Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 45 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 385 2016-06-17

Name

Zubeda Hassan Sakuru

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HALIMA A. BULEMBO (K.n.y. MHE. ZUBEDA H. SAKURU) aliuliza:-
Kumekuwa na ongezeko kubwa la matukio ya kihalifu nchini yanayohusishwa pia na upatikanaji wa hati za kusafiria zaidi ya moja zinazotolewa hapa Tanzania kwa baadhi ya wahalifu kiholela:-
Je, Serikali inachukua hatua gani katika udhibiti wa utoaji hati za kusafiria kiholela?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zubeda Hassan Sakuru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Idara ya Uhamiaji hutoa Pasipoti na Hati za Kusafiria kwa raia yeyote wa Tanzania kwa mujibu wa Sheria ya Pasipoti na Hati za Kusafiria Na. 2 ya mwaka 2002 ili mradi amekidhi matakwa ya sheria hiyo. Pasipoti na Hati za Kusafiria hazitolewi kiholela kwa wahalifu kama Mheshimiwa Mbunge alivyouliza.
Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kutolewa Pasipoti au Hati ya Kusafiria, Idara ya Uhamiaji hufanya uchunguzi wa kujiridhisha kama mwombaji ni raia wa Tanzania na kama hana makosa kihalifu. Serikali kupitia Idara ya Uhamiaji huchukua hatua zifuatazo ili kudhibiti utoaji holela wa Pasipoti pamoja na Hati za Kusafiria:-
(i) Kuwasiliana na idara mbalimbali ili kujiridhisha nyaraka zilizoambatishwa kwenye ombi la Pasipoti au Hati za Kusafiria mfano RITA;
(ii) Kuchukua hatua za kisheria na za kinidhamu kwa watumishi wanaobainika kujihusisha katika utoaji wa Pasipoti au Hati za Kusafiria kwa kukiuka sheria, kanuni na taratibu;
(iii) Kuweka masharti katika utoaji wa Hati za Kusafiria kwa mwombaji aliyeibiwa au kupoteza Hati za Kusafiria;
(iv) Kuwachukulia hatua za kisheria waombaji wa Pasipoti wanaotumia njia za udanganyifu;
(v) Kutuma taarifa za Pasipoti zilizopotea au kuibiwa kwenye Shirika la Polisi la Kimataifa (Interpol) ili kuwakamata wahusika;
(vi) Kuimarisha mfumo wa utunzaji wa kumbukumbu na takwimu za Watanzania walioomba na kupewa Pasipoti Makao Makuu ya Uhamiaji; na
(vii) Kuweka mfumo wa kielektroniki wa utoaji Pasipoti ili kuweza kutambua watu kwa usahihi na kuondokana na tatizo la kughushiwa kwa Pasipoti.
Mheshimiwa Naibu Spika, Idara ya Uhamiaji pia hufuta Pasipoti za watu ambao wamepatikana na hatia za makosa ya biashara ya madawa ya kulevya, utakatishaji fedha, usafirishaji haramu wa binadamu, vitendo vya kigaidi au hata shughuli yeyote haramu kwa mujibu wa Sheria ya Pasipoti na Hati ya Kusafiria Na. 20 ya mwaka 2002.