Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 48 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 416 2016-06-22

Name

Anna Richard Lupembe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:-
Wakazi wa Kichangani katika Wilaya ya Mpanda Mjini hawajawahi kupata hati kwa ardhi wanayomiliki:-
Je, ni lini wananchi wa maeneo hayo watapatiwa hati zao hasa ikizingatiwa kuwa zimechukua muda mrefu sana na haijulikani hatma yao ni nini?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali Na. 416 la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, umilikishwaji wa viwanja katika eneo la Kichangani katika Wilaya ya Mpanda ulifanyika kwenye maeneo ambayo upimaji wake ulikuwa bado haujakamilika. Ili wananchi hao waweze kupewa hatimiliki taratibu za upimaji wa maeneo hayo zinapaswa kukamilishwa kwanza.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu huu umekuwa ukifanywa na Halmashauri nyingi hapa nchini na ulilenga kupunguza mfumuko wa makazi holela mijini. Hata hivyo, baada ya Wizara yangu kubaini kuwa kuna maeneo mengi nchini ambayo yamemilikishwa bila upimaji wake kukamilika hivyo kuwakosesha haki na fursa wananchi kupata hati kutokana na upimaji kutokamilika. Wizara yangu imeingilia kati na kuzitaka Halmashauri zote nchini kuainisha maeneo yote ambayo yako katika demarcation ili upimaji wake ukamilike.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Wizara yangu tayari imetangaza zabuni kwa ajili ya kukamilisha upimaji huo na wazabuni mbalimbali wameshawasilisha zabuni na kufanya kazi hiyo na taratibu za kumpata mzabuni mwenye sifa zinaendelea. Aidha, tunapenda kutoa wito kwa Halmashauri zote nchini ikiwemo Wilaya ya Mpanda kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha upimaji ambao haujakamilika katika maeneo yao yote ambayo yataguswa katika mpango huu wa Wizara.