Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Stanslaus Shing'oma Mabula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nyamagana

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. AMINA N. MAKILAGI) aliuliza:- Je, nini mipango ya Serikali ya kumaliza tatizo kubwa la nyumba za askari hapa nchini?

Supplementary Question 1

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
Kwa kuwa Serikali inakiri kuwepo na tatizo kubwa la upungufu wa nyumba za makazi ya askari polisi na vyombo vingine ambavyo viko ndani ya Jeshi la Mambo ya Ndani. Serikali haioni sasa mipango na mikakati iliyonayo bado haiwezi kuwa ni kigezo cha kukamilisha tatizo hili kubwa tulilonalo nchini?
Swali langu la pili, pamoja na matatizo haya ziko nyumba ambazo zimeshaanza kujengwa takribani miaka mitano leo, zikiwemo nyumba za Mabatini Barracks katika Jimbo la Nyamagana na maeneo mengine kama Musoma na Mikoa mingine yenye matatizo kama haya.
Je, ni lini Serikali itahakikisha nyumba hizi ambazo zikikamilika kwa wakati kwanza tunaokoa upotevu wa fedha nyingi, lakini inasaidia watu wetu wanaohangaika kutafuta makazi kukaa kwenye makazi yaliyo bora na kuwafanya wafanye kazi yao kwa uaminifu na uhakika zaidi? (Makofi)

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianzia na mradi wa nyumba ambazo zipo katika Jimbo lake nikiri kwamba nyumba zile zimefika katika hatua za mwisho kukamilika. Mimi na yeye tuliwahi kufanya ziara kutembelea, tuliona kwamba kuna umuhimu wa nyumba zile kukamilika kwa haraka ili kuweza kutatua tatizo la makazi katika eneo la Nyamagana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo Nyamagana tu, tuna nyumba maeneo mbalimbali nchini ambazo zipo katika hatua za kukamilika, ikiwemo Musoma Mjini, Kagera, Mtambaswala huku Mtwara, Ludewa na kadhalika. Kwa hiyo, kwa kutambua kwamba kuna haja ya kumaliza nyumba hizi ambazo zimefika katika hatua nzuri katika bajeti ya mwaka huu ya maendeleo ambayo tumetenga takribani zaidi ya shilingi bilioni 5.2 malengo ni kukamilisha miradi hii ambayo imefikia katika hatua nzuri na za mwisho.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba tunatarajia katika kipindi cha mwaka huu wa fedha tutamaliza project ile ya Nyamagana (Mabatini) pamoja na nyingine ambazo nimezitaja. Kwa hiyo, ni miongoni mwa mikakati ya Serikali ya kutatua matatizo ya nyumba za askari nchini.