Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Primary Question

MHE. JOHN P. KADUTU (k.n.y. MHE. RICHARD P. MBOGO) aliuliza:- Mwaka 2009 Serikali iliwapa uraia wakimbizi toka Burundi walioingia nchini mwaka 1992 na wengine waliozaliana katika makambi ya wakimbizi ya Katumba, Mushamo na Ulyankulu:- (a) Je, ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kuwapa wakimbizi waliosalia? (b) Ili kuondoa hali ya sintofahamu katika Sheria ya Wakimbizi Na. 20 inayokataza mikusanyiko zaidi ya watu watano, je, ni lini Serikali itafuta hadhi ya makambi ya wakimbizi katika maeneo ya Katumba?

Supplementary Question 1

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza, je, Serikali iko tayari kuwahakikishia wananchi hawa ni lini wale ambao hawajaamua kubaki au kuondoka na kurudi Burundi? Kwa sababu siyo kweli kwamba watu wote wameshapata uraia; wako ambao hawajapata na hawajasema wanataka nini. Je, Serikali iko tayari kutoa tamko nini kifanyike?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna takribani wakimbizi 8,800 ambao hawajapatiwa uraia kati ya wale 162,000 na zaidi ya wale ambao walipatiwa uraia, lakini kulikuwa na sababu kadhaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa sababu hizo ni kwamba wengine ni watoto wa wakimbizi ambao walizaliwa baada ya wazee wao kupata uraia, lakini wakati ambapo Waziri wa Mambo ya Ndani alikuwa hajaidhinisha bado uraia. Wapo wengine ambao hawakupewa uraia; walinyimwa kwa sababu mbalimbali ikiwemo hali zao za uhalifu na mambo mengine ambayo hayakuweza kukidhi vigezo na sifa za kupata uraia nchini kwetu.
Mheshimiwa Spika, sasa ninachoweza kumwambia Mheshimiwa Mbunge ni kwamba kwa wale ambao hawakupata uraia na wamekidhi vigezo na wameomba uraia, maombi yao yanashughulikiwa na yatakapokuwa yamekamilika watapewa uraia kwa wale ambao watakuwa wamekidhi vigezo.