Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 23 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 201 2022-05-16

Name

Priscus Jacob Tarimo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. PRISCUS J. TARIMO aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kusaidia Halmashauri zinazozunguka Mbuga na Hifadhi kwa kutoa CSR kwenye mapato ya utalii?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kupitia utekelezaji wa Sera ya Uwajibikaji Kijamii (Community Social Responsibility - CSR), Serikali inatekeleza miradi ya ujirani mwema kwa jamii zinazozunguka maeneo yaliyohifadhiwa zikiwemo Hifadhi za Taifa, Mapori ya Akiba, Mapori Tengefu na Hifadhi za Wanyamapori za Jamii (WMAs). Katika kutekeleza Sera hiyo, Halmashauri za Wilaya pamoja na jamii zinazozunguka maeneo yaliyohifadhiwa, zinanufaika na mapato yanayotokana na utalii ikiwemo kupatiwa miradi mbalimbali ya kijamii inayoibuliwa na wananchi kwenye sekta mbalimbali ikiwemo Sekta ya Afya, Sekta ya elimu, Sekta ya Maji na Sekta ya Ujenzi. Miradi hii hutekelezwa na Taasisi za Uhifadhi nchini ambazo ni TANAPA, TAWA na NCAA.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Uwindaji wa Kitalii, Serikali pia imekuwa ikitekeleza Sheria ya Kuhifadhi Wanyamapori Na.5 ya 2009 ambayo inaelekeza kuwa asilimia 25 ya fedha zinazotokana na ada za wanyamapori waliowindwa katika vitalu vya uwindaji wa kitalii zirudishwe kwenye halmashauri zinazopakana na maeneo ya uwindaji. Aidha, katika maeneo ya WMAs, Kanuni za WMAs za mwaka 2018 zinaelekeza kuwa asilimia 75 ya ada ya kitalu, asilimia 55 ya ada ya wanyamapori wanaowindwa na asilimia 45 ya gharama za uhifadhi zinazotokana na uwindaji wa kitalii zirudishwe kwa jamii inayomiliki maeneo husika. Wizara imekuwa ikitekeleza matakwa haya kupitia TAWA. Ahsante.