Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 10 Sitting 7 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 104 2023-02-08

Name

Martha Festo Mariki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARTHA F. MARIKI aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kutatua changamoto ya uhaba wa walimu katika shule za pembezoni?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Festo Mariki, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikitoa ajira ili kukabiliana na upungufu wa walimu shuleni, unaotokana na walimu kustaafu, kuacha kazi, kufukuzwa, kufariki na ongezeko la idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa. Tangu mwaka 2018/2019 hadi mwaka 2021/2022, Serikali imeajiri jumla ya walimu 26,598 wakiwemo walimu 16,640 wa shule za msingi na walimu 9,958 wa shule za sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina hakikisha walimu wanaajiriwa na kupangwa katika shule zenye uhitaji zaidi, hususan zilizoko maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2020 Ofisi ya Rais – TAMISEMI iliboresha mfumo maalum wa maombi ya ajira na upangaji wa walimu ujulikanao kama Teachers Allocation Protocol. Kupitia mfumo huo, shule zenye upungufu mkubwa wa walimu hususan zilizoko vijijini hubainishwa, ambapo walimu huomba ajira moja kwa moja kwa kuchagua shule husika iliyopo katika mfumo. Aidha, Ofisi ya Rais – TAMISEMI imetoa maelekezo kwa Makatibu Tawala wa Mikoa yote Tanzania Bara kufanya msawazo wa walimu kutoka shule zenye ziada na kuwapeleka katika shule zenye upungufu zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuajiri walimu kulingana na mahitaji na upatikanaji wa fedha ili kukabiliana na uhaba wa walimu hususani katika maeneo ya pembezoni.