Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:- Uhitaji wa zao la pareto duniani ni mkubwa sana kiasi kwamba inahitajika kwa takribani tani 18,000 hadi 20,000 katika Soko la Dunia na Tanzania tuna uwezo wa kuzalisha hadi tani 8,000 tukiwa na mazingira rafiki. (a) Je, ni kwa misingi gani pareto imepangiwa mnunuzi mmoja tu wa kigeni huku ikiwafungia milango wanunuzi wadogo wa Kitanzania? (b) Je, Serikali inachukua hatua gani kusimamia bei ya zao hilo ambayo imeporomoka kutoka shilingi 2,400 katika kipindi cha wanunuzi wengi hadi shilingi 1,500 chini ya mnunuzi mmoja? (c) Je, Serikali ina mkakati gani wa muda mrefu na muda mfupi wa kuwawezesha wanunuzi wadogo wa Kitanzania kuingia kwenye ushindani na wanunuzi wageni?

Supplementary Question 1

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupewa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumshukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wa Wizara ya Kilimo kwa mkutano tuliofanya na wakulima na wawakilishi wa Wanunuzi mwishoni mwa mwaka 2016.
Mheshimiwa Spika, katika mkutano huo tulikubaliana kuwa wanunuzi wadogo wapewe leseni ya muda na vile vile wajiunge kwenye vikundi na pia hii Kampuni ya pareto ambayo ilikuwa imebinafsishwa kutoka Serikalini kulikuwa na asilimia 10 ambazo walipewa wakulima. Vilevile katika hicho kikao tulikubaliana kuwa zichunguzwe hizo asilimia kumi ziko kwa nani kwa vile wakulima hawakupewa hizo asilimia kumi.
Mheshimiwa Spika, pamoja na makubaliano yote hayo, hakuna hata kimoja kilichozingatiwa na leo hii kuna kampuni mpya mbayo imejenga kiwanda eneo la Inyara, Mbeya ambayo imezingatia vigezo vyote na ilipewa leseni ya kununua pareto kwenye vijiji viwili tu kati ya vijiji zaidi ya 20 vinavyolima pareto. Sasa ni kwa nini Serikali isiboreshe hii Bodi ya Pareto ili tuweze kuboresha kiwango cha zao la pareto?
Mheshimiwa Spika, nashukuru.
La pili vilevile nilitaka kupata uhakika wa Serikali, kwa sababu inavyoelekea hakuna ushindani sasa hivi, watatuhakikishia vipi ya kwamba hawa ambao wametimiza vigezo vyote wanaruhusiwa kununua pareto ili inunuliwe kwa ushindani? Ahsante sana.

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri kwamba Mheshimiwa Njeza amekuwa akifuatilia sana maslahi ya wakulima wake wa pareto, kahawa na mahindi. Kwa hiyo, tumekuwa naye karibu sana. Vilevile nikiri kwamba tulifanya kikao na wakulima, mkutano ambao ulitusaidia sana kupata makubaliano kuhusu namna bora ya kuendesha zao la pareto.
Mheshimiwa Spika, kutokana na mazungumzo yetu, baadhi ya masharti ambayo wakulima na wawakilishi wao tulikubaliana watekeleze, bado wako mbioni kutekeleza na hivyo bado tunasubiri kutoka kwao.
Mheshimiwa Spika, vile vile kuhusiana na leseni ya kampuni za kununua pareto; nilieleze tu Bunge lako Tukufu kwamba zao la pareto ni zao lenye masharti tofauti kidogo na mazao mengine kwa sababu tunachoruhusu kipelekwe nje siyo pareto ghafi, siyo maua, bali ni sumu ghafi. Katika maana hiyo, ili uweze kupeleka nje lile zao ni lazima uwe na kiwanda.
Mheshimiwa Spika, tunafanya hivyo kwa sababu huko nyuma wakati tulikuwa tunaruhusu kupeleka maua nje, kiwango cha pareto yetu kilishuka sana kwa sababu hatukuwa tunaweza kudhibiti ubora wa sumu inayopelekwa nje, ndiyo maana tukaleta ili kunusuru zao lisije likaanguka nchini. Tukaleta kigezo kwamba ni lazima uweze kuwa na kiwanda ili uweze kuzidua au kuchakata na kuwa sumu ghafi.
Kwa hiyo, kampuni yoyote ambayo imekidhi masharti hayo, katika hali ya kawaida tunaruhusu inunue pareto. Kampuni ambayo anaizungumzia ya TAN Extract ya Mbeya ambayo ndiyo imeingia tu sokoni na kutimiza masharti, tutaendelea kutoa leseni ili waweze kununua pareto maeneo mengine zaidi ya vijiji ambavyo wanatoa sasa.
Vilevile nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sasa hatujaona kwamba tatizo ni Bodi ya Pareto lakini ni kanuni na sheria ambayo tumewekeana wenyewe kama wadau na Serikali iko tayari kuirejea na kuangalia upya sheria na kanuni hizo kama itaonekana inafaa.

Name

Yahaya Omary Massare

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Manyoni Magharibi

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:- Uhitaji wa zao la pareto duniani ni mkubwa sana kiasi kwamba inahitajika kwa takribani tani 18,000 hadi 20,000 katika Soko la Dunia na Tanzania tuna uwezo wa kuzalisha hadi tani 8,000 tukiwa na mazingira rafiki. (a) Je, ni kwa misingi gani pareto imepangiwa mnunuzi mmoja tu wa kigeni huku ikiwafungia milango wanunuzi wadogo wa Kitanzania? (b) Je, Serikali inachukua hatua gani kusimamia bei ya zao hilo ambayo imeporomoka kutoka shilingi 2,400 katika kipindi cha wanunuzi wengi hadi shilingi 1,500 chini ya mnunuzi mmoja? (c) Je, Serikali ina mkakati gani wa muda mrefu na muda mfupi wa kuwawezesha wanunuzi wadogo wa Kitanzania kuingia kwenye ushindani na wanunuzi wageni?

Supplementary Question 2

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niulizes swali dogo la nyongeza.
Mheshimiwa Spika, matatizo yaliyopo huko Mbeya Vijijini yanafanana kabisa na matatizo waliyonayo wakulima wa Itigi. Wakulima wa Itigi wanalima mazao mbalimbali yakiwemo mazao ya biashara na mazao ya chakula, lakini wanategemea sana Kampuni hii ya Tanganyika Packers ambalo limetelekezwa na sasa wanalitumia. Mheshimiwa Naibu Waziri alifika pale na aliona hamasa ya wananchi kutaka shamba lile lirejeshwe kwa wananchi kupitia Halmashauri yao.
Je, ni lini sasa Wizara hii italirudisha shamba lile kwa wananchi kwa sababu kampuni hii inayolimiliki ilishafilisika?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati wa ziara yangu Itigi, niliona changamoto ya ardhi waliyokuwanayo wananchi, pamoja na kuwepo na shamba ambalo ni kama limetelekezwa na hivyo kuhitaji jitihada za kuangalia namna ya kuwapatia.
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari mchakato wa kuangalia namna ya kuligawa shamba hilo unaendelea. Wizara yangu kwa kushirikiana na Msajili wa Hazina inatayarisha waraka wa kwenda Baraza la Mawaziri ili hatimaye shamba hilo liweze kugaiwa kwa utaratibu ambao utaonekana unafaa ikiwa ni pamoja na kugawa kwa wafugaji na wakulima wa Itigi.