Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:- Ajira kwa sasa ni tatizo hapa nchini hasa kwa walimu wa sanaa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuajiri katika sekta mbalimbali?

Supplementary Question 1

MHE. FREDY A. MWAKIBETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina swali moja tu la nyongeza. Taifa lolote duniani ili lisonge mbele linahitaji watu waliosoma kada mbalimbali, iwe ni sanaa, sayansi au biashara.
Je, Serikali ina mpango gani wa ku-balance wanafunzi wanaosoma masomo ya sayansi, pamoja na wanafunzi wanaosoma sanaa ili isitokee kama sasa tuna ziada ya wanafunzi wa sanaa zaidi ya 7,463 na inapelekea kutokuwa na ajira. Serikali ina mpango gani kwa miaka ya hivi karibuni na baadaye? (Makofi)

Name

Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Answer

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Serikali, imekuwa ikiendelea kuweka mazingira mazuri na kuhamasisha wanafunzi kusoma masomo ya sayansi. Katika mwaka 2015 mpaka 2016 Serikali ilijikita zaidi katika kuhamasisha Shule za Sekondari kujenga maabara. Katika mwaka 2016/2017 tunasambaza vifaa vya maabara. Hizo zote ni jitihada za kuongeza wanafunzi wa masomo ya sayansi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile napenda kulifahamisha Bunge lako Tukufu kwamba wanafunzi wanayo hiari ya kuchagua masomo. Kwa hiyo, kama Serikali tunatoa mazingira mazuri. Nangependa kuwaomba Waheshimiwa Wabunge tushirikiane kuwahamasisha wanafunzi pia kuona kwamba masomo ya sayansi na teknolojia nayo ni muhimu ili waweze kuyachukua kwa wingi zaidi. (Makofi)

Name

Sebastian Simon Kapufi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Mjini

Primary Question

MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:- Ajira kwa sasa ni tatizo hapa nchini hasa kwa walimu wa sanaa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuajiri katika sekta mbalimbali?

Supplementary Question 2

MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Upungufu mkubwa wa Ikama na zoezi la uhakiki wa vyeti limepelekea shida kubwa ya watumishi katika maeneo ya afya, elimu, Watendaji wa Vijiji, Mitaa na Kata katika Manispaa yetu ya Katavi, kiasi cha kwamba mtumishi mmoja anafanya kazi zaidi ya moja.
Ni lini Serikali itaajiri katika maeneo hayo niliyoyazungumza?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Tunakiri ni kweli kuna upungufumkubwa wa watumishi katika baadhi ya maeneo. Niendelee tu kusisitiza kwamba lengo letu kubwa kama Serikali ni kuhakikisha kwamba, tunaenda kwa kuzingatia maeneo yenye vipaumbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tutahakikisha kwamba tunaimarisha maeneo yenye upungufu mkubwa. Nimweleze tu kwamba katika kada alizozitaja zitakuwa ni miongoni mwa kada ambazo pia tutazipa ajira katika mwaka ujao wa fedha. Vilevile labda nimtoe tu hofu kama nilivyoeleza katika jibu langu la msingi; katika mwaka ujao wa fedha tutatoa ajira 52,436 na labda tu niseme kwa mchanganuo ufuatao:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Sekta ya Elimu tutatoa ajira 16,516 kwa upande wa Sekta ya Afya 14,102, Kilimo 1,487, Mifugo 1,171, Uvuvi 320, Polisi 2,566, Magereza nafasi 750, Jeshi la Zimamoto 1,177, Uhamiaji nafasi 1,500, hospitali za mashirika ya kidini na hiari kwa kuwa nazo tunatoa ruzuku, nafasi 174 pamoja na nafasi nyinginezo 12,673 ambazo zitahusu Sekta zote na jumla kuu ni 52,436.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimtoe Mheshimiwa Kapufi hofu, ikama zote na mapendekezo kutoka kwa waajiri tumezipokea na tutaangalia katika kuimarisha maeneo hayo.

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. FREDY A. MWAKIBETE aliuliza:- Ajira kwa sasa ni tatizo hapa nchini hasa kwa walimu wa sanaa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuajiri katika sekta mbalimbali?

Supplementary Question 3

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri ulituahidi kwamba unaajiri walimu wa hesabu katika shule zetu, lakini ajira iliyotoka mwezi wa nne kwa upande wa walimu ni walimu wa biology na chemistry, ulituletea katika shule zetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi nimesema katika Bunge hili kwamba, katika shule zangu kumi za Babati Mjini za sekondari hakuna shule yenye mwalimu wa hesabu. Sasa naomba nifahamu ni kwa nini msituambie kwamba walimu wa hesabu ninyi hamna na hamna mpango wa kutuletea badala ya kutuahidi kila siku kwamba mtatuletea walimu? Watoto wetu hawasomi hesabu. Naomba kauli ya Serikali. (Makofi)

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Bahati nzuri ninayo orodha ya nafasi 3,081 za walimu wa hesabu na sayansi ambao tumewapangia vituo katika mwezi Aprili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Babati Mjini naweza kuangalia kwa haraka haraka, lakini nitoe tu mfano kwa Tarime DC, tumepeleka walimu wa hesabu, Musoma DC tumepeleka walimu wa hesabu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tutaliangalia na kama katika Manispaa yake hajapata kabisa, tutaweza kulifanyia kazi ili naye aweze kupata walimu hao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tu kumtoa hofu Mheshimiwa Gekul kwamba tulitoa kibali cha walimu wa sayansi na hesabu 4,129 na hizi ni kwa ajira za mwaka 2015. Tayari ukiangalia tumepata tu Walimu 3,081, bado kuna nafasi zaidi ya 1,000 na zaidi katika kibali hicho ambacho tumekitoa, bado hawajajitokeza. Tunashirikiana na Wizara ya Elimu pamoja na Ofisi ya Rais (TAMISEMI) tuweze kupokea maombi hayo, tumeanza kuyachambua. Watakaopatikana naamini ikitokea na walimu wa hesabu wako katika kundi hilo, basi kwa hakika kabla ya mwaka wa fedha na wewe utakuwa umepata walimu hao wa hesabu.