Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rashid Mohamed Chuachua

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Masasi Mjini

Primary Question

MHE. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:- Jeshi la Polisi limekuwa likifanya kazi katika mazingira magumu sana kutokana na uchakavu wa vitendea kazi pamoja na kukosekana kwa magari ya kutosha:- (a) Je, ni lini Serikali itawapatia magari Askari Polisi wa Wilaya ya Masasi kutokana na kutokuwa na magari ya kutosha? (b) Je, ni lini Serikali itarekebisha utaratibu uliopo ambapo askari wanalazimika kutoa pesa zao za mfukoni kuwapa chakula mahabusu? (c) Je, ni lini Serikali itajenga nyumba za askari katika Wilaya ya Masasi?

Supplementary Question 1

MHE. RASHID M. CHUACHUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kupata fursa ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa gari alizozitaja Toyota Land Cruiser na Grand Tiger ni gari mbovu sana ambazo hazifai kufanya kazi katika kipindi hiki ambacho Polisi wana majukumu makubwa. Pia gari la Leyland ambalo amelitaja siyo la kazi ngumu kwa sababu kwanza halina hata four-wheel drive. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kufanya jambo hili ni la dharura kwa askari wetu wa Jeshi la Polisi waishio Masasi ili waweze kupata gari haraka iwekekanavyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa hali ya nyumba za Askari Polisi waishio Masasi ni mbaya sana maana zimejengwa tangu enzi ya mkoloni. Je, Naibu Waziri yuko tayari kuongozana nami hadi Masasi baada ya Bunge hili ili akashuhudie hizo anazoziita nyumba 15 zilizopo?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge wa Masasi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na hoja ya umuhimu wa kupeleka magari mengine katika Jimbo la Masasi ni muhimu na nilieleza hivyo kwenye jibu langu la msingi tunaamini kwamba kuna haja ya kupeleka magari Masasi. Kwa hiyo, tunakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba magari yaliyopo hayatoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli magari yale mawili ni ya zamani ingawa yakitengenezwa yatasaidia. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa tunatambua umuhimu wa Wilaya ya Masasi kuwa na magari ya ziada, kwa sasa hivi hatuna magari mapya lakini pale ambapo yatapatikana katika maeneo ambayo tutayaangalia kwa jicho la karibu moja ni Wilaya ya Masasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na swali lake la pili nimthibitishie kwamba niko tayari kwenda pamoja naye katika Jimbo la Masasi kwa mara nyingine tena. Niliwahi kufika Masasi na nayafahamu mazingira ya Masasi lakini kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge anahisi kuna haja ya kuambatana naye kwa mara nyingine tena basi tutafanya hivyo ili kwa pamoja mimi na yeye tuweze kuona jinsi gani tunaweza tukakabiliana na changamoto mbalimbali zinazohusu vyombo vyetu vya usalama vilivyopo pale hususan Jeshi la Polisi.

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:- Jeshi la Polisi limekuwa likifanya kazi katika mazingira magumu sana kutokana na uchakavu wa vitendea kazi pamoja na kukosekana kwa magari ya kutosha:- (a) Je, ni lini Serikali itawapatia magari Askari Polisi wa Wilaya ya Masasi kutokana na kutokuwa na magari ya kutosha? (b) Je, ni lini Serikali itarekebisha utaratibu uliopo ambapo askari wanalazimika kutoa pesa zao za mfukoni kuwapa chakula mahabusu? (c) Je, ni lini Serikali itajenga nyumba za askari katika Wilaya ya Masasi?

Supplementary Question 2

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru umenipa nafasi ili niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niishukuru sana Wizara ya Mambo ya Ndani kutupatia fedha kujenga nyumba sita za askari pale Babati Mjini, kwenye Mtaa wa Bagala Ziwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jengo la RPC katika Mkoa wetu wa Manyara liko Mtaa wa Komoto. Tangu mwaka 2006 liko kwenye lenta, miaka 13 sasa Wizara hamjatuletea fedha. Mmeweza kutuletea shilingi milioni 150 kazi inaendelea, ni lini sasa mtatuletea fedha kwa ajili ya kukamilisha jengo la RPC pale Babati Mjini? Ahsante.

