Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 26 Radio and Television Broadcasting Services Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 215 2016-05-23

Name

Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Primary Question

MHE. MARTIN M. MSUHA aliuliza:-
Wananchi wa Tarafa za Hagati, Mbuji na Mkumbi hawapati matangazo ya Redio ya TBC kutokana na Kituo cha TBC- Songea kutokuwa na uwezo wa kurusha matangazo na badala yake wanapata matangazo ya redio toka nchi jirani ya Malawi:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza uwezo wa kurusha matangazo ya kituo cha TBC- Songea ili wananchi wa Tarafa hizo wapate habari kupitia TBC?

Name

Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Answer

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Martin Alexander Mtonda Msuha, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, matangazo ya Radio ya Taifa kupitia mtambo wa masafa ya kati yaani Medium Wave yenye nguvu ya Kilowati 100 yalikuwa yakisikika vizuri katika Wilaya mbalimbali za Mkoa wa Ruvuma wakati mtambo huo ulipokuwa ukifanya kazi. Tangu mwezi Julai, 2013 mtambo huo haufanyi kazi kutokana na uchakavu na hivyo kuathiri usikivu wa matangazo ya TBC katika maeneo kadhaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa wananchi kupata matangazo, TBC ililazimika kuhamisha mitambo yake miwili ya Radio yenye uwezo wa Kilowati moja kwa kila mmoja iliyokuwa imefungwa eneo la Mshangano - Songea na kuifunga eneo la juu la mlima wa Matogoro (Songea) ili angalau usikivu wake usambae eneo kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kufunga mitambo hiyo, matangazo ya TBC- Songea yameboreshwa. Hata hivyo, kutokana na uwezo mdogo wa mitambo ya FM inayotumika kwa sasa mawimbi yake ya sauti hayafiki mbali sana ukilinganisha na yale ya mitambo ya Medium Wave iliyokuwa ikitumika wakati wa awali ambayo yanafika eneo kubwa zaidi la Mkoa wa Ruvuma zikiwemo Tarafa za Hagati, Mbuji, na Mkumbi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kukabiliana na changamoto za usikivu hafifu katika maeneo kadhaa Mkoani Ruvuma, TBC imeshafanya upembuzi yakinifu wa kufunga mitambo ya FM yenye uwezo wa kilowati moja katika eneo la Mbamba Bay lililopo Wilaya ya Nyasa ili kuongeza usikivu wa redio na TBC. Katika bajeti ya mwaka wa 2016/2017, Wizara yangu imetenga fedha za maendeleo kwa ajili ya kufunga mtambo eneo la Mbamba Bay. Kazi hiyo ya uboreshaji wa matangazo katika eneo hilo itaanza mara tu fedha za kununua na kufunga mitambo zitakapotolewa.