Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Esther Lukago Midimu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:- Wilaya ya Itilima ni moja kati ya Wilaya mpya zilizoanzishwa hivi karibuni ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi:- Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuwezesha kujenga ofisi na nyumba za watumishi katika Makao Makuu ya Wilaya ya Itilima eneo la Itilima?

Supplementary Question 1

MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba nimuulize swali dogo tu la nyongeza. Kwa kuwa, watumishi wetu hawa inawalazimu kuishi Wilaya nyingine ya Bariadi ambapo kuna umbali wa Kilometa 100 kwenda na kurudi kila siku.
Je, Serikali haioni kuna umuhimu wa kuharakisha makazi haya ili watumishi hawa waishi katika maeneo husika?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali inaona hilo, ndiyo maana hata Halmashauri yenyewe ya Itilima katika mkataba wao waliosaini na National Housing, bahati mbaya mkataba ule ulikuwa haujahusisha Ofisi ya Rais -TAMISEMI wala Ofisi ya Mkuu wa Mkoa pale katika Ofisi ya RAS na ndiyo maana Ofisi ya Rais - TAMISEMI iliona kwamba licha ya mapungufu yaliyokuwepo lakini ofisi iweze kutoa kile kibali kwa mkataba ule. Hivi sasa Ofisi ya Rais - TAMISEMI imeshatoa kibali, na kwa sababu fedha tayari ninazo na kibali kimeshapatikana, imani yangu ni kwamba ujenzi kupitia Shirika la Nyumba utakamilika haraka iwezekanavyo ili kuondoa kero ya watumishi ambao wanapata taabu kutoka katika Halmashauri moja kwenda Halmashauri nyingine.

Name

Savelina Slivanus Mwijage

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:- Wilaya ya Itilima ni moja kati ya Wilaya mpya zilizoanzishwa hivi karibuni ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi:- Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuwezesha kujenga ofisi na nyumba za watumishi katika Makao Makuu ya Wilaya ya Itilima eneo la Itilima?

Supplementary Question 2

MHE. SAVELINA S. MWIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Wilaya ya Bukoba Vijijini wanategemea Wilaya yao iliyoko Bukoba Mjini na ina umbali mkubwa sana, kata zake ziko mbali sana kuja kufika Bukoba Mjini, ni lini Serikali itaona umuhimu wa watu wa Bukoba Vijijini kupata Wilaya yao karibu?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika hili tumelichukua, lakini mchakato wa Wilaya, mchakato wa Halmashauri upo na una taratibu zake. Mimi naomba niwahimize ndugu zangu wa Bukoba na Mheshimiwa Mbunge hapa nadhani katika hili atakuwa amejipnga vyema, tufuate ule mchakato wa kawaida, tupitishe katika Halmashauri zetu, tupitishe katika vikao vya DCC, RCC, mwisho wa siku ikifika katika Ofisi ya Rais -TAMISEMI jukumu letu kubwa ni kuweza kuangalia matakwa ya jamii na kuangalia mahitaji ya msingi yakiwa yamekamilika basi tutamalizia hilo zoezi. Ahsante sana.

Name

Ritta Enespher Kabati

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:- Wilaya ya Itilima ni moja kati ya Wilaya mpya zilizoanzishwa hivi karibuni ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi:- Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuwezesha kujenga ofisi na nyumba za watumishi katika Makao Makuu ya Wilaya ya Itilima eneo la Itilima?

Supplementary Question 3

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.
Kwa kuwa Wilaya ya Kilolo ilipata kuwa hadhi ya Wilaya toka mwaka 2002 lakini majengo mengi katika Wilaya bado hayajakamilika, kama Hospitali ya Wilaya bado wanatumia Hopitali ya Mission, Makao Makuu ya Polisi bado hayajajengwa kwenye Wilaya yake na vilevile Mahakama bado hakuna…
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa naomba uulize swali!
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, je, huwa vigezo gani vinatumika katika kuweka mipango kujenga hizi Wilaya? Kwa sababu Wilaya za zamani bado hazijatimiziwa majengo yote na zinaanzishwa Wilaya mpya, nilitaka nijue vigezo gani vinatumika?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba miundombinu ya Wilaya ya Kilolo bado haijakamilika, siyo Wilaya ya Kilolo peke yake isipokuwa ni Wilaya mbalimbali, vipaumbele vinavyotumika kwanza mazoezi yote yanaanza katika mchakato wa bajeti, na ndiyo maana mwaka huu ukiangalia tuna karibu Wilaya zipatazo 44, hizi ni Halmashauri na Wilaya mpya mbalimbali ambazo tumezipa fedha.
Hali kadhalika tunaangalia upungufu katika maeneo mbalimbali. Imani yangu kubwa ni kwamba suala la Kilolo limesikika na kwa sababu tuna Wilaya mpya na Halmashauri nyingine tunaendelea katika ujenzi wa miundombinu, tukifika katika mafungu yetu ya Mikoa utakuja kubainisha kwamba jinsi gani kila Mkoa katika mafungu yake yameweza kuelekezwa. Ile sehemu ambapo miundombinu haijakamilika lakini Wilaya ambazo ni mpya tunaanza kuziasisi tena upya, jinsi gani tume-allocate funds katika mwaka huu wa fedha ili tuweke hali halisi ya kuhakikisha kwamba wafanyakazi katika maeneo hayo waweze kufanyakazi katika mazingira rafiki.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA(MHE. GEORGE B. SIMBACHAWENE): Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana yaliyotolewa na Naibu Waziri Jafo, nilitaka tuelewane kwenye jambo hili la uanzishaji wa maeneo mapya ya utawala.
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni gumu na sote hapa tunafahamu kwamba maombi haya ya kuanzisha haya maeneo yanatokana na mahitaji ya wananchi. Lakini ni sisi wenyewe kwenye maeneo yetu ndiyo huwa tunaanzisha haya. Kwa kuwa maombi haya yanakuja mengi na wakati mwingine Serikali siyo rahisi sana kupata fedha kwa mara moja kujenga mahitaji yote ya Makao Makuu ya Halmashauri au Wilaya ni lazima tuvumiliane. Ni lazima tuvumiliane twende kidogo kidogo na ndiyo maana Serikali imekuwa ikitenga milioni 500, tunaamini tukifanya hivyo kwa miaka mitano, miaka minne, tunaweza tukakamilisha majengo yote.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuvumiliane kwa sababu Wabunge wengi wanakuja kuniona wakiwa na maombi mapya ya maeneo mengine ya utawala, sasa tukianza kuulizwa maswali kama kwa nini tunakuwa hatujajipanga na tunayaanzisha, kuna wengine hapa mmeahidi huko mlikotoka kwamba sisi tutahakikisha hapa panakuwa Mji Mdogo, sisi tutahakikisha tunakuwa na Halmashauri, sisi tutahakikisha tunakuwa na Wilaya.
Sasa tuvumiliane na tuende pamoja na tuamini kwamba kadri Serikali itakapopata uwezo tutakuwa tunafanya, lakini jambo hili ni gumu.