Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 6 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 81 2023-09-05

Name

Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Primary Question

MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza:-

Je, nini mkakati wa Serikali kuvifanya vivutio vya mapango ya Handebezya na jiwe linalocheza kuwa na tija kwa Taifa?

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutekeleza mikakati mbalimbali inayolenga kuendeleza, kukuza na kutunza vivutio vya utalii vilivyopo Ukerewe vikiwemo Mapango ya Handebezya na Jiwe linalocheza vinavyopatikana katika Kisiwa cha Ukerewe. Mikakati hiyo ni pamoja na kutangaza vivutio hivyo kwa kutumia vyombo mbalimbali vya habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, mathalan, Wizara kupitia TTB iliratibu ziara ya Kituo cha Televisheni cha ITV kwenda kutembelea baadhi ya vivutio vya utalii vilivyopo Ukerewe vikiwemo Mapango ya Handebezya na jiwe linalocheza kwa ajili ya kuandaa documentary ambayo itakapokamilika itaonyeshwa katika kipindi cha ITV cha Chetu ni Chetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mafunzo yanaendelea kutolewa kuhusu uanzishwaji wa utalii wa utamaduni ambapo hadi sasa kuna vikundi vya utalii wa utamaduni vikiwemo Ukerewe (Ukerewe Cultural Tourism Enterprises) na Nansio (Nansio Cultural Tourism Enterprises).

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Maliasili na Utalii imeendelea kushiriki katika maonesho na matamasha mbalimbali yakiwemo Maonesho ya Biashara ya Afrika Mashariki na Tamasha la Bulabo yanayofanyika katika Kanda ya Ziwa kwa lengo la kutangaza vivutio vya utalii na fursa za uwekezaji zilizopo katika ukanda huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Wizara itaendelea kuhamasisha uwekezaji wa miundombinu inayoelekea katika maeneo yenye vivutio vya utalii, ujenzi wa huduma za malazi zenye hadhi pamoja na kuboresha huduma za kijamii, ikiwemo maji, umeme, huduma za kibenki na mawasiliano.