Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

John Wegesa Heche

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. JOHN W. HECHE aliuliza:- Mgodi wa North Mara (Acacia Gold Mine) umeanza uchimbaji wa ardhini (underground) sasa yapata mwaka mzima bila kuweka wazi kama kuna mabadiliko ya kimkataba na kitendo hiki ni hatari kwa usalama wa kijiografia kwa wakazi wanaozunguka mgodi huo:- Je, kwa nini Serikali isizuie zoezi hili mpaka mikataba iridhiwe na Serikali za Kijiji na kuanza upya bila kuwepo makandokando?

Supplementary Question 1

MHE. JOHN W. HECHE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza nitambue jitihada ambazo zimefanywa na Waziri, Mheshimiwa Muhongo katika kujaribu ku-ssetle down issue hii na wananchi wa Tarime wanasubiria kwa hamu sana majibu yake kuhusu malipo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, niulize maswali mawili ya nyongeza. Nataka Waziri atambue kwanza kwamba neno „mongo’ siyo neno la siku moja, ni neno la Kikurya lenye maana ya sehemu ya kutunza mali. Kwa hiyo, mgodi ule upo enzi na enzi na watu wa pale wametegemea maisha hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa leo Waziri anakuja na jibu hapa, siku moja nilimwambia awe anafanya research, anasema hakuna mkataba wowote ambao kijiji kinaingia na mgodi. Mimi nina mikataba ya Serikali ya Vijiji hivi, hii hapa ya mwaka 1995 ambayo mgodi uliingia na Serikali za Vijiji alivyovitaja hapo kwamba kwenye kila uchimbaji watakuwa wanatoa asilimia moja kama royalty kwenye Serikali za Vijiji. Hizi fedha zimesomesha watoto wetu pale, zimejenga shule na maisha ya vijiji vile wamekuwa wakifaidika na pesa hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tangu waanze kwenda underground wameacha kulipa royalty kwenye Serikali za Vijiji. Nataka Waziri atuambie ni lini mnauamuru mgodi huu uanze kulipa royalty, kwa sababu mnasema hauchimbi kwenye eneo la kijiji lakini pamoja na underground wako eneo la kijiji, hawako Singida wala hawako Mwanza, wako Tarime. Kwa hiyo, nataka majibu hayo atuambie ni lini wanaanza kulipa hiyo royality? Mkataba husika nitawapa hapa.
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Naibu Waziri wa Mazingira tangu mwezi wa Pili amekuja akachukua pale sample za maji na kwa wiki nzima hii pit ya Gokona imekuwa ikimwaga maji kwenye Mto Tigite ambapo watu wanalalamikia kwamba yana sumu na yanaathiri mali zao. Sasa nataka Waziri atoe kauli kuhusiana na hili kwamba pit ya Gokona sasa inamwaga maji kwenye Mto ule na yanaathiri maisha ya watu pale, mifugo na jamii nzima. Nataka atoe kauli kuhusiana na suala hilo ambalo linafanyika kwa wiki nzima sasa.

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikubaliane na Mheshimwa Heche, kwamba neno mongo ni utajiri kule kwao na kuhila ni utajiri kule kwetu Usukumani, namshukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nijibu sasa kwa weledi sana swali lake la kwanza. Nimsahihishe kidogo Mheshimiwa Heche, mikataba iliyoingiwa kati ya vijiji saba pamoja na mgodi wa Acacia ni mkataba wa malipo ya royalty siyo mikataba ya uchimbaji. Hilo ni suala la msingi sana Mheshimiwa Heche na Waheshimiwa Wabunge kulielewa. Pamoja na hayo, nikubali tu kwamba ule mkataba ulioingiwa kati ya vijiji na mgodi ambapo kila kijiji kinalipwa royalty asilimia moja bado unaendelea na wataendelea kulipwa kwa mujibu wa mikataba ile. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze kwenye swali lake la pili, inaonekana kwamba mtaalam wa NEMC ameenda kuangalia kwenye Mto Gokona na kuona kwamba kuna athari za mazingira. Serikali yetu ya Awamu ya Tano, Mheshimiwa Waziri wangu tarehe 22/2/2016 aliunda Kamati Maalum ya kufanya uchunguzi wa matatizo yote katika Mgodi wa North Mara. Katika Kamati ya watu 27 iliyoundwa Mheshimiwa Heche ametoa wawakilishi wake wanne. Kwanza, Mheshimiwa Heche tunakupongeza sana kwa kutuma wawakilishi wako wanne kwenye Kamati ile.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme tu kwamba Kamati iliyoundwa kwa ajili ya kuchunguza masuala yote ya Mgodi wa North Mara ikiwa ni pamoja na matatizo ya kimazingira ina ToR (Hadidu za Rejea) 27. Kati ya hizo, tano zinahusiana na matatizo ya athari ya mazingira kwenye Mto Gokona. Kwa hiyo, naamini kwamba taarifa itakapokuja na imeshakuja tunaifanyia kazi, utekelezaji wa mapendekezo ya Kamati hiyo yatatolewa na Mheshimiwa Heche atapewa maelekezo ya hatua za Serikali zilizochukuliwa.