Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Primary Question

MHE. NAPE M. NNAUYE (K.n.y MHE. PROF. NORMAN A. S. KING) aliuliza:- Pamoja na juhudi nzuri zinazofanywa na Serikali kupeleka umeme vijijini:- Je, ni lini Vijiji 86 vya Wilaya ya Makete hususani Tarafa ya Ukwama, Lupalilo, Ikuwa, Matamba na Bulogwa watapatiwa umeme?

Supplementary Question 1

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini Mheshimiwa Naibu Waziri atakumbuka kwamba walipokwenda kuzindua REA III kwa Mkoa wa Iringa, walifanya assumption kwamba ndiyo wamezindua na Mkoa wa Njombe, lakini hii mikoa ni mikoa miwili tofauti, inawezekana TANESCO mnaona kama ni Mkoa mmoja lakini hii ni Mikoa miwili tofauti. Je, ni lini mtakwenda kuzindua REA III kwa Mkoa wa Njombe specific kwa Mkoa wa Njombe badala ya kuunganisha Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Iringa?
Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; vipaumbele vya kusambaza umeme wa REA III katika maeneo mengi, katika vijiji vimefanyiwa ofisini na Watendaji wa TANESCO bila kushirikisha viongozi kwenye maeneo husika na hasa kwa Mkoa wa Lindi hasa katika Jimbo la Mtama. Yapo maeneo mengi ukiangalia vijiji vilivyowekwa, vipaumbele vyake nadhani vimezingatiwa zaidi ofisini bila kujali hali halisi ya mazingira. Je, ni lini hawa Watendaji wa TANESCO pamoja na Wakandarasi watakaa na viongozi kwenye maeneo husika ili wakubaliane vipaumbele wapi tuanzie na wapi tuishie wakati wa awamu mbalimbali zinazoendelea za kusambaza umeme kwenye maeneo yetu? (Makofi)

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda sana kumpongeza Mheshimiwa Nape kwa jinsi ambavyo anatupa ushirikiano katika Jimbo lake la Mtama.
Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na suala la uzinduzi, tumefanya uzinduzi ambao kwa kweli katika miaka ya nyuma tulikuwa hatufanyi na mantiki kubwa ilikuwa ni kuwatambulisha Wakandarasi pia kuwajulisha viongozi pamoja na Waheshimiwa Wabunge ili waweze kushiriki ipasavyo kwenye zoezi zima. Kwa hiyo, nataka tu kusema kwamba, katika Jimbo la Mtama hata katika Mkoa wa Njombe, katika Mkoa wa Njombe kimsingi tulifanya uzinduzi Kesamgagao lakini kama ikibidi tutarudi.
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kazi yetu ni kuwafikishia umeme wananchi wa Njombe. Kwa hiyo, niseme tu kwamba wala halina shida, tutapanga siku na tutarejea ingawa Mkandarasi ameshafika site. Kwa hiyo, niwape faraja wananchi wa Njombe, tutaendelea kulifanyika kazi, watatualika tutakwenda pia kuwazindulia rasmi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na vipaumbele niseme tu, kazi ambayo Mkandarasi anatakiwa kuifanya na hili nitoe kama tangazo kwa Wakandarasi pamoja na TANESCO wanaowasimamia, utaratibu wa kwanza kwa Mkandarasi yeyote kabla hajaanza kazi anatakiwa kwanza awashirikishe Waheshimiwa Wabunge wa Majimbo husika na Viongozi wa maeneo hayo na kutofanya hivyo tutachukua hatua kali sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunafanya hivyo kwa sababu tunataka kuepuka vijiji muhimu kurukwa, maeneo ya vipaumbele kurukwa, pamoja na taasisi za umma. Kwa hiyo, nitoe angalizo, nakushukuru Mheshimiwa Nape lakini nachukua nafasi hii kuwatangazia rasmi kuwatangazia rasmi Wakandarasi pamoja na TANESCO kuhakikisha wanawashirikisha Waheshimiwa Wabunge, Madiwani na Viongozi wa maeneo husika ili kuhakikisha kwamba hakuna maeneo, vijiji wala taasisi za umma zitakazorukwa. Hilo ni angalizo nashukuru sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Nape wakati wa uzinduzi wa Lindi ni kweli hakuwepo lakini vijiji vyako vya Rondo Mheshimiwa vitapata umeme, Nyangamara watapata umeme, Chiwerewere watapata umeme, kwa hiyo bado Mheshimiwa Nape wananchi wake wa Mtama awape uhakika huo.