Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Primary Question

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA aliuliza:- Mradi wa REA umekuwa ukisuasua katika maeneo ya vijiji vya Rufiji hususan Tarafa ya Mkongo, Kata za Mkongo, Ngorongo, Kipungila na Kata ya Mwaseni na Ngarambe. Je, ni lini mradi huo utakamilika katika hatua inayofuata?

Supplementary Question 1

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli anasema kwamba msema kweli ndiyo mpenzi wa Mungu na mimi naomba niulize maswali ya kiukweli ukweli.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la umeme Rufiji ni takribani mwaka mmoja sasa tunapata umeme kwa saa nne tu kwa siku. Hali hii imesababisha vijana wa pale Ikwiriri kufunga viwanda vyao vidogo vya furniture kwa kuwa umeme wakati mwingine unakuja usiku. Naomba kufahamu kauli ya Serikali waliyoitoa kwamba nchi hii hakuna mgawo wa umeme, je, Rufiji siyo sehemu ya Tanzania? Hilo ni moja.
Swali la pili, wananchi hawa wa Rufiji hawana barabara hata robo kilometa, hawana maji, hawana hospitali hata X-ray machine hawana japokuwa wilaya hii ni ya zamani sana. Mchango wa Rufiji kwa Pato la Taifa ni asilimia 19 kutokana na hifadhi ya Taifa pamoja na misitu. Naomba kufahamu kwa nini Serikali inawachonganisha wananchi wa Jimbo la Rufiji na Chama chao cha Mapinduzi?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nampongeza sana Mheshimiwa Mchengerwa kwa maswali yake mazuri, lakini kwa jinsi anavyowawakilisha wananchi wa Rufiji. Mheshimiwa Mchengerwa hongera sana na wananchi wako nadhani watapata maendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijielekeze kwenye maswali mazuri ya nyongeza ya Mheshimiwa Mchengerwa. Suala la kukatikakatika kwa umeme, maeneo yanayopatiwa umeme kutoka Somanga Funga ambao ni mtambo unaosambaza umeme maeneo ya Rufiji pamoja na Kilwa, ni kweli kabisa kuna tatizo hilo. Kama nilivyowaeleza juzi mtambo wetu wa Somanga Funga ulikuwa na matatizo. Mtambo huu una vituo vitatu na mashine tatu za kuzalisha umeme, lakini mashine zilikuwa na matatizo ya uchakavu jambo ambalo tunalifanyia kazi na Serikali imetenga shilingi bilioni tatu kwa ajili ya ukarabati. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mchengerwa pamoja na wananchi wa Rufiji mtambo huo utarekebika na kukatika umeme kutaisha kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hata ule mtambo wa tatu ambao pia ulikuwa na hitilafu tunafunga sasa mtambo mwingine kwa ajili ya kuboresha uzalishaji wa umeme kwenye Mji wa Rufiji ambao unagharimu shilingi bilioni mbili. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mchengerwa na wananchi wake watapata umeme wa uhakika hivi karibuni. Nimhakikishie vijiji vyake vyote vya Luwe, Ngarambe, Ngombani, Kilimani A na B na Mashariki vyote vitapata umeme. Kwa hiyo, wananchi watapata umeme wa uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikiri kwamba Rufiji ni sehemu ya Tanzania kama vijiji vingine. Sasa nijibu swali la pili kwa nini Serikali inawachonganisha wananchi wa Rufiji na maeneo mengine, sidhani na sina uhakika Mheshimiwa Mchengerwa. Nikiri kwamba Serikali haiwachonganishi wananchi wa Rufiji na maeneo mengine. Japo swali lako linahusiana na masuala ya barabara, maji, umeme lakini kwa vile Serikali ni moja nimhakikishie kwamba Serikali ya Awamu ya Tano haiwachonganishi wananchi na Rufiji na maeneo mengine. Ahsante sana.