Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 34 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 279 2016-06-01

Name

Dr. Dalaly Peter Kafumu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Igunga

Primary Question

MHE. DKT. DALALY P. KAFUMU aliuliza:-
Mbuga ya Hifadhi ya Wembere ni mbuga iliyotelekezwa na Serikali na kupoteza sifa za kuendelea kuwa hifadhi na sasa inatumika na wafugaji kulisha mifugo na wakulima kulima alizeti na mpunga kwenye eneo hilo.
Je, ni kwa nini Serikali isibadilishe matumizi ya mbuga hiyo badala yake ipimwe na kutumika kwa wafugaji na wakulima na kuondoa migogoro inayoendelea kati ya wakulima na wafugaji ambayo wakati mwingine inasababisha mauaji na uharibifu wa mali?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Dalaly Peter Kafumu, Mbunge wa Igunga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mbuga ya Wembere ipo ndani ya mipaka ya mikoa ya Tabora na Singida. Umuhimu wa eneo hili ni pamoja na kuwa chanzo cha maji yanayokwenda katika maziwa Eyasi na Kitangire. Mbuga hiyo pia ni maarufu kwa aina (species) za mimea na wanyamapori mbalimbali na muhimu kwa mazalia ya ndege mbalimbali wenye sifa za Kitaifa na Kimataifa. Eneo hilo linatambuliwa Kimataifa kama mahsusi kwa kundi muhimu la uhifadhi wa ndege duniani tangu mwaka 2001.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwa eneo hilo linakabiliwa na changamoto ya uvamizi kwa shughuli za kilimo na ufugaji kama alivyobainisha Mheshimiwa Mbunge, bado Serikali haijaitelekeza mbuga hiyo na kinyume chake eneo hilo linatumika kwa shughuli za uwindaji wa kitalii ambapo linaliingizia Taifa fedha za kigeni na kutoa ajira kwa wananchi waishio kando ya eneo hilo. Kwa mfano, katika kipindi cha mwaka 2013/2014 hadi 2015/2016 Serikali imepata kiasi cha dola za Kimarekani 142,450 kutokana na shughuli za uwindaji katika vitalu vilivyoko ndani ya eneo hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhimu kiikolojia wa eneo hilo Kitaifa na Kimataifa Wizara yangu itaendeleza majadiliano na Serikali ya Mkoa wa Tabora na Singida ili kuona uwezekano wa kupandisha hadhi eneo hilo ili kuwa na uhifadhi endelevu wa bioanuai zilizopo.