh’wale pamoja na Manhangu kwa pale Mpwapwa ni kati ya miradi ya ule mpango wa vijiji kumi ambao Wizara imekuwa ikiifanyia kazi na vijiji hivi kwa hakika vilikuwa na changamoto kubwa sana ya maji, lakini kwa awamu hii sisi tumejipanga kuhakikisha kuona kwamba miradi ile kwenye ile programu ya vijiji kumi tunakwenda kuisimamia ambayo ina vijiji takribani 177 vyote tunakwenda kuhakikisha tunarekebisha pale ambapo kidogo palikuwa na mapungufu. Lakini vilevile tutahakikisha wananchi wetu wanakwenda kupata maji safi na salama na ya kutosheleza.

Name

Shamsia Aziz Mtamba

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Mtwara Vijijini

Primary Question

MHE. GEORGE N. MALIMA Aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la muda mrefu la uhaba wa maji kwa wananchi wa Mji wa Mpwapwa?

Supplementary Question 2

MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ili nami niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilianza mpango wa kulipa fidia kwa wananchi wa Mtwara Vijijini waliopitiwa na bomba la maji mwaka 2015; nataka kujua mradi huu umekwamia wapi wakati uthamini ulishaanza kufanyika?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika,ahsante kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shamsia kutoka Mtwara Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi ambao umeshafanyiwa usanifu Serikali tumejipanga tunakuja kuhakikisha kuona kwamba usanifu ule unakamilika na utekelezaji wake utakamilika. Miradi yote namna ambavyo ipo kwenye mikataba namna ambavyo tumekuwa tukiianza tunakwenda kuhakikisha kwamba maji yanatoka na changamoto zote ambazo zilikuwepo huko nyuma kwa kipindi hiki tunakwenda kuzimaliza.

Name

Ally Juma Makoa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kondoa Mjini

Primary Question

MHE. GEORGE N. MALIMA Aliuliza:- Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la muda mrefu la uhaba wa maji kwa wananchi wa Mji wa Mpwapwa?

Supplementary Question 3

MHE. ALI J. MAKOA: Mheshimiwa Naibu Spika,ahsante sana; kwa kuwa tatizo la Mji wa Mpwapwa linafanana na Mji wa Kondoa, Halmashauri ya Mji wa Kondoa ina tatizo kubwa la muda mrefu la maji na tatizo ni uchakavu wa miundombinu.

Ni lini Serikali itapeleka fedha kutatua tatizo la miundombinu chakavu ya maji iliyojengwa miaka ya 1970?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika,ahsante, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Makoa kutoka Kondoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi yote ambayo muda wake wa uhai umekwisha kwa maana ya lifespan imesha- expire sasa hivi tayari tumeshaanza mchakato wa kuona namna gani mwaka ujao wa fedha kukarabati labda kwa kubadilisha mabomba kama yamechakaa sana au kuongeza mabomba kwa maana ya mtawanyo wa miundombinu au kuona kwamba kama kipenyo kilikuwa kidogo tutaweka mabomba makubwa kulingana na idadi ya watu namna ilivyoongezeka na uhitaji wa maji safi ulivyoongezeka hivyo nipende kumwambia Mheshimiwa Ali Makoa kuwa Kondoa napo tunakwenda kupaletea mapinduzi makubwa kuondoa changamoto ya maji.