Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI K.n.y. MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI aliuliza:- Je, Serikali imefanya tathmini ya mafunzo wanayopatiwa vijana chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu baada ya kumaliza mafunzo?

Supplementary Question 1

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, vijana wanatofautiana katika sifa, makundi na mahitaji; je, ni kwa kiasi gani programu hizi zimezingatia changamoto hiyo?

Swali la pili, tumeona katika sekta ya elimu sasa tumekuja na mtaala mpya ambapo mafunzo ya stadi kwa maana ya amali yataanza katika ngazi ya msingi; je, katika hayo maboresho ambayo Serikali inakusudia kuyafanya Serikali iko tayari kuzingatia eneo hili la mtaala mpya wa elimu?

Name

Paschal Katambi Patrobas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Shinyanga Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rashid Shangazi ambalo kwanza ni kuhusiana na sifa na makundi mbalimbali ya vijana, jinsi ambavyo Serikali imeweka programu za kuweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali tumeweka programu mbalimbali kulingana na mtawanyiko wa makundi pia mikakati imewekwa kwa ajili ya kuangalia namna gani ambavyo vijana hawa wanaweza kufikiwa wote katika Taifa. Moja ya programu ambazo tumeziweka tumeangalia pia programu kisekta, kwa mfano kwenye sekta ya elimu, vijana walio wengi kama viongozi wa baadaye wa Taifa hili wamewekewa programu na Serikali ya kupewa msaada wa elimu bure au elimu bila malipo mpaka Kidato cha Sita na akimaliza Kidato cha Sita ataenda Chuo Kikuu ambako anakutana na mkopo na sasa Dkt. Samia Suluhu Hassan amefikisha mkopo wa elimu ya juu kufikia shilingi bilioni 734.

Mheshimiwa Mwenyekiti, programu nyingine ambayo ipo ya kisekta ni kwenye eneo la uchumi, biashara na uwekezaji. Hapo pia tuna Baraza la Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi, sambamba na hilo kwenye Halmashauri zetu tumeweka programu ya utoaji wa mikopo pia fursa za ajira na mitaji. Katika eneo hilo zile asilimia nne zinaenda kwa ajili ya vijana na watu wenye ulemavu lakini pia wanawake, wanasaidiwa hata awe amemaliza Chuo Kikuu au hayupo kwenye sekta ya kisomo anaweza akapata fedha zikamsaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye sekta ya madini, tumeenda kisekta katika Wizara kuangalia, sekta ya madini pia wapo wale wachimbaji wadogo wadogo vijana, nao wanawezeshwa huko kulingana na programu na miongozo ambayo tumeiweka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya kilimo pia tuna BBT LIFE ambayo ni Building Better Tommorrow kwa ajili ya kuwasaidia vijana waweze kujifunza namna ya kunenepesha mitamba ya ng’ombe na pia kufanya cage fishing na mafunzo mengine yanayoendana na masuala ya uchumi wa bahari. Zaidi ya hapo kwenye kilimo tuna vijana, tuna BBT LIFE ambayo ni kilimo biashara. Mafunzo yanaendelea na zaidi ya vijana 800 walikuwa wanufaika na programu hizi ni endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sekta nyingine ya ajira na kazi, tuna kitengo maalum cha ajira kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu cha TAESA, ambapo vijana wanaomaliza vyuo vikuu wanaenda kwa ajili ya mafunzo ya utayari kazini. Pia tuna programu za ukuzaji ujuzi, tuna programu za wanagenzi, zote hizi zinalenga kuwagusa vijana kwenye makundi mbalimbali. Zipo pia programu kwenye sekta ya michezo na sekta nyingine kwa sababu ya muda, lakini uone jinsi gani Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan imewaangalia vijana katika maeneo yote. Hata wale ambao wana-aspire kwenye uongozi wa Taifa kwenye maeneo ya siasa, vyama vya siasa tumefanya mabadiliko ya Sheria hapa kwamba vijana waangaliwe pia katika kupewa fursa kwenye vyama vyao na kuweza kupata fursa za uongozi. Ahsante. (Makofi)