Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 23 Water and Irrigation Wizara ya Maji 199 2022-05-16

Name

Maryam Azan Mwinyi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Chake Chake

Primary Question

MHE. MARYAM AZAN MWINYI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakomesha shughuli za ukataji miti, kilimo na ujenzi karribu na vyanzo vya maji ili kulinda vyanzo vya maji?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali za Maji Na.11 ya mwaka 2009. Katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imekamilisha uandaaji wa Mipango ya Muda Mrefu ya Kuhifadhi Vidakio vya Maji (Catchment Conservation Plans) katika mabonde yote tisa nchini. Mipango hiyo imeweka dira, vipaumbele na utaratibu mzuri wa utunzaji wa vyanzo vya maji katika maeneo ya vidakio vya maji na mipango hiyo itatekelezwa hadi mwaka 2035.

Mheshimiwa Spika, Serikali katika kuhakikisha inakomesha shughuli za ukataji miti kilimo na ujenzi karibu na vyanzo vya maji, hadi sasa jumla ya vyanzo vya maji 191 vimewekewa mipaka ikiwa ni hatua za kuzuia shughuli za kibinadamu katika vyanzo hivyo na vyanzo 44 vipo katika hatua ya kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali ili vilindwe kisheria. Vilevile, jumla ya Jumuiya za Watumia Maji 162 zimeanzishwa katika maeneo ya vyanzo vya maji ili kuwashirikisha wananchi katika shughuli za utunzaji wa vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, elimu ya utunzaji wa vyanzo vya maji itaendelea kutolewa kwa wananchi ili wafanye shughuli za kiuchumi katika maeneo ambayo hayana athari kwa vyanzo vya maji na mazingira kwa ujumla.