Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 5 Good Governance Ofisi ya Rais TAMISEMI. 48 2016-02-01

Name

Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Primary Question

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE aliuliza:-
Serikali katika awamu zote imekuwa ikiweka kipaumbele katika sekta ya Kilimo na Mifugo kwa umuhimu wake kwa maendeleo ya wananchi katika nchi yetu, lakini Wilaya ya Kilwa kama ilivyo katika maeneo mengine ya nchi yetu, imekuwa na migogoro inayotishia amani kati ya wakulima na wafugaji katika baadhi ya Vijiji vikiwemo vya Ngea, Kinjumbi, Somanga, Njianne, Namandungutungu na Matandu, kutokana na wafugaji kupitisha, kulisha, kunywesha na kuharibu mazingira katika mashamba ya wakulima na Hifadhi ya Misitu ya Vijiji kama Msitu wa Likonde, Mitarute na Bwawa la Maliwe katika Kijiji cha Ngea, ambacho hakipo katika mpango wa kupokea wafugaji:-
Je, Serikali inatoa wito gani kwa wafugaji wanaoruhusu mifugo yao kuwatia hasara na njaa wakulima na kuharibu mazingira ya baadhi, ili kuepusha uvunjifu wa amani ambao unaweza kutokea wakati wowote kuanzia sasa?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI WA TAMISEMI, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vedasto Edgar Ngombale, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli Wilaya ya Kilwa imekuwepo migogoro ya wafugaji na wakulima, hususan katika Vijiji vya Ngea, Kinjumbi, Somanga, Njianne na Namandungutungu. Ufuatiliaji umebaini kuwa sababu kubwa ya migogoro hii ni baadhi ya wafugaji kuingiza mifugo yao katika mashamba ya wakulima na baadhi ya wakulima kuingia katika maeneo ya wafugaji. Hivyo, migogoro hiyo inatokea panapokuwepo mwingiliano baina ya makundi haya ya wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi iliandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi kwa vijiji 14 vya Wilaya ya Kilwa ambao uliainisha maeneo kwa ajili ya kilimo, ufugaji, biashara, makazi na uwekezaji. Licha ya mpango wa matumizi bora ya ardhi kuandaliwa bado kumekuwa na tabia ya kutofuata sheria ya Ardhi Na. 13 na Na. 14 zote za mwaka 1999 na hivyo kusababisha mwingiliano usio wa lazima.
Mheshimiwa Spika, kutokana na tatizo la migogoro ya wakulima na wafugaji kuwa kubwa, ninawaagiza Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya, wote kuhakikisha kwamba suala hili linakuwa ajenda ya kudumu katika vikao vya Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Mkoa na utatuzi wake ufanyike kwa njia shirikishi. Serikali haitasita kuchukua hatua kwa wale wote wanaokiuka Sheria, vikiwemo vitendo vya rushwa, hali ambayo imesababisha migogoro hii kuendelea kuwepo.