Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:- Kwa muda mrefu kumekuwa na migogoro ya mipaka baina ya wananchi na Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) katika maeneo ya Mkonkole Kata ya Tambuka Reli, Usule Kata ya Mbungani na Kata ya Cheyo Tabora Mjini:- Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka wa kutatua mgogoro huo ambao ni wa muda mrefu?

Supplementary Question 1

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA. Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Tabora hasa Manispaa imezungukwa na kambi za jeshi kwa eneo kubwa. Kutokana na hali hiyo kumekuwa na migogoro mikubwa ambayo inapelekea wananchi ambao wamekuwa wakitumia maeneo kwa muda mrefu kufikia hata kupigwa wanapokuwa wanafanya shughuli zao. Kwa mfano, kuna eneo ambalo kuna barabara inapita katika kata nne eneo la Uyui, kuna eneo la Rada, barabara hii ni ya miaka mingi na ni hiyo tu ambayo wananchi wa kata hizo nne wanaitumia, ikifika saa moja na nusu mpaka saa mbili usiku, wananchi wakipita maeneo maeneo yale wamekuwa wakipigwa na wakati mwingine hata kunyanganywa vifaa vyao vya usafiri zikiwemo baskeli. Je, Serikali ina mpango gani kuhusiana na eneo hilo ambalo wananchi wamekuwa wakitumia kama barabara?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa shughuli nyingi zimesimama katika maeneo hayo hasa za wananchi ambao walikuwa wakitumia maeneo hayo kwa kulima ambayo wamekuwa wakilima muda mrefu, lakini wengine na shughuli zao za kiutamaduni kwenye mapori ambayo wamekuwa hata hawayapi athari yoyote. Je, kutokana na hali hiyo ambayo ni ya muda mrefu Mheshimiwa Waziri yupo tayari sasa kuja Tabora ili tuweze mimi na yeye kwenda kukagua maeneo haya na kuyapatia utatuzi ambao ni mgogoro wa muda mrefu? (Makofi)

Name

Dr. Hussein Ali Mwinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwahani

Answer

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara inayopita kuelekea eneo la Rada la jeshi na kwamba wananchi wanapopita hapo wanapigwa, suala hili nitalifuatilia ili niweze kupata taarifa rasmi ya nini hasa kinachoendelea. Hakuna sheria inayoruhusu wananchi kupigwa, lakini kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge nitakuwa tayari kwenda kufanya ziara katika eneo hili la Tabora Mjini ili nijionee mimi mwenyewe hali ilivyo pale na tutafute ufumbuzi, suluhu kwa ajili ya maslahi ya pande zote. Ni vema wananchi watambue kwamba, yale mapori yanayoonekana kama hayana kazi, ni maeneo ambayo wanajeshi wanafanya mazoezi, kwa hiyo yana kazi maalum. Tukifanya hii ziara, tutaweza kuambatana na viongozi wa jeshi ili tuone ni ufumbuzi gani ambao unaweza ukapatikana.