Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions

Name

Nusrat Shaaban Hanje

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NUSRAT S. HANJE aliuliza: - Je, Serikali imetekeleza kwa kiwango gani Mkakati wa Afrika wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STISA – 2024) kufuatia maendeleo makubwa ya sayansi, teknolojia na ubunifu duniani?

Supplementary Question 1

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa tunafahamu wote kama Taifa hatuna Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu lakini pia Sheria ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) imepitwa na wakati.

Je, Maonesho ya kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu MAKISATU yanatekelezwa kwa sera ipi?

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Wizara ya Habari, Mawasiliano ya Habari na Teknolojia ya Habari yote yana masuala ya teknolojia jambo ambalo linasababisha tushindwe kuelewa nani hasa mhusika wa masuala ya teknolojia kwenye Taifa letu. Je, Wizara ipo tayari sasa kuanza kuishauri Serikali kwa vielelezo hatua kwa hatua waanzishe Wizara mpya ambayo itashughulika na masuala ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu; ukizingatia mabadiliko ya sayansi na teknolojia ulimwenguzi lakini mapinduzi ya nne ya viwanda kama ilivyo nchi za Kenya, Afrika Kusini na Rwanda? (Makofi)

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Shaaban Hanje kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Nusrat kwa ufuatiliaji wake wa karibu wa masuala ya sayansi, teknolojia na ubunifu, lakini kipekee nichukue fursa hii kuwapongeza Wabunge wote ambao waliweza kufika na kutembelea kwenye mashindo yetu ya MAKISATU ambayo yalianza tarehe 16 – 20 Mei, 2022 katika Uwanja wetu wa Jamhuri pale Dodoma.

Mheshimiwa Spika, naomba nimtuoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba dhana hii ya utekelezaji wa mashindano hayo ya MAKISATU ni msimamo au ufuatiliaji wa karibu wa Serikali kuhakikisha kwamba mashindano haya au ubunifu nchini unaweza kuimarishwa.

Mashindano haya yanatekelezwa kwa mujibu wa sera ya ubunifu ya mwaka 1996. Tunakiri kuna mapungufu machache kwenye sera hii, lakini ndio ambayo tunazingatia katika utekelezaji wa mashindano haya.

Mheshimiwa Spika, lakini kama nilivyozungumza katika kipindi kilichopita kwamba, sera hii tunakwenda kuifanyia maboresho makubwa, lakini naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kupitia mashindano haya tumeweza kuibua bunifu zaidi ya 1,785, lakini vilevile zaidi ya bunifu 200 zimeweza kuendelezwa na zaidi ya bunifu 26 zimeweza kuingia sokoni kuona namna gani Serikali inasimamia kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali lake la pili anazungumzia suala la Wizara ya Elimu pamoja na Wizara ya Habari kuwa na suala hili la teknolojia. Ni kweli, tunaomba tukiri kwamba, Wizara ya Habari na Wizara ya Elimu zote zina teknolojia ndani, lakini utekelezaji wa teknolojia hii unategemea na mawanda yale ambayo Wizara imepewa kupitia hati idhini ya uanzishwaji wa Wizara husika.

Mheshimiwa Spika, kwa vile ametoa ushauri namna gani sasa Serikali inaweza kutenganisha maeneo haya ya ubunifu na Wizara hizi; basi tubebe ushauri huo, twende tukaufanyie tathmini na tuweze kuufanyia kazi ili tuweze kuona namna gani tunaweza tukatekeleza.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Name

Fatma Hassan Toufiq

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NUSRAT S. HANJE aliuliza: - Je, Serikali imetekeleza kwa kiwango gani Mkakati wa Afrika wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STISA – 2024) kufuatia maendeleo makubwa ya sayansi, teknolojia na ubunifu duniani?

Supplementary Question 2

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Ugunduzi na ubunifu ni miongoni mwa nyanja muhimu sana katika ukuzaji uchumi na maendeleo. Nini mkakati wa Serikali katika kuendeleza ugunduzi na ubunifu katika nyanja za vijijini na hasa kwa wanawake?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika majibu yangu ya msingi kwamba, kwanza tuna sera ya namna gani ubunifu na ugunduzi unasimamiwa au unaratibiwa katika maeneo yote. Katika kulisimamia hilo, Serikali baada ya kuona hii sera mwaka 2018 tumeandaa mwongozo wa namna gani masuala haya ya ubunifu yanaweza kusimamiwa na kuratibiwa kuanzia ngazi ya vijiji, kata, Tarafa, Wilaya, mpaka kufika katika ngazi ya Taifa ambako huko watu wote tunaweza tukawakuta.

Mheshimiwa Spika, ukitaka kuangalia kwa umakini kabisa katika mashindano yetu haya ya MAKISATU yameweza kubeba makundi yote, kuna makundi karibu saba tumeweza kuyazingatia tunapokwenda kuwagundua wagunduzi wetu au watafiti wetu katika maeneo yote ya vijijini mpaka katika ngazi ya Taifa. Kwa hiyo, katika eneo hili na wanawake vilevile wanaingia kwa namna moja au nyingine.

Mheshimiwa Spika, Nakushukuru sana.

Name

Prof. Patrick Alois Ndakidemi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Vijijini

Primary Question

MHE. NUSRAT S. HANJE aliuliza: - Je, Serikali imetekeleza kwa kiwango gani Mkakati wa Afrika wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STISA – 2024) kufuatia maendeleo makubwa ya sayansi, teknolojia na ubunifu duniani?

Supplementary Question 3

MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa. Je, Serikali ina mkakati gani kusaidia wabunifu kuhatamia teknolojia zao au ku-incubate wakati wakijiandaa kuanzisha viwanda vidogo vidogo?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa kaka yangu, Profesa Ndakidemi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimejibu katika majibu yangu ya nyongeza kwenye maswali yaliyopita kwamba, katika kipindi cha miaka minne iliyopita Serikali ilianzisha mashindano ya MAKISATU ambayo tulianza mwaka 2019 na mwaka huu sasa ni awamu ya nne. Katika mashindano haya zaidi ya bunifu elfu moja mia saba na themanini na kitu yaliweza kuibuliwa na zaidi ya bunifu 200 zimeweza kuendelezwa au kuatamiwa na zaidi ya bunifu 26 tayari zimeshapelekwa sokoni, sasa kitu gani tunachofanya?

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwapata hawa wagunduzi au wabunifu tunawapeleka kwenye zile hub zetu, tuna center mbalimbali nchini kote ambazo zinawalea na Serikali sisi tumeweza kupeleka fedha katika maeneo haya. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tumeweza kupandisha bajeti ya kuwalea hawa wabunifu wetu kutoka bilioni 3.0 mpaka bilioni 9.0 katika mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali tayari imeshafanya eneo leke na katika kipindi hiki hizi bunifu tulizozipata katika mashindano haya yaliyopita, zaidi ya milioni 700 tumeshazipeleka tayari kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, hawa tunakwenda kuwaendeleza ili bunifu hizi ziende kuwa biashara na bidhaa ambayo tunaweza tukaipeleka sokoni.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.