Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 1 Water and Irrigation Wizara ya Maji 5 2016-09-06

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Primary Question

MHE. CAPT. MST. GEORGE H. MKUCHIKA aliuliza:-
Mradi wa Maji wa Makonde ulijengwa mapema miaka ya 1950 kwa lengo la kuondoa kero ya maji katika uwanda wa Makonde wenye Wilaya za Newala, Tandahimba na sasa Mtwara Vijijini; lakini mradi huu mitambo yake imechakaa na watumiaji wameongezeka ambapo upatikanaji wa maji kwa Wilaya ya Newala ni 31% tu.
Je, Serikali inalifahamu tatizo hilo na inachukua hatua gani kutatua tatizo hili?

Name

Eng. Isack Aloyce Kamwelwe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Katavi

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI NA UMWAGILIAJI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji na Umwagiliaji naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Huruma Mkuchika, Mbunge wa Newala Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua tatizo la upatikanaji wa maji katika maeneo mengi hapa nchini likiwemo eneo linalohudumiwa na Mradi wa Maji ya Kitaifa wa Makonde.
Mheshimiwa Spika, katika mpango wa muda mfupi mwaka 2015/2016 Serikali kwa kushirikiana na shirika la DFID kutoka Uingereza ilikamilisha ukarabati wa visima virefu sita eneo la Mitema na kufunga pampu katika visima hivyo. Kukamilika kwa kazi hizo kumeongeza uzalishaji wa maji kutoka lita milioni 7.4 hadi lita milioni 14.8 kwa siku, hivyo kuongeza huduma ya maji katika baadhi ya maeneo yanayohudumiwa na Mradi wa Makonde.
Mheshimiwa Spika, katika mpango wa muda mrefu, Serikali kupitia Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji ilifanya upembuzi yakinifu na usanifu wa Mradi wa Kitaifa wa Makonde na kugundua kuwa chanzo cha Mitema katika Bonde la Mambi kina maji ya kutosha ya kuweza kuhudumia wananchi wa maeneo mbalimbali ya Wilaya za Nanyamba, Tandahimba pamoja na Newala.
Mheshimiwa Spika, kupitia mkopo wa masharti nafuu wa dola za Marekani milioni 500 kutoka Serikali ya India, Mradi wa Makonde umetengewa dola za Marekani milioni 87.41 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa mradi huo. Aidha, wakati mradi mkubwa ukisubiriwa Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni mbili katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya Mradi wa Kitaifa wa Makonde.