Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 6 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 89 2023-09-05

Name

Mussa Ramadhani Sima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Mjini

Primary Question

MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha maslahi ya Wathibiti Ubora wa Walimu nchini ili kuinua ubora wa elimu?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima, Mbunge wa Singida Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanza kutekeleza Muundo mpya wa Utumishi wa Maafisa Udhibiti Ubora wa Shule kuanzia Julai, 2023 ambao unatoa maslahi na motisha kwa Maafisa Udhibiti Ubora wa Shule kwa kuwaongezea Mishahara na kuwabadilishia ngazi ya mishahara kutoka TGTS kuwa TGQS. Hii ina maana kuwa kwa sasa mwalimu atakayeteuliwa kuwa Mdhibiti Ubora lazima awe amefikia ngazi ya mshahara ya TGTS G pamoja na sifa nyingine za uteuzi wa viongozi wa elimu kwa kuzingatia mwongozo wa uteuzi. Aidha, maslahi mengine ni kuongeza ukomo wa ngazi ya mshahara toka TGTS I hadi TGQS J yenye maslahi makubwa kuliko awali. Muundo huo umetambua majukumu makubwa ya Wadhibiti Ubora wa Shule.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuboresha mazingira ya utendaji kazi ya Wadhibiti Ubora wa Shule, Serikali imefanikiwa kutoa vifaa mbalimbali vya TEHAMA kwa Wadhibiti Ubora wa Shule Tanzania Bara, ambapo vishikwambi 1,680 vilitolewa kwa Maafisa Udhibiti Ubora wa Shule, photocopia 234, kompyuta za mezani 769, printer 450 na kompyuta mpakato (laptops) 1,002.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika kipindi cha mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imefanikiwa kujenga ofisi tano za Wadhibiti Ubora wa Shule katika Halmashauri za Wilaya ya Njombe, Tarime, Bunda, Ubungo, na Nyasa na hivyo kufanya au kuwezesha halmashauri 181 kuwa na ofisi. Lengo ni kuimarisha mazingira ya kufanyia kazi, nakushukuru.