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Pauline Gekul, Mbunge wa Babati Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi kabisa kwamba jengo hilo linahitaji kukamilika. Tunayo majengo kadhaa nchi nzima ambayo yanahitaji kukamilishwa, siyo tu kwa Jeshi la Polisi, kwa upande wa Jimbo lake la Babati, nadhani atakubaliana nami hata jengo la Uhamiaji nalo linahitaji kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, si dhamira ya Serikali kuona majengo haya yanafikia robo ama nusu kukamilika. Dhamira ya Serikali ni kuona majengo haya ambayo yametumia fedha nyingi na yana umuhimu mkubwa kwa ajili ya vyombo vyetu yakamilike haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ambayo inatukabili ni fedha kwamba bajeti haitoshi kukamilisha majengo yote kwa wakati mmoja. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Mbunge avute subira, pale ambapo hali ya kibajeti itakaa vizuri tutakamilisha majengo yote mawili ikiwemo la Polisi na Uhamiaji katika Jimbo lake pamoja na majengo mengine ambayo yanasubiri kukamilishwa nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ya mwaka huu tumetenga fedha kiasi ambazo zitaendelea kutatua changamoto hiyo. Kadri miaka inavyokwenda na hasa tukitilia maanani uchumi wa nchi yetu unakwenda vizuri sasa kutokana na kazi kubwa ya Serikali ya Awamu ya Tano, chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, naamini kabisa miaka ya mbele tutakuwa na fedha za kutosha kuweza kukamilisha majengo yote ambayo hayajakamilika.

Name

Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Primary Question

MHE. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:- Jeshi la Polisi limekuwa likifanya kazi katika mazingira magumu sana kutokana na uchakavu wa vitendea kazi pamoja na kukosekana kwa magari ya kutosha:- (a) Je, ni lini Serikali itawapatia magari Askari Polisi wa Wilaya ya Masasi kutokana na kutokuwa na magari ya kutosha? (b) Je, ni lini Serikali itarekebisha utaratibu uliopo ambapo askari wanalazimika kutoa pesa zao za mfukoni kuwapa chakula mahabusu? (c) Je, ni lini Serikali itajenga nyumba za askari katika Wilaya ya Masasi?

Supplementary Question 3

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Mtwara kimejengwa enzi ya Mkoloni na hivi sasa ukiingia mle ndani kinakaribia kubomoka, kinauliza kabisa niue nikuache, niue nikuache? Kila mwaka tunazungumza ndani ya Bunge na Serikali inasema imetenga bajeti. Kwa nini mpaka leo Serikali haileti fedha kwa ajili ya kukarabati kituo hiki ambacho hivi sasa kinatarajia kubomoka?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maftaha Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu yatakuwa ni yale yale tu kwamba vituo vinavyohitaji kukarabatiwa ni vingi ikiwemo hiki cha Mtwara Mjini. Hata hivyo, kwa sababu kituo hiki nakifahamu na gharama zake za ukarabati si kubwa sana pengine mimi na Mheshimiwa Mbunge wakati tukisubiri hali ya bajeti ikae vizuri tushauriane ikiwezekana hata kwenda pamoja jinsi ya kutafuta njia zingine mbalimbali za kusaidia kukiweka vizuri kituo hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya hivyo katika maeneo mbalimbali nchini kwa kutumia rasilimali nyingine nje ya kibajeti. Nina hakika kwa gharama ndogo za ujenzi zinazohitajika katika kituo hicho tunaweza tukafanikiwa tukashirikiana. Naamini Mheshimiwa Maftaha ni mchakapazi kwa hiyo, hata nikimshawishi na yeye kupitia fedha za Mfuko wa Jimbo achomoe kidogo halafu tushirikiane kutafuta wadau basi tutaweza kukitendea haki kituo hiki.