Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 11 Sitting 31 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 405 2023-05-23

Name

Issa Ally Mchungahela

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Primary Question

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA aliuliza: -

Je, lini Serikali itamaliza tatizo la umeme Mkoani Mtwara hususani Wilaya ya Masasi na Jimbo la Lulindi?

Name

Stephen Lujwahuka Byabato

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukoba Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Lulindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Masasi inapata umeme kutoka katika Kituo cha Kuzalisha Umeme kwa Kutumia Gesi cha Mtwara chenye uwezo wa megawati 30.4 na pia umeme wa Gridi ya Taifa kupitia njia ya msongo wa kilovoti 33 kutokea Songea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya umeme Mkoani Mtwara, Wilayani Masasi ikiwemo Jimbo la Lulindi inatokana na Umeme mdogo usiotosheleza (low voltage) kwenye baadhi ya maeneo ya Wilaya hiyo kwa sababu ya umeme kusafiri umbali mrefu, uchakavu wa miundombinu hasa nguzo na vikombe pamoja na uharibifu kwenye miundombinu ya njia ya msongo wa kilovoti 132 unaotokana na watoto kupiga manati vikombe katika baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondoa tatizo hili Serikali kupitia TANESCO imetenga shilingi bilioni mbili ili kujenga njia ya kutoka Nanganga hadi Masasi. Aidha, ufungaji wa Auto Voltage Regulator (AVR) mpya yenye ukubwa wa MVA 20 kati ya Tunduru na Namtumbo unaendelea ili kuwezesha umeme wa kutosha kutoka Ruvuma kufika Masasi na maeneo ya jirani. Pia, kwa kutumia Shilingi Milioni 600 Serikali inaendelea kubadili vikombe vilivyopasuka na kuweka vya plastiki na nguzo za miti zilizooza zinabadilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuwa na ufumbuzi wa kudumu wa tatizo la umeme katika Mkoa wa Mtwara, Serikali imepanga kuunganisha Mkoa wote na Gridi ya Taifa kupitia miradi miwili ya Gridi Imara ambayo ipo katika hatua za utekelezaji. Miradi hii ni ujenzi wa njia kuu ya umeme ya msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Tunduru na kutoka Tunduru hadi Masasi. Ahsante.