Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 45 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 381 2016-06-17

Name

Rashid Mohamed Chuachua

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Masasi Mjini

Primary Question

MHE. RASHID M. CHUACHUA aliuliza:-
Sera ya Serikali ya kujenga zahanati kwa kila kijiji na kituo cha afya kwa kila kata haijatekelezwa vyema katika Jimbo la Masasi ambapo hakuna kata yenye kituo cha afya cha Serikali na zahanati zilizopo ni saba tu:-
(a) Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa zahanati na vituo vya afya katika kata 14 za Jimbo la Masasi?
(b) Je, Serikali inaweza kukiri kuwa kuna haja ya kuzipandisha hadhi Zahanati za Chisegu, Mumbaka na Mwenge Mtapika ili ziwe na vituo vya afya na hatimaye kuipunguzia mzigo Hospitali ya Mkomaindo pamoja na kusogeza huduma kwa jamii?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Mohamed Chuachua, Mbunge wa Masasi Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa zahanati kila kijiji, vituo vya afya kila kata na hospitali kila wilaya unafanywa na Halmashauri kwa kushirikisha nguvu za wananchi kupitia Mpango wa Fursa na Vikwazo kwa Maendeleo (O&OD - Opportunity and Obstacle to Development). Kazi hii inafanyika kwa awamu katika Halmashauri zote, kulingana na bajeti iliyotengwa kila mwaka. Halmashauri ya Wilaya ya Masasi katika mwaka wa fedha 2015/2016 imeweka kipaumbele katika ujenzi wa zahanati ya Namatunu, Makarango, Mtaa wa Silabu ambao unaendelea. Aidha, katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2016/2017 zimetengwa shilingi milioni 70 kwa ajili ya umaliziaji wa zahanati hizo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya na Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto, inafanya tathmini ya miradi ya zahanati na vituo vya afya ambavyo havijakamilika pamoja ili kubaini vijiji na hata ambazo hazina miundombinu hiyo ili kujua gharama halisi zinazohitajika kumaliza miradi hiyo au kuanza ujenzi mpya.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kupandisha zahanati kuwa vituo vya afya, Halmashauri imeshauriwa kuanzisha mchakato huo kupitia vikao na kuwasilisha mapendekezo hayo, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto ili kupata kibali.