Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Venant Daud Protas

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igalula

Primary Question

MHE. VENANT D. PROTAS aliuliza:- Je, lini Serikali itapeleka Askari na kulipa fidia kwa Wananchi waliovamiwa na Tembo kwenye makazi na mashamba yao Jimbo la Igalula?

Supplementary Question 1

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu ya Serikali naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Kumekuwa na wimbi kubwa la tembo kuvamia makazi ya watu na mashamba, lakini kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kuna askari wanatokea Ngara. Tumekuwa tukitoa taarifa ya uvamizi wa tembo huwa inachukuwa zaidi ya siku mbili mpaka nne kwenda kutatua tatizo hilo.

Mheshimiwa Spika, je, Serikali mtanipa lini askari watakao kaa katika Jimbo la Igalula siyo hao wa Ngara na siwajui na sijawahi kuwaona?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, tumekuwa na uvamizi na uharibifu wa mali za wananchi na mwaka jana tulikwenda kufanya tathmini wananchi zaidi ya hao 17 walivamiwa na uharibifu mkubwa. Lini mtawalipa fidia wananchi waliopata athari hizo? Nakushukuru sana. (Makofi)

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Venant Daud Protas, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli nchi yetu imekuwa na wimbi kubwa la matukio ya wanyama wakali na waharibifu kushambulia maeneo ya wananchi wetu. Serikali imekuwa ikijitahidi kuhakikisha kwamba pale tunapopata taarifa tunawatuma askari wetu kwa haraka kwenda kusaidia kukabiliana na changamoto hizi.

Mheshimiwa Spika, sasa tathmini iliyokuwa imefanyika ilionekana kabisa askari hawa tuliokuwa nao kwenye eneo lile wana uwezo wa kushughulikia jambo hili, lakini kwa sababu ya concern ya Mheshimiwa Mbunge baada ya kikao hiki cha leo nitakaa nae tuweze kuona ni jinsi gani tunaweza kushirikiana na halmashauri kutoa mafunzo kwa maafisa wanyama pori wa vijiji ili waweze kushirikiana na wale wa Serikali kuondokana na changamoto iliyopo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuwalipa hawa wananchi ambao wamepata madhara haya kama nilivyosema kwenye jibu la msingi tuko kwenye hatua za mwisho za kufanya tathmini ili tuweze kuwalipa. Tathmini hii ikikamilika nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wale watakaostahili kulipwa watapata malipo yao kwa wakati.